0


Kama kuna kitu bora ambacho mtu yoyote anayehitaji kufanikiwa anatakiwa akichague na kukisimamia ni kuwa na msimamo wa kuishi katika ndoto yake pasipo kuyumbishwa na upepo wa aina yoyote ule unaokuja mbele yake. Ni muhimu sana kuishi katika ndoto yako, kwa kuiamini na kuifuata kwa ujasiri ndio nyenzo tosha ya kukuletea mafanikio makubwa katika maisha yako.
Utafiti unaonesha watu wengi waliofanikiwa na kuwa na mafanikio makubwa katika hii dunia tangu enzi na enzi, ni wale walioamua kuchagua kufanya jambo moja kwa kujitoa na kuliamini pasipo kusikiliza mazingira ya nje yalikuwa yanatoa mchango hasi wa kuwazuia kuendelea mbele. Ukisoma vizuri katika kitabu cha Think and Grow Rich Book kilichoandikwa na mwandishi mahiri na mashuhuri wa enzi hizo Bwana Napoleon Hill. Bwana Hill anajaribu kutoa kanuni kubwa na ya kwanza ya mtu anayehitaji kufanikiwa ni kuwa mwenye uhitaji (Desire of Something).
Uhitaji wako ndio unaokusukuma kutegemea mafanikio katika eneo fulani unalohitaji uone mafanikio hayo kwa hali ya uhalisi. Hebu fikiria kwa muda huu ni kitu gani unachohitaji ukipate au ukifanikishe katika maisha yako kabla ya kuondoka hapa duniani. Wakati ukifikiria hivyo, hebu tazamia kama hakuna jambo lolote linaloweza kukuzuia kufanya hivyo na ukiweka imani kuwa inawezekana kutokea na wewe kufikia katika eneo hilo kwa haraka.
Hebu jiulize binafsi wewe kama wewe katika Maisha yako una ndoto gani? Una jambo gani unalotamani kulifanikisha na likaleta matokeo chanya na makubwa kwenye maisha yako na ya watu wengi waliokuzunguka? Kama una ndoto ya kuwa mfanyabiashara au mwekezaji mkubwa kama Dangote unazani ni rahisi; ni lazima ujitoe kikweli kweli ili kufikia katika eneo hilo, lakini fahamu kuwa inawezekana kabisa kufikia hapo.
Hizi ndio njia 4 ambazo unaweza kuzitumia kwa ajili ya kukusaidia kufikia ndoto yako kwa uharaka zaidi hasa kwako wewe uliyekwisha kutambua ndoto na maono ya kuishi kwako duniani ni nini. Tumia njia hizi katika maisha yako ya kila siku naamini utaona matokeo makubwa ambayo hukuwahi kuyategemea kutokea.
1: Chukua hatua ya haraka kuifuata ndoto yako.
Kwa nini uogope kuifuata ndoto yako? Yawezekana ndoto yako ni kuanzisha kampuni kubwa ya uzalishaji wa vyakula kama bakhresa, lakini bado hujiamini kama utaweza kufanya hivyo. Mimi nataka kukuambia UNAWEZA kama ukiamua kuchukua hatua kidogo kidogo hakika utaona matokeo makubwa muda si mrefu na dunia itakutambua kwa hilo.
Watu wengi wanatamani mambo makubwa na kuwa wenye maono makubwa maishani mwao, ila watu hawa si wenye kutaka kuchukua hatua madhubuti ya kivitendo katika kufikia katika maono na ndoto zao. Hofu na mashaka ndio imekuwa chanzo cha wengi kushindwa kuchukua hatua; hebu amua leo kuondoa hofu na mashaka ndani yako na amua kuchukua hatua ya kuifuata ndoto yako, utafanikiwa.
2: Ondoka katika Mazingira Hasi.
