0
Siku moja nilibahatika kumsikiliza mwalimu wa masuala ya mafanikio Darren Hardy ikizungumzia hadithi moja iliyonihamasisha zaidi katika kufuata na kutimiza malengo yangu. Hadithi hii ya kuhamasisha zaidi ilimuhusu mmiliki mmoja wa biashara aliyekuwa amepata hasara katika biashara yake, iliyomfanya aingie katika wasiwasi mkubwa kutokana na kutokufahamu hakika ni wapi pakupata tena fedha kwa ajili ya kusimamisha na kuifanya biashara yake kuendelea kusimama.
Katika kipindi hicho cha kujihoji na kutafuta jibu ni wapi pakupata fedha, ghafla alikuja mwanaume mzee sana na kukaaa karibu na mahali alipokuwa amekaa. Mzee yule akamuuliza, kwa nini una wasiwasi mkubwa mwanangu? Mfanyabiashara yule akamjibu yule mzee kwa kumwambia kuhusu uhitaji wake wa haraka wa kuhusu fedha za kuendeshea biashara yake iliyopata hasara kubwa na kutaka kufa. Ndipo yule mzee akasema, ninaweza kukusaidia kwa kukupatia cheki ya hela, kisha tukutane siku kama ya leo mwakani mahali hapa kwa ajili ya kunilipa. Kisha yule mzee hakukawia akaondoka muda ule ule mahali pale.
Baada ya yule mzee kuondoka, ndipo mfanyabiashara yule alipoamua kufungua cheki aliyopewa na kuamua kusoma ndani na ndipo akakuta kiasi cha $500,000 zilizosainiwa chini kwa jina la John D. Rockefeller. Ndio. hakuamini, alikuwa ni John D. Rockefeller aliyekuwa tajiri mkubwa sana duniani wa kipindi hicho ambapo kwa leo hii tunaweza kumpa hadhi ya mtu kama Bill Gates. Kwa mshtuko na furaha kubwa aliyoipata mfanyabiashara yule, hakuamini kabisa kama tatizo la fedha alililokuwa nalo limeondoka kwa ghafla namna ile. Jambo hilo lilimfanya kupata matumaini makubwa na kuwa mtu mwenye shauku kubwa ya kuendelea kufanya biashara yake kwa upya kabisa.
“It takes no more time to see the good side of life than to see the bad.”
-Jimmy Buffett
Aliamua kuchukua cheki ile kisha akaiweka mahali salama pasipo kuibadili katika fedha taslimu bali alihifadhi kama ilivyo hadi yule mzee atakaporudi. Baada ya hapo akajikita zaidi katika biashara yake na kufanya kazi kwa nguvu zote kwa kutumia njia mbadala. Alikuwa tayari kufanya biashara na kuongeza faida zaidi kwa kujikita kwenye mikakati mipya ya kumfanya atengeneze faida zaidi ili kuzuia hasara kundelea kudidimiza biashara yake anayoifanya. Alibaki akishikilia cheki yenye nusu ya milioni dola aliyokuwa amehifadhi pasipo kuitumia wala kuigusa kwa kitu chochote kile.
Baada ya muda kwenda na mwaka mmoja kupita, mfanyabishara yule aliamua kurudi mahali pale alipokutana mara ya kwanza na John D. Rockefeller akiwa na cheki yake mkononi. Mzee yule alijitokeza kwa mbali akija kwa mara nyingine hadi mahali pale alipokaa mfanyabiashara yule. Ndipo mfanyabiashara yule alipoamua kumshawishi mzee yule kupokea cheki yake aliyompatia na kurudisha shukrani zake kupitia msaada wake, lakini ghafla muuguzi mmoja alikuja akikimbia huku akijaribu kumzuia yule mfanyabiashara kutokufanya chochote. Muuguzi yule alisema, mtu huyu (yule mzee) amejaribu kuondoka nyumbani mara kwa mara na kuanza kuzunguka kwa watu na kujaribu kuwashawishi watu kuwa yeye ni John D. Rockefeller.
Muuguzi yule aliamua kuanza kumwomba msamaha mfanyabiashara yule dhidi ya kitendo alichokifanya mzee yule juu yake. Ndipo mfanyabiashara yule akashikwa na hali ya juu ya mshangao na kupigwa butwaa dhidi ya kile anachokisikia muda ule akijiuliza maswali kwamba, mwaka mzima amekuwa ni mtu wa kufanya kazi kwa bidii na kwa kujitoa kwa kufanya mikakati mingi ya kunusuru biashara yake kuanguka moja kwa moja, na hata kufikia kuanza kutengeneza faida tena, lakini akifanya hivyo kutokana na ushawishi mkubwa aliokuwa anaujenga katika akili yake kwa ajili ya kunusuru na kuweka salama nusu ya mamilioni ya dola alizokabidhiwa ili kujenga uaminifu. Lakini ghafla anakuja kutambua kuwa zile fedha hazikuwa za kweli ingawa zilimfanya kuamsha ari mpya (morale) ya kufanya kazi kwa bidii na hata kufikia kurudisha biashara yake katika mazingira mazuri. Hii ilimpa nafasi ya kujenga ujasiri mpya ndani yake ulioweza kumsadia kufanikisha mambo mengi katika maeneo mengine ya maisha yake.
