0
Never Giver Up 3
Ni hakika kabisa ili mtu afanikiwe kwenye ndoto yake aliyonayo ni lazima awe na kiwango cha juu sana cha njaa au shauku (to be hungry) ya kufikia ndoto yake; huwezi kufikia mafanikio makubwa sawa na unavyotaka kama ndani yako hauna shauku ya kutosha ya kukufikisha kwenye mafanikio hayo unayoyahitaji. Wenye njaa ya mafanikio ndio wanaoteka miliki na nguvu za dunia; angalia wafanyabiashara wakubwa na wanasiasa wakubwa duniani; hao wote na wengine wengi ukifatilia historia zao utakuta pamoja na kupitia misukosuko mingi juu ya kufikia ndoto zao lakini hawakukata tamaa ya kufuata na kuishi ndoto zao walizonazo. Ndani yao njaa ya kufanikisha ndoto zao haikuzuiwa na kitu chochote kile mbele yao bali walijitoa kwa dhati hadi kufikia hapo tunapowaona leo hii.
Nipo wazi kukuambia kuwa leo unahitaji njaa au shauku ya kutimiza ndoto yako kwa kiwango cha juu sana kila siku ili uweze kuona matokeo makubwa unayoyahitaji katikati ya maisha yako. Kumbuka watu wenye njaa ya mafanikio na kutimiza ndoto zao huwa hawachoki mapema njiani ni watu wenye hatua endelevu za kufuata ndoto zao (Unstoppable people); ni watu wasiokoma kutengeneza picha mpya kila siku kwa ajili ya maisha yao ya badae (Imagination people); hawachoki kutafutafuta wanachokitaka (Uncommon people); ni watu wasiokata tamaa (refuse to give up); si watu wenye kutoa sababu mbalimbali katika kuchukua hatua (no excuse is acceptable to them); ni watu wenye kufanya vitu ambavyo wengi leo hawavifanyi ili kesho wawe na maisha ambayo wengi watakuwa hawana.
Sababu 5 zifuatazo kwa nini unapoteza njaa au shauku ya kufanikisha ndoto yako:
1: Unapenda kuishi maisha ya watu wengine.
Kuna watu ni rahisi sana kuishi maisha ya watu wengine kuliko kuishi maisha ya ndoto zao binafsi. Hii imekuwa ni sababu kubwa ya watu wengi kuwapelekea kukata tamaa haraka pale wanapoona wamezidiwa viwango fulani vya kimaisha na watu wanaowatizama. Kuwa na mtu unaweza kumtumia kama mfano (role model) kwenye maisha yako si vibaya, ila ni mbaya sana pale unapotaka kulingana na mtu huyo kwa muda mfupi huku haujui mtu huyo amepitia magumu mangapi hadi akafikia hatua hiyo aliyopo leo. Unahitaji kubadilika na kuishi maisha yako binafsi na si maisha ya mtu mwingine.
Acha kuiga maisha ya watu wengine na kuyaishi, kwani huko ni kujishusha na kutokutambua uwezo mkubwa Mungu alioweka ndani yako. Kuna watu wengi leo wameingia kuimba kwa ajili ya kuona watu fulani wanaimba hatimaye wanapofikia mahali fulani na kuona wanapwaya katika kitu walichokimbilia wanarudi nyuma na kukata tamaa, inakubidi utafute kusudi na wito wa kwako duniani; usifanye mambo kwa kufuata watu wengine wanavyofanya. Usiende kuimba kisa umemwona mtu fulani anaimba na kukubalika, usiwe mwandishi kisa umeona kuna mtu mwandishi anafanya uandishi na anakubalika; chunguza kipaji chako na amua kukitumia kwa ufanisi ili ufikie viwango vya juu unavyovitaka binafsi.
2: Haujiamini na Unajilaumu binafsi kwa kila kitu.
Hofu na mashaka pamoja na kujilaumu binafsi juu ya kila kitu unachofanya ni mojawapo ya tabia inayoweza kuwa sababu kubwa ya kupoteza njaa na shauku ya ndoto yako. Unapofanya jambo fulani na kukosea au usipolifanikisha kama ulivyokuwa unataka, huo si wakati mzuri kwako wa kuanza kujilaumu na kupoteza imani juu ya uwezo wako ulionao, bali unachotakiwa ni kujifunza kutokana na makosa hayo na kukubaliana na hali hiyo ili uweze kuchukua hatua mpya zaidi itakayokuwezesha kuwa bora zaidi kuliko mwanzo. Unapojilaumu binafsi kwa hatua ndogo na ya mwanzo uliyoshindwa kufanikisha, unakuwa unaifunga akili yako isipate kuona milango mingine ya kukusadia kutoka na kufanikisha jambo husika.
