0


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein amesema kuwa uchumi wa Zanzibar umezidi kumeimarika sambamba na Serikali kufanikiwa kuongeza kiwango cha makusanyo ya kodi ambapo kwa kipindi cha Januari hadi Novemba, mwaka 2016 jumla ya sh. bilioni 441.3 zimekusanywa kutoka vyanzo vya ndani. 

Katika risala yake ya kuukaribisha mwaka mpya 2017 aliyoitoa leo kupitia vyombo vya habari, Ikulu mjini Zanzibar Dkt. Shein amesema kuwa kwa kipindi kama hiki mwaka 2015 Serikali ilikusanya Sh. bilioni 336.6 ikimaanisha kwamba miezi kumi ya mwanzo ya mwaka 2016, mapato yameongezeka kwa Sh. bilioni 104.7 sawa na ukuaji wa asilimia 31.1.

Amesema kuwa sambamba na mafanikio hayo, washirika wa maendeleo wamethamini kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya kuwaletea maendeleo wananchi ambapo katika kuthibitisha imani yao kwa Zanzibar, Serikali imepokea jumla ya Sh.bilioni 54.53 kutoka kwa Washirika wa Maendeleo kati ya Januari hadi Oktoba 2016.
Aidha, Dkt. Shein amesisitiza kauli yake aliyoitoa Disemba 10, 2016 katika maadhimisho ya siku ya Maadili kwenye viwanja vya bustani ya Victoria ya kuwataka viongozi wa umma wanaohusika  kujaza fomu kwa kuzingatia maelekezo yaliotolewa kwenye fomu hio na waepuke kutoa taarifa zisizo za kweli kwani kufanya hivyo ni kitendo cha kuvunja maadili ya uongozi. 

Akieleza juu ya amani na utulivu katika kusherehekea mwaka mpya, Dk. Shein amesema Serikali haitosita kumchukulia hatua mtu yoyote au kikundi cha watu kitakachofanya vitendo vinavyohatarisha amani na usalama wa wananchi na mali zao pamoja na wageni wanaoitembelea Zanzibar.

Dk. Shein ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa wananchi wote kushirikiana kukomesha vitendo vya udhalilishaji, amesema ufumbuzi wa changamoto hiyo unahitaji mchango wa kila mmoja na sio Serikali pekee.

Pia, Dk. Shein  ameendelea kutoa wito kwa wananchi kushiriki katika maadhimisho ya miaka 53 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar, yanayotanguliwa na shamra shamra mbali mbali za uzinduzi wa miradi wa miradi na uwekaji wa mawe ya msingi.

Post a Comment

 
Top