0

 
RAIS JAKAYA KIKWETE
Vuguvugu la kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba limeshika kasi hivi sasa.
Tumeshuhudia baadhi ya wanasiasa wakitangaza nia na tumejionea makundi kadhaa katika jamii yakijitokeza ‘kuwaomba’ wale yanaowaona kuwa na sifa kujitokeza kuomba kupitishwa na vyama vyao kuwania nafasi hiyo ya juu kabisa katika uongozi wa nchi. Kwa vyovyote vile, uchaguzi wa mwaka huu utakuwa na hamasa, msisimko na kila aina ya mbinu kulinganisha na uliopita hasa ikizingatiwa kwamba safari hii Taifa litalazimika kumpata Rais wa Awamu ya Tano.
Hiyo ina maana kwamba ndani ya chama tawala, joto la kumpata mgombea urais halitakuwa kama ilivyokuwa miaka mitano iliyopita kwani hata waliokuwa na nia au tamaa ya nafasi hiyo, walijua fika kwamba wasingeweza kubadili utaratibu wa chama chao kwani Rais Jakaya Kikwete alikuwa amemaliza kipindi kimoja tu kati ya viwili anavyoruhusiwa kwa mujibu wa sheria za nchi.
Safari hii, Rais Kikwete anang’atuka, tumeshuhudia na kusikia kila aina na patashika za wanaCCM wanaowania kumrithi.
Lakini uchaguzi wa safari hii, tofauti na mwingine wowote uliowahi kufanyika chini ya mfumo wa vyama vingi tangu mwaka 1995, tutashuhudia upinzani ulio imara na uliojipanga vizuri zaidi.
Tofauti na miaka iliyopita, vyama vikubwa vya upinzani chini ya mwamvuli wao wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), vimeamua na vimeanza mchakato wa kupata jina moja tu la mgombea urais. Hiyo ikimaanisha kwamba kutakuwa pia na vuguvugu kubwa la wanasiasa kuwania kupitishwa na umoja huo.
Kutokana na sababu hizo tulizozitaja. Tunaamini kwamba hali ya kisiasa katika taifa hasa katika kipindi hiki cha kusaka wagombea siyo katika urais tu, bali ubunge na udiwani itakuwa ngumu na ya wasiwasi mkubwa.
Tayari tumeshaanza kusikia vilio vya rafu kutoka kwa wanasiasa wenyewe kwa wenyewe na hata wananchi, mambo ambayo tunaamini kwamba yasipofanyiwa kazi kwa maana ya kuyadhibiti, hali inaweza kuwa mbaya.
Kwanza, vyama husika vinapaswa kufungua milango na kuruhusu wanachama wake kujitangaza na siyo kutoa ruhusa inayoambatana na masharti na vigezo vigumu.
Tunaamini kwamba hiyo ndiyo njia sahihi ya kumpata rais mwenye vigezo hasa ikizingatiwa kwamba hakuna sifa za kitaifa za kumpata rais wa nchi, ukiondoa zile za vyama hivyo, ruhusa hiyo ingetoa mwanya kwa vigezo vya maadili ya kijamii na utamaduni kutumika kuwachuja.
Lakini pia tunadhani kwamba hiki ni kipindi muhimu cha elimu ya uraia, wananchi wanatakiwa kujengewa uwezo wa kuelewa maana ya ushindani wa kisiasa ambao hautaliingiza Taifa katika machafuko.
Hiki ndicho kipindi cha kuanza kuwajenga wananchi kifikra kuelewa mchakato mzima wa uchaguzi na siyo kusubiri dakika za lala salama.
Lakini pia hiki ndicho kipindi cha kuwajenga wananchi kisaikolojia, kumpokea kiongozi mpya wa nchi ambaye atakuwa na dhamana ya kuliongoza Taifa hili, pengine kwa muongo mwingine mmoja.
Tunapenda kusikia kauli kutoka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), vyama vya siasa na wadau wengine juu ya masuala haya muhimu kwa mustakabali wa taifa hili kwa miaka mingine mitano. Tunachelea kusema kwamba haya yasipofanyiwa kazi kwa makini, patashika hii ya kupata viongozi ikianza tunaweza kujuta.MWANANCHI

Post a Comment

 
Top