Chunga tabia ya kujilaumu bali kubaliana na matokeo madogo uliyoyapata hata kama hayajakutosheleza sawa na ulivyokuwa ukitaka. Kumbuka wewe unauwezo mkubwa sana ndani yako kuliko jinsi unavyofikiri, unahitaji kufanikisha ndoto yako na si kukata tamaa mapema; jiamini na amini unaweza zaidi sana ishi ndoto yako.
3: Unaridhika mapema sana.
Watu wengi sana wanapopata mafanikio kidogo tu kutokana na hatua fulani wanazochukua katika malengo na mipango waliojiwekea, basi watu hawa wanaridhika haraka na kusahau kabisa ndio kwanza pamekucha. Ndio. hapo ndio kwanza pamekucha. Huwezi kuanzisha biashara leo baada ya kuona wateja wamekuwa wengi basi ndio uridhike kwa kisa cha wateja kuwa wengi kwako unaanza kudharau wateja wengine, tambua huko ni kukosa nidhamu na kwa mtindo huo hautochukua muda mrefu utapoteza wateja wote na sifa nzuri zote ulizokuwa nazo hapo mwanzoni.
Acha kuridhika mapema kwa unachokipata, tambua mafanikio hayana mwisho ni jinsi wewe utakavyoamua kundelea kupigania ndoto yako ili ufikie kipimo cha juu kabisa ambacho Mungu amekwisha kukupimia tangu ukiwa tumboni mwa mama yako. Una uhalali wa kuwa na kiwango cha juu sana cha mafanikio bila serikali yoyote duniani kukuingilia kama ni mafanikio yaliyotokana na njia halali kabisa. Acha kuridhika mapema, na kama ni hivyo basi Bill Gate na mabilionea wengine wote duniani wasingefikia hapo walipo; acha kujipimia kiwango kidogo nje ya kile Mungu alichokupimia tumboni mwa mama yako.
“Una haki ya kutajirika ilimradi unafanya shughuli halali. Hakuna mwenye haki ya kukupimia kiasi cha utajiri halali Mungu aliokupa.”
Reginald Mengi
4: Unapenda kufanyiwa kila kitu. Hautaki kuchukua hatua mwenyewe.
Angalia mara ngapi linapotokea suala la kulichukulia hatua huwa unachukua hatua haraka mwenyewe pasipo kutaka mtu mwingine akufanyie? Hilo ni swali kwako. Kuna watu kwenye maisha yao ni kama vile hawana viungo vyote vya mwili; hawa ni watu wenye kupenda kufanyiwa kila kitu na watu wengine hata vile ambavyo vilitakiwa kufanyika na wao binafsi na vilivyo na umuhimu mkubwa kwao. Kumbuka kuwa,“kufanyiwa kila kitu na mtu mwingine ni kuchagua kulaumu na kuumia kwa maumivu mengi.”
Punguza tabia ya kupenda kufanyiwa kila kitu hata ambacho kipo kwenye uwezo wako wa kukifanya binafsi. Unapofanyiwa kila kitu unaweza ukawa umechagua kufanyiwa vitu chini ya kiwango ambacho ulikuwa unakihitaji; na hapo ndio mwanzo wa kutoa malaumu na kusababisha kupoteza shauku ya kufanya upya jambo husika. Acha mara moja tabia hii na amua mara moja kupenda kuchukua hatua mwenyewe ili uweze kufikia mafanikio makubwa unayoyataka juu ya ndoto yako.
5: Umekata tamaa mapema.
Je, umekata tamaa mara ngapi kwenye kuifaata ndoto yako? Usikubali kukata tamaa mapema hivi kwenye kuifata ndoto yako ya maisha. Kukata tamaa mapema kwenye ndoto yako ni kuruhusu kupoteza kila kitu ulichokianza na kuamua kuishi maisha yaliyo chini ya kiwango chako. Usikubali kukata tamaa juu ya ndoto yako (Never giver up on your dream).
Fanya zoezi hili:
1: Andika changamoto 5 unazoona zinakuzuia kuifata na kuishi ndoto yako sawa na unavyotaka.
2: Tumia changamoto hizo kama faida ya kukupa matokeo mapya na makubwa baada ya kuchukua hatua juu yake.

Post a Comment

 
Top