0

 MBUNGE WA MUSOMA VIJIJINI, PROFESA SOSPETER MUHONGO.
MBUNGE wa Musoma Vijijini, Profesa Sospeter Muhongo, amesikitishwa na wizi wa dawa na uharibifu wa baadhi ya vifaa katika Kituo cha Afya cha Murangi, wilayani Musoma na kuagiza wahusika wachukuliwe hatua.
 Muhongo alitoa agizo hilo mapema wiki hii wakati akikabidhi msaada wa vifaa mbalimbali vya afya, vikiwamo vitanda maalumu 10 na baiskeli za wagonjwa vilivyotolewa na wafadhili kutoka Australia kwa ajili ya kituo hicho.

Kabla ya makabidhiano ya vifaa hivyo, alipokea taarifa kutoka kwa wananchi kuhusiana na wizi wa dawa uliomhusisha mlinzi wa kituo hicho na kuharibiwa kwa gari la wagonjwa alilokabidhi Machi, mwaka huu.

Taarifa hizo zilimkasirisha Profesa Muhongo, ambaye pia ni Waziri wa Nishati na Madini, hivyo kuagiza wahusika wote wachukuliwe hatua ili iwe fundisho kwa wenye tabia za namna hiyo.

Akizungumzia gari hilo, Profesa Muhongo alisema lililotolewa na serikali ya Japan kwa ajili ya wananchi wa jimbo la Musoma Vijijini ili kusaidia kuondokana na usumbufu waliokuwa wakiupata.

Mbali na gari hilo, alisema serikali ya Japan ilimwahidi magari mengine zaidi ikiwa gari hilo litatunzwa vizuri na kutumika kwa shughuli iliyokusudiwa.

“Hii ni aibu kubwa. Hata wafadhili watatushangaa na kutucheka, dawa nyingi tulipewa na wafadhili na gari lile tulikabidhiwa likiwa bado jipya na kwa Tanzania magari ya namna hiyo yapo mawili tu, ni hapa na Muhimbili,” alisema.

Aliongeza kuwa serikali ya Japan ilitoa Sh. milioni 170 kwa ajili ya kuboresha kituo hicho cha afya na kuongeza kuwa atamwomba Balozi wa Japan nchini kufanya ukaguzi wa matumizi ya fedha hizo.

Profesa Muhongo aliwaagiza madiwani kufuatilia ili kubaini hatua iliyofikiwa ya matumizi ya fedha hizo na kwamba endapo itadhihirika kuna ubadhirifu wa aina yoyote, hatua za kisheria zichukuliwe ikiwa ni pamoja na kurejesha fedha hizo.

Alisema anashangazwa kupewa taarifa hizo na wananchi huku viongozi wakiwa kimya bila kuonyesha hatua walizochukua, hivyo kuwataka madiwani kutokuwa waoga katika kuwachukulia hatua wanaofanya ubadhirifu.

Pia aliwaagiza Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Dk. Thadeus Makwanda, na Kaimu Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya cha Murangi, Dk. Josephat Karambo, kuhakikisha hadi Januari 15, mwakani, gari hilo liwe limetengemaa.

Post a Comment

 
Top