0


BEI ya mafuta ghafi katika soko la dunia imepanda kutoka Dola 30.77 za Marekani kwa pipa hadi kufikia Dola 40 ikiwa ni kwa mara ya kwanza tangu Desemba mwaka jana.

Taarifa iliyotolewa juzi na Shirika la Habari la Marekani, CNN ilionesha bei hiyo imepanda kwa asilimia 54 ikiwa ni wiki tano baada ya kushuka hadi Dola 26.05 kwa pipa.

“Soko linakuwa sana. Tunaweza kuendelea kuona hali tete,” alisema Mkurugenzi wa timu ya nishati huko Nasdaq, Tamar Essner.

Mafuta hayo yamepanda Jumatano ya wiki hii huku wazalishaji wakuu wakiongozwa na Saudi Arabia na Urusi kukubaliana kukutana Doha- Qatar mwezi ujao kujadili masuala ya mafuta.
“Sidhani kama hili limejikita katika misingi. Bado tuko juu ya usambazaji. Tuko katikati ya mchakato wa kuliweka sawa na hilo linachukua muda,” alisema Essner.

Hapa nchini mmoja wa watendaji wa ndani ya Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura) ambaye hakutaka jina lake liandikwe kwa sasa alisema bei hiyo inaanza kutumika baada ya miezi miwili.

“Kama mafuta yakiagizwa leo (jana) basi bei hiyo itaanza kutumika Mei 18, mwaka huu kwani bei zinabadilika kila baada ya miezi miwili. Hiyo ni crude oil (mafuta ambayo hayajachakatwa),” alisema.

MTANZANIA Jumamosi lilimtafuta kwa njia ya simu Kaimu Mkurugenzi wa Waagizaji wa Mafuta ya pamoja hapa nchini, Michael Mjinja ambaye alisema utaratibu uliopo hapa nchini ni kuagiza kila mwezi na kwamba mafuta yanayoagizwa ni yale yaliyochakatwa ambayo pia bei yake inabadilika kulingana na soko hilo.

“Ikipanda kwenye soko la dunia impact yetu ni baada ya miezi miwili, hatununui mafuta ghafi tunanunua mafuta safi, bei nayo inabadilika,” alisema Mjinja.

Alitoa mfano kuwa bei ya mafuta ghafi juzi ilikuwa pipa moja ni Dola za Marekani 40.035 na bei ya jana inapatikana leo.

“Machi 16 mwaka huu mafuta ghafi ilikuwa dola za Marekani 38.705, ilipanda karibia dola 1.3, kwa upande wa mafuta ya petroli ambayo tunaagiza Metric Tani na diseli ambayo inanunuliwa kwa pipa ni dola 46.85,” alisema Mjinja.

Hivi karibuni kuliibuka sintofahamu baada ya Ewura kusema kuwa mafuta yaliyoagizwa bila ya kushindanisha zabuni ndiyo yanayosababisha bei ya soko la ndani isishuke kadiri inavyotakiwa huku Waziri George Simbachawene ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini akisema alichukua uamuzi huo kutokana na wasiwasi wa usalama wa nchi baada ya kumalizika kwa uchaguzi mkuu.

Simbachawene ambaye hivi sasa ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Tamisemi) akiwa katika Serikali iliyopita aliagiza kununuliwa kwa mafuta hayo kwa Sh bilioni 40 kwa matumizi ya Septemba, Oktoba na Novemba mwaka jana bila ya kushindanisha zabuni zilizokuwa mezani.

Post a Comment

 
Top