Kuna mambo 3 tunayojifunza katika habari hii uliyoisoma na wewe mahali hapa:
1: Jiulize. Unahitaji nini cha kukuhamasisha ili kuchukua hatua dhidi ya hatima ya kile ulichokata tamaa kukifanya.
Mara nyigi huwa tunapitia katika nyakati ngumu na zenye changamoto nyingi katika maisha yetu. Jiulize ni hatua gani unayochukua kukunusuru na kukata tamaa pale unapopitia katika wakati mgumu ili kukuhamasisha usikwame na kuacha kuchukua hatua dhidi ya kutimiza ndoto zako. Hakuna mtu ambaye hapitii au hajawahi kupitia changamoto katika maisha yake, ila utofauti uliopo kati yetu ni namna gani tunavyoweza kushikamana na changamoto hizo ili kunusuru maisha yetu yasitoke nje ya mfumo mzima wa mambo yetu tunayofanya kila siku yanayotupelekea katika kufikia katika mafanikio yetu tunayoyataka.
Kila unapopitia changamoto fulani ni rahisi sana kujilaumu na kulaumu watu wengine dhidi ya hali yako nzima unayopitia katika maisha, lakini ukweli ni kwamba ni mara ngapi wewe binafsi umekuwa ukiwajibika dhidi ya maisha yako ili kufikia hatua ya kujipa nguvu dhidi ya safari yako ya kufuata mafanikio ya ndoto yako. Hakuna mtu wa kukupa kila kitu unachotaka au unachozani kinaweza kuwa msaada mkubwa kwako wa kukufanikisha moja kwa moja katika ndoto uliyonayo. Unapaswa kufahamu wewe ndiye dreva wa maisha yako unayetakiwa kuendesha gari lako kwa makini zaidi hata kama utapita kwenye milima na mabonde mengi, kikubwa ni kutazama wapi unakoelekea ili uweze kufika salama na kwa wakati sahihi.
2: Una uwezo mkubwa ndani yako. Tafuta mtu wa kukuhamasisha na kukuongoza ili kukutia nguvu zaidi kuchukua hatua.
Mfanyabiashara tuliyemsoma hapo juu kwenye stori yake, tunaona hakuweza kufanya lolote baada ya kushindwa kujua ni wapi pakupata fedha zitakazomsaidia kuendelea kuinua na kusimamisha biashara yake mpya. Lakini baada ya kukutana na mtu aliyempatia cheki bandia ingawa wakati huo hakujua kama amepokea cheki bandia, alijikuta ghafla akipata nguvu ya kufanya kazi kwa bidii ili kuweza kutunza uaminifu kwa tajiri mkubwa aliyempatia fedha zile hata pasipo kuzitumia fedha alizopokea. Hii inaonyesha ni jinsi gani alivyokuwa na shauku ya kuonyesha uaminifu wa kiwango cha juu sana hasa kwa mtu mkubwa kama yule ambaye kwa uhalisia alijua fika ni John D. Rockefeller kabla ya kuzibitika si kweli.
“I’m a success today because I had a friend who believed in me and I didn’t have the heart to let him down.” -Abraham Lincoln
Ukweli ni kwamba ili mtu yoyote afanikiwe anahitaji watu wanaoweza kumpa hamasa kila siku hasa katika eneo lake la “field” analofanya. Hii inamsaidia mtu kuwa mwenye nguvu na hata kuamsha ari (morale) ndani ya mtu ya kufanya kazi kwa bidii pasipo kukata tamaa dhidi ya changamoto anazokutana nazo kila mara. Nipo hapa kukutia moyo kuwa amini unaweza kufanya lolote lile unaloona kwako ni gumu hadi hivi sasa, jiamini na amni unaweza, ishi ndoto yako.
3: Ili ufanikiwe katika eneo lolote lile maishani unahitaji kiwango cha juu sana cha ujasiri ndani yako.
Kuna msemo mmoja wa kiswahili unaosema uoga wako ndio umasikini wako. Tunachokiona kwa huyu mfanyabiashara ni ujasiri wa ajabu na nidhamu ya hali ya juu ya kuweza kukaa na cheki yenye kiasi kikubwa cha fedha pasipo kuchukua uamuzi wowote wa kwenda benki hata siku moja kwa ajili ya kuzitoa. Kama ningekuwa ni mimi, naamini yawezekana ningekuwa tayari nimeenda benki haraka sana kwa ajili ya kutoa fedha zile, kwa sababu tayari nilikuwa kwenye kiwango cha juu cha kutokuwa na amani dhidi ya maendeleo ya biashara yangu. Ndio maana unapaswa kila wakati kuwa mwangalifu na mawazo yako na vizuri kufikiri kwa kina na chanya zaidi kabla ya kuchukua maamuzi yoyote yale.
Jiulize ni kwa nini umeshindwa kuanza biashara? Ni kwa nini unashindwa kuonana na mtu unayejua fika ni mtu anayeweza kukusaidia katika hatima njema ya kufikia ndoto yako? Nataka nikuambie umekosa ujasiri bado unatanguliza hofu mbele yako, na hii ndio sababu ya wewe kushindwa kuendelea mbele na kufanikiwa katika maisha yako. Amua kuanzia sasa kuwa miongoni mwa watu wenye kiu na shauku ya juu ya mafanikio ili uweze kufikia kilele cha ndoto yako uliyonayo.

Post a Comment

 
Top