Mambo makubwa yanayotarajiwa kuchukua nafasi katika vikao hivyo
vitakavyoanza saa 72 zijazo ni kuwajadili wanachama wake ambao baadhi ni
mawaziri waliokumbwa na kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow na tathmini
ya wanachama wake sita walio katika adhabu ya mwaka mmoja baada ya
kutiwa hatiani kwa kudaiwa kufanya kampeni za urais kabla ya muda.
Pia kamati hiyo, inatarajia kutumia vikao hivyo kuangalia namna ya
kupata wagombea watakaokubalika na wananchi kuelekea kwenye
kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mkuu wa rais, wabunge na madiwani.
Akiwa katika ziara ya kuwashukuru wananchi kwa kuipa CCM ushindi
kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa mkoani Tanga hivi karibuni, Katibu
Mkuu wa CCM, Abdurahman Kinana alisema chama hicho kitaanza rasmi vikao
vyake vya ngazi ya Taifa kupitia masuala mbalimbali yanayokihusu.
Alipoulizwa kuhusu agenda hizo katika vikao hivyo jana, Katibu wa
Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alikuja juu na kusema hakuna kitu
kama hicho… “Hata mkiiandika vibaya CCM, itashinda tu,” na kisha kukata
simu. Hata hivyo, habari zilizopatikana jana jioni kutoka ndani ya CCM,
zinasema kuwa sekretarieti ya chama hicho, inakutana leo mjini Dodoma
kuandaa ajenda za kikao hicho kitakachoanza Jumatatu ijayo.
Mawaziri waliokumbwa na kashfa ya escrow ni Waziri wa Ardhi, Nyumba
na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka ambaye ni pia Mjumbe wa
Kamati Kuu ya CCM.
Profesa Tibaijuka tayari ameondolewa kwenye nafasi yake ya uwaziri
baada ya kukiri kupewa Sh1.6 bilioni na Mkurugenzi wa VIP Engineering,
James Rugemalila.
Wengine waliotajwa kupewa mgawo na Rugemalila ni Mwenyekiti wa Kamati
ya Bunge ya Bajeti, Andrew Chenge na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya
Sheria na Katiba, William Ngeleja.
Pia Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo yupo katika uchunguzi kuhusiana na kashfa hiyo.
Mbali na wahusika wa Akaunti ya Escrow, kikao hicho cha Kamati Kuu ya
CCM kitachunguza maadili ya viongozi wakiwamo waliokumbwa na zuio la
kujihusisha na kampeni kwa miezi 12, huku mienendo yao ya kisiasa
ikifuatiliwa.
Watakaojadiliwa ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi, Teknolojia,
January Makamba, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa na Waziri Mkuu
mstaafu, Frederick Sumaye.
Wengine ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,
Bernard Membe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu),
Steven Wasira na aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini ambaye ni
Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.
Kinana akiwa Tanga alikaririwa akisema: “Wiki ijayo tunaanza kukaa
vikao vya kupimana sisi viongozi juu ya uadilifu wetu ndani ya Serikali,
tunataka kuwa na viongozi wenye kujua Watanzania wanataka nini na
uadilifu wao usiwe hata na chembe ya shaka.”
Alisema salamu za CCM kwa Watanzania kwa mwaka 2015 ni ahadi ya
kuweka mkazo katika maadili kwa viongozi wake na kwamba itafanya
tathmini kwa lengo la kujipanga kwa uchaguzi mkuu ujao.
“Watanzania wanataka viongozi wasiokuwa na urasimu umangimeza, wenye
mlolongo wa itifaki na wanaoweza kushuka chini,” alisema Kinana.
Msingi wa hukumu
Kikao cha tathmini cha wiki ijayo ni mfululizo wa baada ya kikao cha
mwisho cha Agosti mwaka jana kilichokutana chini ya Mwenyekiti wake,
Philip Mangula kupitia taarifa za utekelezaji wa adhabu kwa makada sita
wa chama hicho wanaodaiwa kuanza kampeni kuwania urais kabla ya wakati.
Kufanyika kwa kikao hicho kulitokana na agizo la Mangula ambaye pia
ni Makamu Mwenyekiti wa CCM, alilolitoa Februari 8, mwaka jana akizitaka
ofisi zote za ngazi ya mikoa na wilaya kufungua mafaili kupitia
mienendo ya wagombea walioanza kampeni za uchaguzi wa kuteuliwa kugombea
urais kabla ya wakati. Makada hao waliozuiwa kujihusisha na kampeni kwa
miezi 12 na adhabu zao zinamalizika Februari 18.
Hatua ya kufanyia tathmini hiyo ni kutokana na kuelezwa kuwa pamoja
na adhabu hiyo, baadhi yao walikuwa wakikiuka na kuendelea na mikakati
ya kampeni kwa kukusanya watu wa kupanga nini cha kufanya tayari kwa
uchaguzi wa mwaka huu.
Katika kikao hicho cha Kamati Ndogo ya Maadili na Nidhamu, ilielezwa
kuwa katika kipindi cha miezi kadhaa, timu za maofisa usalama wa chama
zilisambazwa mikoa yote na kukusanya taarifa za makada hao.
Kikao kama hicho cha Kamati Kuu kilikutana Julai 16, mwaka jana na
kupokea taarifa za harakati za baadhi ya wanachama wa CCM walioonyesha
nia ya kuomba ridhaa ya chama kuwania urais.
Kutokana na hali hiyo, Kamati Kuu iliitaka Kamati ya Maadili kufanya
marejeo na kuangalia utekelezaji wa adhabu kwa makada hao sita.
Siku moja baadaye, Julai 17, mwaka jana, Nape alisema endapo Kamati
ya Usalama na Maadili itabaini kama makada hao walikiuka mwenendo wa
utekelezaji wa adhabu waliyopewa, watapoteza sifa… “Baada ya kutafakari
kwa kina, Kamati Kuu inapenda kuwakumbusha kuwa ili wasipoteze nia ya
kugombea ni muhimu wakazingatia katiba, kanuni na taratibu za chama
zinazosimamia masuala hayo.”
MWANANCHI
MWANANCHI
Post a Comment