Dk Slaa atarajiwa kuchukua fomu kugombea
Fomu za ubunge, udiwani mwisho kutolewa
kesho
Celina Mathew
WAKATI makada wa vyama vya NCCR-
Mageuzi na CUF wakiwa wametangaza
kugombea urais, Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chadema), kimeanza mchakato
wa kumpata mgombea wake wa nafasi hiyo.
Chama cha NCCR-Mageuzi tayari
kimemtangaza Dk. Joseph Kahangwa kuwa
mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania huku Chama cha Wananchi (CUF)
Profesa Ibrahim Lipumba akijitokeza kuwania
kiti hicho kwa mara ya tano.
Kutokana na hali hiyo, Chadema kimesema
mchakato wa uchukuaji na urejeshaji wa
fomu kwa wagombea urais unaanza Julai 20
hadi 25, mwaka huu, na uchukuaji na
urejeshaji fomu za ubunge ulianza Mei 18
hadi Juni 25, mwaka huu.
Ofisa Habari wa Chadema, Tumaini Makene
aliliambia gazeti hili Dar es Salaam jana
kuwa uchukuaji wa fomu hizo za ubunge
unalenga majimbo ambayo chama hakina
wabunge kwa sasa, pamoja na fomu za
ubunge wa viti maalumu.
Makene alisema mchakato wa uchukuaji na
urudishaji fomu kwa ngazi ya ubunge na
udiwani unaendelea vizuri na kwamba
mwisho wa wagombea kuchukua na
kurudisha fomu hizo ni kesho na baadaye
michakato mingine itafuata.
Alisema kwa sasa hana majina ya wabunge
au madiwani waliorejesha fomu kwa sababu
mchakato huo unafanyika nchi nzima.
Alisema wabunge wanarudisha katika
majimbo yao na madiwani katika kata zao.
Hata hivyo, taarifa kutoka ndani ya chama
hicho zinaeleza kuwa huenda Katibu Mkuu
wa chama hicho, Dk. Willbrod Slaa
akagombea nafasi hiyo na ndiye anayepewa
nafasi kubwa.
Katika uchaguzi wa mwaka 2010, Dk. Slaa
alipeperusha vyema bendera ya chama hicho
katika uchaguzi wa rais baada ya kuibuka
mshindi wa pili nyuma ya Rais Jakaya
Kikwete.
Mwaka 2005, Mwenyekiti wa chama hicho
taifa, Freeman Mbowe aligombea kiti cha
urais na kwamba mwaka huu, mwenyekiti
huyo hajaweka bayana kama atarejea
kugombea ubunge katika Jimbo lake la Hai
mkoani Kilimanjaro.
Makamu Mwenyekiti Zanzibar, Salum
Mwalimu ameshachukua fomu za kuwania
ubunge Jimbo la Mkwajuni Zanzibar. Jimbo
hilo ndilo pekee ambalo liliachwa kwa
Chadema baada ya majimbo mengine
kuachiwa CUF chini ya Umoja wa Katiba ya
Wananchi (Ukawa).
Ukawa unaunganisha vyama vya upinzani vya
Chadema, CUF, NCCR Mageuzi na NLD,
vimepanga kusimamisha mgombea mmoja
wa urais katika uchaguzi wa mwaka huu, na
kwamba baada ya kila chama kumpata
mgombea wake watakaa kumchagua mmoja
kati yao kupeperusha bendera ya upinzani.
Tayari Chama Cha Mpinduzi (CCM),
kimeanza mchakato wa kumpata mgombea
wake wa urais kwa makada wake kuchukua
fomu kutafuta saini za wadhamini 450
kutoka mikoa 15. Mpaka sasa makada
ambao wamejitokeza kuchukua fomu ni 40.
Post a Comment