0
Pangani. Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais  Mazingira na Muungano,  January Makamba amesema mradi wa kudhibiti mabadiliko ya tabianchi katika Mji wa Pangani uko mbioni kuanza.

January amesema mradi huo unalenga kudhibiti maji ili mjini huo ‘usimezwe’ na Bahari ya Hindi na kwamba utaanza hivi karibuni kwa gharamu ya Sh3 bilioni.

Waziri huyo amesema hayo wakati akikagua eneo  litakalojengwa ukuta wa Mto Pangani  ambalo limeathiriwa na mabadiliko ya tabianchi.

January amesema Pangani inakabiliwa na changamoto ya kipekee kwa sababu dalili zinaonyesha mji huo unakwenda chini ya kina cha maji ya bahari.

Amesema mradi huo unaotekelezwa na Ofisi ya Makamu wa Rais, ulibuniwa mwaka 2009  lakini haukuanza kwa sababu fedha zilikuwa hazitoshi.

Mkurugenzi wa Mazingira,  Ofisi ya Makamu wa Rais, Richard Muyungi amesema wameshakamilisha mchakato wa  kupata mkandarasi wa nje na anahitajika  mmoja  tu kwa sababu atashirikiana  na  kampuni  za ndani ya  nchi.

Post a Comment

 
Top