1
Kabla hajajulikana na kuwa mtu maarufu kama hivi leo, mtu huyu aliwahi kupambana na hali ngumu ya maisha ili kufikia mafanikio aliyokuwa akiyatarajia daima. Namzungumzia si mwingine bali ni Walt Disney ambaye ndani ya mwaka 1919 aliwahi kufanya kazi na mojawapo ya gazeti la habari na kwa muda mfupi akafukuzwa kazi na bosi aliyemwajiri baada ya kukosa maono na mawazo ya ubunifu katika kazi.
Mwezi Januari 1920, Disney kwa mara ya kwanza aliweza kuanzisha kampuni yake ya muda mfupi inayojihusisha na masuala ya sanaa hasa katika utengenezaji na uchoraji wa picha za katuni. Hata hivyo, pamoja na kujituma katika kuanzisha kampuni yake ya kwanza, aliendelea na kazi iliyokuwa ikimpatia fedha zingine za pembeni katika kampuni iliyojulikana kwa jina la Kansas City Ad. Hakuishia hapo tu kwani baada ya muda mfupi aliweza kuanzisha studio yenye mafanikio makubwa, lakini haikuweza kuwa na faida ya kujitosheleza katika kuwalipa wafanyakazi mshahara mzuri. Na katika muda mfupi kampuni yake iliingia katika madeni hata kufikia hatua ya kushindwa kujiendesha na hatimaye kufilisika.
Lakini kushindwa haikuwa sababu kwake ya kutokujaribu tena, kwani baada ya hapo Disney aliamua kuanzisha studio katika mji mkuu maarufu wa kutengeneza filamu, Hollywood, California. Na kwa mara nyingine Disney pamoja na mshirika wake Ub Iwerks kwa kupitia studio yake ya Walt Disney, aliweza kutengeneza filamu ya kwanza ya katuni iliyoweza kufanikiwa sana kibiashara na mauzo ijulikanayo kwa jina la Oswald the Lucky Rabbit. Kwa kifupi huyu ndie mtu aliyekuja kufanikiwa sana hata kufikia kushinda tunzo nyingi ndani ya jiji la Hollywood na kupata mafanikio makubwa sana katika tasnia ya uzalishaji filamu, Disney ni miongoni mwa watu waliokufa ingawa wanaishi kwa nguvu ya mawazo yao yaliyokuwa na nguvu ndani yake na yanayoongea hadi leo.
Leo hii studio ya Walt Disney ni miongoni mwa studio maarufu sana ndani ya jiji la Holywood, studio inayozalisha filamu nyingi kutoka kwenye mji huo huku ikiwa si tu kwenye eneo la katuni kwa sasa bali hadi filamu za kawaida. Kama umekuwa mfatiliaji wa karibu wa filamu kadhaa zinazotengenezwa ndani ya jiji la Hollywood basi hautakosa kuona filamu hata mojawapo yenye lebo ya Walt Disney kwa mwaka. Studio hii ndio iliyomzalishia Disney utajiri mkubwa katika kipindi chake alichoishi hadi hivi leo, na hata kufikia kumiliki maeneo makubwa katika nchi nyingi duniani yenye majumba makubwa yajulikanayo kama Disneyland ili kukutanisha watoto na wazazi wao kwa ajili ya michezo mbalimbali.  Jiulize ni mawazo au wazo gani ulilonalo ambalo linaweza kuwa sababu ya kufanya ndoto yako kuwa halisi na kuleta mafanikio makubwa katika maisha yako?
“All our dreams can come true if we have the courage to pursue them.” -Walt Disney
disneyland-3
Haya ndio mambo matatu ya kujifunza kutoka kwa Walt Disney:
1: Haijalishi watu wanakuonaje, ukiamua kuamini uwezo ulionao utafanya mambo makubwa.
Mafanikio yako yapo njiani hata kama hauoni jambo hili kwa wakati huu, kama ukiamua kuamini hadi mwisho uwe na uhakika utaona uhalisi ukitokea. Haijalishi watu wanadharau uwezo mdogo ulionao kwa sasa ila ukiamini unaweza na kuongeza bidii ya kufanya unachokipenda kila siku pasipo kughairisha uwe na uhakika ipo siku utawashangaza watu wengi sana waliokudharau na dunia itafahamu uwezo na mafanikio yako. Usikubali kuwa miongoni mwa watu wale wanaosemwa kidogo tu kisha wanamua kukata tamaa katika kuzifuata ndoto zao, amua kuchukulia kusemwa kama changamoto ya kukupa nafasi ya kuendelea mbele zaidi.
Watu wengi wanapokutana na maneno ya watu huwa ni wepesi wa kukata tamaa hata kuacha kutenda majukumu yao ya kila siku yanayowapelekea kufanikiwa katika ndoto walizonazo. Jiulize kama Walt Disney angeamua kukata tamaa na kusikiliza maneno ya bosi wake wa mwanzo kuwa hana ubunifu hata kufikia kumfukuza kazi, je, leo hii tungepata kumjulia wapi na kujifunza mambo haya mazuri kutoka kwake? Disney alifahamu uwezo wake ndio maana pamoja na kusemwa hakukata tamaa bali alitumia maneno yale aliyosemwa kama sehemu ya kumfanya kuongeza bidii (maneno yalimu- encourage) baada ya kufukuzwa akatumia changamoto hiyo kutambua uwezo mkubwa zaidi alionao hadi alipofanikiwa.