Mazingira hasi yawezekana ni mazingira hasa ya watu; mazingira yasiyotoa mchango wowote wa kukusaidia kutimiza ndoto yako. Kuwa mbali na watu wenye mawazo hasi (marafiki wataabishaji) wakati wote dhidi ya kile unachotaka kukifanya na kukiamini kwenye maisha yako. Jifunze kuchuja mchele na mawe ili uwe bora katika eneo lolote lile; usikubali kuvunja meno yako kwa kula mawe kisa watu.
Wapo watu kazi yao kubwa ni kuwarudisha wengine nyuma badala ya kuwatia moyo kwa kila hatua nzuri wanayochukua. Usikubali kukatishwa tamaa iwe na watu waliokuzunguka au hata mazingira mengine binafsi yanayokupa picha ya kushindwa katika kuitumikia ndoto yako. Amini katika ndoto yako na shikilia ndoto hiyo hadi mwisho utafanikiwa kwa wakati wake.
3: Tafuta mchango wa watu wengine.
Jifunze kuwa karibu na watu wenye mawazo chanya na wale wenye uwezo wa kutoa mchango mkubwa kwenye ndoto ya maisha yako. Tengeneza kundi lako maalum mnaoendana (mastermind group) kimawazo na wenye wivu wa mafanikio na pia mnaoweza kushirikiana katika kufikia mafanikio makubwa. Hapa mtatiana moyo kila wakati na kupeana mbinu mpya kila siku kwa ajili ya kufikia ndoto mlizonazo.
Hii ni njia nzuri na nyepesi sana katika kukusaidia kufanya mambo kwa uharaka na kufikia katika hatua nzuri ya mafanikio makubwa ya ndoto yako. Wapo watu ambao watafurahi kama ukiamua kuwashirikisha jambo zuri ulilonalo au unalotaka kulifanya na watakua tayari kukusaidia kwa hali na mali ili uweze kufanikiwa; amua kuwa na watu wa namna hii na ambatana nao kila siku ili waweze kuwa msaada tosha kwako wa kutimiza ndoto yako. Ukikutana na watu wa namna hii husiwe msiri kwao bali waambie ukweli wa kile unachokitegemea kukifanya maishani mwako.
4: Jifunze kusoma vitabu na kutafuta ushauri.
Hii ndio tabia muhimu sana kwa mtu mwenye shauku kubwa ya kuhitaji kufikia ndoto yake. Ni vizuri ujenge tabia ya kujifunza kutoka kwa watu wengine waliofanikiwa na kukutangulia katika mafanikio waliyonayo kwa kupitia kusoma vitabu, kusikiliza Audio, kuwatizama kwa njia ya video, nakadhalika. Mimi binafsi ni msomaji wa vitabu sana tena sana na kila wiki ninamaliza kitabu kimoja hadi viwili au tatu ikitegemea na ukubwa wa kitabu; na tangu nimeanza kusoma vitabu sijawahi kupungukiwa bali nimefanikiwa kupata mbinu nyingi sana za kunisaidia kufanikiwa zaidi katika maisha yangu.
Tafuta mtu unayemwamini pia aweze kuwa mshauri na muhamasishaji (mentor or coach) wa mambo unayofanya ili kufikia ndoto yako. Wapo watu unaoweza kuwatumia kwenye maisha yako ili waweze kukupa ushauri kwa kila hatua unayotaka kuichukua mbele yako. Unaweza kunitumia hata mimi binafsi kama mshauri wako kama utahitaji kufanya hivyo au kupata kibali kwa jambo hilo.
Nataka nikuambie ni kweli inawezekana kufikia ndoto yako kama UKIAMUA. Amua leo hii ili uboreshe kesho yako. Nakupenda na wote tupo kwenye kundi moja la kutafuta kutimiza ndoto zetu. Karibu sana katika mtandao huu na usichoke kuutembelea kila siku kwa makala zenye mafunzo mazuri ya kukuhamasisha.
Kama unahitaji ushauri au nami kuwa mshauri wako katika maeneo tofauti unayohitaji mafanikio. Wasiliana nami kwa mawasiliano haya yafuatayo.

Post a Comment

 
Top