0


        RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein amesema kuwa si vyema misikiti kuwa chanzo cha mizozo, mivutano na migongano na badala yake iwe sehemu ya kuwaunganisha Waislamu kwani hayo ndio mafunzo ya Mtume Muhammad (S.A.W).

Dkt. Shein ameyasema hayo jana mara baada ya ufunguzi wa masjid Muhammad (S.A.W) uliopo Fujoni Mzambarauni, Wilaya ya Kaskazini B, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Akitoa nasaha zake kwa waumini wa dini ya Kiislamu wa Fujoni na vijiji vya karibu, Dkt. Shein ameeleza kusikitishwa kwake na tukio lililofanywa na  baadhi ya waumini wa Kiislamu hivi karibuni huko kisiwani Pemba la kuchoma moto msikiti, kuiba mashine ya kupandishia maji sambamba na baadhi ya waumini kubaguana katika baadhi ya misikiti. 

Amesema kuwa misikiti ina mchango muhimu katika kuwaunganisha wanajamii wanaosali pamoja na huwapelekea kujuana na kushirikiana katika masuala mbali mbali na kusisitiza umuhimu wa kuitunza misikiti ukiwemo msikiti huo mpya ambao una sifa zote.


Dkt. Shein amesema,  kuwapatia watoto elimu ni jukumu la kila mzazi, hivyo wazazi pia wanapaswa kuwa na ushirikiano na walimu kwa kila hali ili wapate moyo wa kuitekeleza kazi yao ambayo inajulikana kuwa ni ngumu.
Aidha alitumia fursa hiyo kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu wale wote walioshiriki katika ujenzi wa msikiti huo azidi kuwafunguliwa milango ya riziki bna watilie baraka katika kufanya shughuli zao.
Nae Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Mahonda  Alhajj Balozi Seif Ali Idd, ameeleza juhudi zilizochukuliwa katika kuhakikisha mfadhili wa ujenzi wa msikiti huo anapatikana ikiwa ni pamoja na kutimiza ahadi yake ya kutafuta mfadhili wa msikiti huo.

Nao wananchi wa Shehia ya Fujoni katika risala yao walieleza  furaha yao kwa kujengewa msikiti huo mpya ambapo walieleza kuwa hapo kabla msikiti uliokuwepo ulikuwa haukidhi haja kutokana na udogo wake, uchakavu sambamba na kwenda masafa marefu kufuata misikiti kwa ajili ya sala za Idd na Ijumaa.

Viongozi mbali mbali wa Serikali, viongozi wa dini ya kiislamu, wananchi na wageni kutoka ndani na nje ya Zanzibar walihudhuria katika ufunguzi huo wa masjid Muhammad (S.A.W).

Post a Comment

 
Top