RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Zanzibar imepiga hatua kubwa katika mafanikio ya kimaendeleao
Dk. Shein aliyasema hayo huko katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi
la zamani, MnaziMmoja Mjini Zanzibar wakati akifungua Semina ya siku moja kwa
Viongozi na Watendaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu Umuhimu wa
Takwimu na Matumizi yake.
Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa hakuna sababu ya kuyabeza maendeleo makubwa
yaliopatikana hapa nchini lakini kuna kila sababu ya kutatua changamoto ya
kutokuwepo kwa takwimu sahihi katika taasisi za Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar.
Dk. Shein ambaye pia, alikuwa Mwenyekiti wa Semina hiyo, alisema kuwa kutokana
na hali hiyo ndio maana akaona haja ya kuandaliwa mafunzo hayo ambayo
yatasaidia kwa kiasi kikubwa kufikia malengo yaliokusudiwa ambapo mwishoni
yatakuja na maazimio ambayo hatimae yatafanyiwa kazi.
Aidha, Dk. Shein alisema kuwa hakuna jambo lolote la maendeleo linaloweza
kufanyika na kufanikiwa bila ya kuwepo kwa takwimu sahihi na ufanyaji tafiti
huku akisisitiza kuwa upatikanaji wa takwimu sahihi na kwa wakati ni msingi
muhimu katika kupanga na kutekeleza mipango yote ya maendeleo.
Rais Shein alieleza kuwa juhudi mbali mbali zimechukuliwa na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar katika kutatua changamoto hiyo ikiwa ni pamoja na kuunda
Idara ya Sera na Utafiti, Sheria ya Takwimu lakini bado changamoto hizo
zimekuwepo, hivyo aliwataka washiriki wa Semina hiyo kufuatilia kwa makini
mafunzo hayo na kuyafanyia kazi ipasavyo.
Sambamba na hayo, Dk. Shein alisema kuwa kwa upande wa Takwimu Zanzibar
imekuwa ikifanya vizuri na kutumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Ofisi ya
Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Pia, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Katibu Mkuu Kiongozi
na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee,Wizara ya Fedha na
Mipango pamoja na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
kwa kushirikiana pamoja katika kuandaa
Semina hiyo.

Post a Comment