0

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewataka viongozi ambao wamehusika kuhujumu fedha zaidi ya sh milioni 500 za ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Handeni wajiandae kwenda magereza.
Magufuli ametoa rai hiyo leo alipokuwa katika ziara yake ya siku ya kwanza mkoani Tanga ambapo ameagiza uchunguzi ufanyike na wale wote waliohusika kwenye kuhujumu fedha hizo waanze kuzirudisha au wajiandae kwenda magerezani.
“Nyinyi mnafahamu waliofaidika na hiyo hospitali badala ya fedha kuipeleka kwenye majengo wao wakaipeleka kujinufaisha wao na mimi ni mtumbua majipu nipo hapa leo, Waziri ameshazungumza kwamba atatuma tume ya kuchunguza, tunaomba wananchi wa Kata ya Mkata mshirikiane nao ili majibu yapatikane haraka ili wale waliojinufaisha na hizo fedha waanze kuziandaa kuzirudisha au waanze kujiandaa kwenda gerezani kwa sababu tunataka fedha za Watanzania zisitumike hovyo” alisema Rais Magufuli.
Mbali na hilo Rais Magufuli alitoa siku 15 uchunguzi huo uwe umefanyika na kugundulika viongozi ambao wametumia fedha za ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya Handeni ili hatua zichukuliwe dhidi yao.

Post a Comment

 
Top