Historia ya Mgonjwa
Mnamo tarehe 9 Agosti 2015, mgonjwa mwenye umri wa miaka 39 kutoka katika kambi
ya wakimbizi ya Nyarugusu alipokelewa katika hospitali ya Mkoa wa Kigoma Maweni
akiwa na dalili za kutokwa na damu sehemu mbalimbali za mwili hasusan kwenye fizi,
macho na masikio. Vile vile alikuwa na dalili za kuchoka na mwili kuwasha. Mgonjwa
huyu hakuwa na homa. Alipata matibabu katika hospital hiyo na kwa bahati mbaya
mnamo tarehe 10 Agosti, 2015 mgonjwa huyu alifariki dunia. Mgonjwa huyu alikuwa
hana historia ya kusafiri kutoka nje ya mkoa wa Kigoma wala kutembelewa na mtu
aliyesafiri kutoka nchi za Afrika Magharibi zenye ugonjwa wa Ebola.
Mgonjwa huyu alikuwa ni mkimbizi wa kutoka nchi ya Burundi ambaye ameishi katika
kambi ya Nyarugusu kwa miaka mitatu. Mgonjwa huyu alikuwa mmojawapo wa
wakimbizi waliokuwa wasafirishwe katika mpango wa kawaida chini ya Shirika la
Kimataifa linalohudumia wakimbizi kwenda Marekani. Safari hiyo ilikuwa ianze tarehe 9
Agosti 2015.
Hatua zilizochukuliwa
1. Mgonjwa huyu alipatiwa matibabu katika hospitali ya Maweni Kigoma mpaka
mauti ulipomkuta.
2. Uongozi wa Afya Kigoma unafuatilia ndugu wa karibu wa mgonjwa huyu, pamoja
na wahudumu wa Afya waliomuhudumia mgonjwa huyu kuona kama
wataonyesha dalili zinazofanana na ugonjwa aliokuwa nao mgonjwa huyu.
Ufuatiliaji huo umeanza tarehe 9 Agosti 2015. Mpaka leo hakuna mtu mwingine,
aliyeonyesha dalili za ugonjwa huu.
3. Sampuli ya mgonjwa huyu imechukuliwa na kupelekwa kwenye maabara ya
Taifa ya Afya ya Jamii, ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii iliyopo Dar es
Salaam kwa uchunguzi zaidi ili kujua chanzo cha ugonjwa huu.
4. Mazishi ya marehemu huyo yamefanyika chini ya uangalizi wa Afya mkoa, kwa
kuzingatia Utaratibu wa Kanuni za Kimataifa za kuzuia maambukizi.
Hitimisho
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii inapenda kuwahakikishia wananchi kuwa mpaka
sasa, hakuna uthibitisho wowote kuwa mgonjwa huyu amekufa na ugonjwa wa Ebola.
Aidha kwa kuwa ugonjwa bado unaendelea nchi za Afrika Magharibi, Wizara inazidi
kusisitiza wananchi kuchukua tahadhari za kujikinga na ugonjwa wa Ebola na
magonjwa mengine ya kuambukiza. Ikiwa ni pamoja na
o Kuepuka kugusa au kuingiwa na mate, damu, mkojo, jasho, kinyesi, machozi na
majimaji mengine yanayotoka mwilini mwa mgonjwa mwenye dalili za ugonjwa
wa Ebola kupitia sehemu zenye michubuko au vidonda.
o Kuepuka kushughulikia maiti ya mtu aliyekufa akiwa na dalili za ugonjwa wa
Ebola; badala yake watoe taarifa kwa uongozi wa kituo cha kutoa huduma za
Afya kwa ushauri. Wataalam watasimamia maziko ikiwa kifo kitatokea.
o Wananchi waepuke mila na desturi zinazoweza kuchelewesha kupata huduma
muhimu na kuzidi kueneza ugonjwa wa Ebola.
o Kutoa taarifa mapema kwa viongozi wa Serikali na watoa huduma za Afya katika
ngazi zote pale anapotokea mtu mwenye dalili za ugonjwa wa Ebola.
o Kuwahi katika vituo vya kutolea huduma za Afya pale mtu anapohisiwa kuwa na
dalili za ugonjwa huu.
o Kunawa mikono mara kwa mara ili kuepuka kusambaza ugonjwa ikiwa mtu
atakuwa ameshika mgonjwa au mazingira yenye maambukizi.
o Kutumia kemikali za kuua vijidudu kutakasa mikono.
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii itatoa taarifa pindi majibu ya maabara
yatakapopatikana.
BOFYA HAPA KUIPATA TAARIFAA HII
Post a Comment