2: Usikubali kufeli mara moja kuwe kizuizi cha kuanza tena.
Mara nyingi huwa tunatamani tupate mafanikio ya haraka yasiyopitia changamoto yoyote ile, na hata pale inapotokea kushindwa katika jambo fulani tunajikuta tunakata tamaa kwa haraka, pasipo kufahamu kuwa hakuna mafanikio yoyote yanayoweza kutokea kwenye maisha yetu pasipo kupitia changamoto nyingi zinazoweza kutuimarisha na kutufanya kuwa imara hapo badae. Kumbuka kila unapojikwaa na kuanguka mahali fulani hiyo ni njia mojawapo ya kukusaidia kupata mbinu na mikakati mipya itakayokufanya uimarike katika kitu unachokifanya.

Maisha yako ya mafanikio yanategemea sana unavyokubaliana na changamoto unazokutana nazo kila siku na kuchukua hatua ya kuzitafutia majibu ili kukuzalia mawazo mapya ya kukupeleka mbele zaidi. Jiulize ulipofeli kwenye jambo ulilokuwa umeanza kulifanya, je, ulikata tamaa kufanya tena au uliamua kurudisha moyo wako nyuma na kurejea kufanya kwa mara nyingine ili kuleta matokeo?

3: Chunguza katika mawazo mengi uliyonayo, amini lipo wazo moja la kukutoa.
Si watu wengi wenye tabia ya kuandika mawazo wanayoyapata kila siku na kuyafatilia kama njia yao ya kutokea na kufanikiwa. Jiulize ni mawazo gani niliyonayo ambayo naweza kuyageuza kuwa fedha na kuleta utajiri mkubwa katika maisha yangu? Chunguza mawazo yako mengi uliyonayo kisha amua kuchagua wazo moja unaloona katika hilo unaweza kulisimamia kwa kutoa nguvu na muda wako mwingi kila siku (focus- concentration) ili kuleta matokeo chanya kwenye maisha yako. Usiruhusu mawazo yako uliyonayo muda huu kupita pasipo kuyachunguza na kuyachukulia hatua za kivitendo ili kuzaa mafanikio halisi katika maisha yako.
Leo hii amua kuanza kuorodhesha mawazo yote uliyonayo katika kitabu chako (ideas book), kisha chagua wazo moja unaloona kwa kupitia hilo unaweza kulitekeleza kwa haraka kulingana na mazingira uliyonayo kwa sasa. Fanya utafiti kama hatua ya awali inayoweza kukusaidia kufahamu kama wazo lako linaweza kutekelezeka (applicable) kwenye mazingira uliyonayo, huku ukiweka nguvu kubwa ya kufahamu soko la kitu unachotaka kufanya. Usijaribu kuanza kufanya biashara au jambo lolote lile pasipo kufahamu soko la bidhaa au huduma unayotaka kutoa. Chunguza soko la wazo ulilonalo kisha amua kuwekeza nguvu na muda katika utekelezaji baada ya kufahamu nguvu ya wazo lako ndani ya soko.
JIAMINI NA AMINI UNAWEZA. ISHI NDOTO YAKO.
“Money doesn’t excite me my ideas excite me.” -Walt Disney
disneyland-1

Post a Comment

  1. JAMANI NAOMBENI MSAADA WA HIZO KATUNI ZINAVOCHORWA KAMA NI KWENYE COMPUTER AU KARATASI

    ReplyDelete

 
Top