0
Sukari ya ndani ikipewa uzito, ni dhahiri
Sukari ya ndani ikipewa uzito, ni dhahiri mashamba ya miwa kama hili yataendelezwa na hivyo kuchangia uchumi wa Taifa. Picha ya Maktaba.  

Bajeti ya Serikali ya mwaka 2015/16, iliyosomwa bungeni na Waziri wa Fedha, Saada Mkuya inaainisha mpango wa makusudi wa Serikali wa kuizuia sukari kutoka nje ya nchi kuingia katika soko la ndani kirahisi.
Katika mpango huo, Mkuya anasema kuwa ushuru kwa sukari kuingia nchini utaongezeka kwa zaidi ya mara mbili ya kiwango kilichokuwa kinatozwa mwaka uliopita.
Mtu anaweza kujiuliza, nini maana ya mpango huo? Je una tija kwa wananchi na taifa kwa jumla? Ili kuweza kufahamu vyema hali hii ni vyema ukapata majibu namna mpango huu unavyoweza kutoa manufaa kwa taifa, viwanda na wakulima wa miwa. Kabla ya kujua hayo ni vyema ikafahamika hali halisi ya uzalishaji pamoja na matumizi.
Uzalishaji sukari
Takwimu za Wizara ya Kilimo na Chakula, zinaonyesha kuwa mahitaji ya sukari nchini, kwa matumizi ya nyumbani ni tani 590,000 kwa mwaka wakati uzalishaji ni wastani wa tani 300,000. Uzalishaji huu ni sawa na nusu ya mahitaji.
Hii pekee kiuchumi inaonyesha kuwa zipo fursa za uwekezaji, kuongeza ajira na kuimarisha sekta ya viwanda na kilimo nchini.
Ripoti ya hivi karibuni iliyotolewa na Kampuni ya Nishati na Kilimo cha Miwa ya Agro EcoEnergy (T) Ltd inaeleza kwamba Serikali ikiweka vizuri mipango yake katika sekta ya sukari, inaweza kupiga hatua kubwa ya maendeleo na kupunguza umaskini.
Kwanza inaelekeza kuwa Tanzania ina ardhi ya kutosha inayoweza kuzalisha miwa kwa wingi. Hii ni fursa inayoweza kuwanufaisha wakulima wengi kwa sababu viwanda vitanunua miwa kwa wingi na vitashirikiana na wazalishaji kuboresha zao hilo.
Jambo jingine ni kwamba sekta ya Sukari nchini inajiuza yenyewe kwa sababu soko kubwa lipo, hivyo wenye mitaji mikubwa hawatakuwa na wasiwasi kwamba wanaweza kupata hasara.
Kwa sababu hiyo, Agro EcoEnergy wanaamini kuwa Serikali ikijenga mazingira mazuri, viwanda vya sukari nchini vitakua na kuongezeka na vitaongeza ajira ya maelfu ya watu.
Jambo jingine la faraja katika mpango huo ni kwamba mabaki ya miwa yatakayozalishwa na viwanda yatatumika kuzalisha umeme kwa kuwa ni chanzo kizuri cha nishati hiyo.
Kwa kuwa Serikali tayari imezuia sukari ya nje kuingia nchini kiholela ina maana kwamba sasa mazingira mazuri kwa mpango huo wa Agro EcoEnergy, unaweza kutekelezeka.
Mkurugenzi wa Kiwanda cha Sukari Kagera, Ashwiin Rawa anasema kuwa endapo wananchi wataiona fursa ya kujikwamua kiuchumi iliyopo kwenye sekta hiyo, taifa linaweza kusonga mbele na kujitosheleza na hata kuwa na ziada ya kuuza nje.
Rawa anaeleza kuwa licha ya kiwanda hicho kilichopo chini ya mwekezaji, Super Group of Companies kutilia mkazo kilimo cha umwagiliaji, kinawategemea zaidi wakulima wadogo wanaokizunguka.
Kuyumba kwa bei ya Sukari
Meneja wa Kiwanda cha Sukari Mtibwa, Hamad Yahya anasema kuyumba kwa bei ya sukari nchini kunatokana na wafanyabiashara wanaokwepa kodi na huuza bidhaa kwa bei ya chini.
Kitendo hicho huwasababishia hasara wazalishaji wa ndani, inayotokana na kupata kidogo kuliko gharama za uzalishaji.
Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana alipotembelea Mtibwa wakati akiwa kwenye ziara yake ya kuizungukia mikoa ya Kanda ya Ziwa, anasema katika moja ya mambo ambayo chama kinayahimiza sasa kwa nguvu zote ni lazima uwekezaji uwe ni kwa ajili ya kuwanufaisha wananchi.
“Nimesikia kilio chenu juu ya magendo na naahidi kuishauri serikali ya chama changu kuchukua hatua juu ya jambo hilo ili kuleta manufaa kwa wananchi pamoja na serikali yenyewe,” alisema Kinana.
Mipango ya kinana imekuja kuonekana wazi kwenye bajeti ya mwaka huu, ambayo inaweka mikakati ya kuzuia sukari inayotoka nje, hasa kwa magendo, ili kuimarisha viwanda na kuongeza ajira viwandani na kwa sekta ya kilimo cha miwa.
Kudhibiti sukari ya magendo
Mkutano uliofanyika Morogoro, ukiwakutanisha wadau na Serikali na wadau wa zao la sukari, ilipendekezwa Serikali kudhibiti sukari ya magendo.
Pamoja na hilo, iliafikiwa kuwa Serikali isimamie mfumo mzima wa usambazaji wa bidhaa hiyo nchini ikiwa ni pamoja na kuwadhibiti wafanyabishara wenye tabia ya kuhodhi soko lake kwa lengo la kusababisha upungufu usio halisi.
John Mzee, mkulima wa zao hilo kutoka Kilombero mkoani Morogoro anasema kuwa familia yake imekuwa ikiendeshwa kwa kutegemea kilimo cha miwa kwa muda mrefu.
Anafafanua kuwa kuna wakati wakulima wadogo huzalisha kwa wingi kiasi cha kukosa soko la uhakika hivyo akasema wakulima wengi watafaidika iwapo viwanda vitaongezwa.
Anasema kuongezeka kwa viwanda vya sukari kutahamasisha wengi kuingia katika kilimo hicho na kitawasaidia katika kuongeza kipato na hata utajiri.
“Mimi na ndugu zangu wote tumesoma kupitia kilimo hiki. Ninakifahamu vizuri kwani nimekuwa nashirikiana na familia yangu kukiendesha.
“Kama soko lingekuwa linaeleweka tungekuwa wakulima wakubwa sana. Viwanda viongezwe, ushindani utatufaidisha, tutatajirika,” anasema John.
Serikali sikivu ni ile inayosikiliza wananchi wanataka nini, jambo gani litawafaidisha na kulitekeleza. Bila shaka kitendo cha Serikali kusikiliza kilio na kukiingiza kwenye bajeti kwa mikakati ya utekelezaji ni jambo zuri lenye manufaa kwa taifa.
Kilichobaki ni kuendelea kusimamia utekelezaji kwa kuzuia sukari ya nje kuingia kiholela kwenye soko la ndani. Ni matarajio ya Watanzania kuwa baada ya miaka michache wawekezaji katika sekta ya sukari wataongezeka na ajira za viwandani na kilimo, nazo zitakuwa nyingi na kuwafanya wananchi wengi kuondokana na umaskini.MWANANCHI

Post a Comment

 
Top