0
Lindi Yetu


Faith Nipwapwacha
  Na. Ahmad Mmow, Lindi.
Tabia ya baadhi ya wanaume kushindwa kuwapa ushirikiano wake zao wanapokuwa wajawazito imetajwa kuwa inachangia vifo kwa akina mama wajawazito na watoto wachanga.
 
Hayo yameelezwa leo na muuguzi msitahafu, Faith Nipwapwacha katika siku ya kwanza ya warsha ya siku mbili kuhusu namna ya kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga.

Nipwapwacha ambae alikuwa ni miongoni mwa wawezeshaji wa warsha hiyo alikemea tabia ya baadhi ya wanaume kuwazuia wake zao kuhudhuria kliniki na kuwapa huduma za msingi wanapokuwa wajawazito.

Badala yake wanakuwa wepesi wa kuchangia na kuandaa gharama za mazishi pindi vinapotokea vifo vya akina mama na watoto wachanga. Alisema vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga vinaweza kuepukika iwapo jamii hasa wanaume wakibadili mtazamo. Kwasababu vifo vingi vinatokana na sababu zinazoweza kuzuilika.

Akibainisha kuwa kuwasaidia akina mama wajawazito ni hatua muhimu katika kupunguza vifo hivyo. Hata hivyo uzoefu unaonesha baadhi wanaume nikwazo katika kuwafanya wake zao kihudhuria kwenye vituo vya kutolea huduma za afya. Badala yake wanakuwa na huruma na kuonesha upendo kwa maiti kwa kufanya gharama kubwa za mazishi.
"Utawaona akinababa wamejazana kwenye gari kufuata maiti ya mama mjamzito, wanachingia pesa nyingi kwa ajili ya mazishi, lakini mama huyo angekuwa anahudhuria kliniki asingepoteza maisha," alisema Nipwapwacha.

Alibainisha kwamba alipokuwa mtumishi wa umma kwa nafasi yake ya uuguzi alibaini kwamba vifo vingi vya akina mama wajawazito na watoto wachanga vinasababishwa na kukosa mahitaji ya msingi, ambayo kwa kiasi kikubwa yanapatikana kirahisi katika maeneo wanayoishi na kwenye vituo vya kutolea huduma ambako wangeweza kupata ushauri na baadhi ya dawa. Ikiwamo vidonge vya kuongeza damu.

Huku akitoa wito kwa jamii kuguswa na vifo hivyo na kutambua kuwa kuwasaidia wajawazito ni njia bora ya kuokoa uhai wao. Badala ya kuona ni jambo la kawaida.

Alisema jamii inawajibu wa kuchangia mahitaji ya msingi kwa wajawazito wanapokaribia kujifungua.
"Akina mama wengine wanafariki kutokana na upungufu wa damu, lakini jamii inauwezo mkubwa wa kuondoa tatizo hilo iwapo itachangia. Lakini pia vijiji vingine havina zanahati na wanaume wengine uwezo wao ni mdogo, maeneo kama hayo kuna umuhimu wa kuchangia gharama za usafiri kumfikisha zahanati badala ya kusubiri kuchangia kwa ajili ya kurudisha maiti," aliongeza kusema Nipwapwacha.

Kwa upande wake mkurugenzi wa kituo cha msaada wa kisheria kwa wanawake na watoto mkoa wa Lindi (LIWOPAC), Cosma Bulu, aliwaasa akina mama wazitambue haki zao, wazidai na wapaze sauti pindi wanapoonewa na kunyanyaswa na waume zao.

Akibainisha kuwa akina mama wengi wanadhulumiwa haki zao. Hata hivyo wanashindwa kulalamika na kuomba msaada. 

Warsha hiyo ya siku mbili inafanyika katika manispaa ya Lindi na kuwashirikisha baadhi ya wananchi wa vijiji vilivyopo kata za Nyangamara, Milola na Nangaru yameandaliwa na LIWOPAC kwa ufadhili wa shirika la kuhudumia asasi za kiraia (FCS).

Post a Comment

 
Top