0

Wall 3
Neno “Ukuta” limekuwa ni neno maarufu kwa sasa nchini Tanzania kutokana na namna lilivyotumiwa na Chama cha upinzani cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) karibu mwezi mzima sasa kama sehemu ya kudai haki yao kwa serikali ya Tanzania kwa yale wanayoyaona hayapendezi kwao kulingana na wao binafsi wanavyosema na kudai zaidi na si mimi. Chama cha chadema kimejipanga kufanya maandamano ya kudai haki hiyo siku ya tarehe mosi mwezi ujao wa tisa ambayo itakuwa ni siku ya alhamisi, ingawa serikali imeshapinga kutokufanyika kwa maandamano hayo na kuonya watu wasijaribu kufanya hivyo kwani kwa kufanya hivyo itakuwa ni kosa kisheria kutokana na kutokufuata sheria na marufuku hiyo iliyotolewa na serikali kuhusu maandamano hayo.
Mbali na hayo mimi si mwanasiasa na makala hii haipo kwa ajili ya kuzungumzia masuala ya siasa au kutoa taarifa yoyote ile kwa lengo la uchochezi wa masuala ya siasa au masuala yoyote yale yanayohusiana na suala hili la ukuta, bali makala hii nimeitoa kwa ajili ya kijikita zaidi katika kukuhamasisha wewe msomaji wangu binafsi hasa kwa ajili ya kuchukua hatua juu ya maisha yako kwa lengo la kujiletea maendeleo binafsi kwako. Nimetumia neno “ukuta” ambalo linatumiwa na chama cha chadema kwa ajili kuhamasisha wafuasi wao kuandamana na kudai haki kwa serikali na zaidi likiwa na maana ya “kuiwekea ukuta serikali kwa yale ambayo chadema inaona inaonewa kwa sasa wao na wananchi wote.”
Kwa mfano utakumbuka masuala ya Ukuta wa Berlin (kijerumani Berliner Mauer) ulitenganisha sehemu mbili za jiji la Berlin (Ujerumani) kuanzia 13 Agosti 1961 hadi 9 Novemba 1989. Mashariki ya Berlin ilikuwa sehemu ya nchi ya kikomunisti Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani na magharibi ya jiji ilikuwa chini ya mamlaka ya Marekani, Uingereza na Ufaransa. Ukuta huu ulikuwa na urefu wa kilomita 45.3 ukiwa sehemu ya mpaka kati ya madola mawili ya Ujerumani yaliyokuwepo kuanzia 1949 hadi 1990. Ukuta wa Berlin ulikuwa mfano uliojulikana zaidi wa “pazia la chuma” katika Ulaya lililotenganisha nchi za kikomunisti za Ulaya mashariki na nchi za Ulaya magharibi. Takriban watu 200 waliuawa walipojaribu kuvuka ukuta kutoka mashariki kwenda magharibi.
Chanzo cha ukuta huu ulikuwa ugawaji wa jiji la Berlin baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia tangu 1945. Nchi washindi ziliamua kugawa Ujerumani yote wakaanzisha kanda nne zilizotawaliwa na Umoja wa Kisovyeti, Marekani, Uingereza na Ufaransa. Berlin ilikuwa ndani ya kanda ya kisoyeti lakini ikiwa mji mkuu wa Ujerumani ilitangazwa kuwa mkoa wa pekee ikagawiwa pia katika kanda nne za washindi. Tangu 1946 washindi walianza kutoelewana na kipindi cha vita baridi kilianza ambako nchi za magharibi (Marekani, Uingereza, Ufaransa) zilisimama dhidi ya nchi za mashariki zilizoongozwa na Umoja wa Kisovyeti. Ukifatilia suala hili la ukuta kwa israel na palestina utakuna nalo pia.
Tukiachana na mfano huo basi tambua Neno ukuta linajulikana maana yake na kwa maana yake ya kawaida tu ni kwamba, “ukuta ni kizuizi kinachojengwa kwenye nyumba au jengo kwa ajili ya kuziba uwazi unaoweza kujitokeza katika nyumba au kuikamilisha nyumba au jengo hilo kuwa kamili.” Ndio maana waswahili wa kale walisema, “usipoziba ufa (uwazi uliojitokeza), utajenga ukuta (yaani utang’aramia kujenga ukuta mkubwa zaidi au ukuta mzima ili kuziba sehemu kubwa zaidi ya uwazi uliojitokeza).
Pamoja na maana hiyo ya kawaida kabisa ambayo tumeipata au nimekupatia hata kabla ya kuingia kwenye kamusi ya kiswahili sanifu kuitizama na kuangalia maana yake kamili ya neno hilo hasa kwa kuwa ni neno jepesi kueleweka kwa kila mtu. Wapo watu wamekuja na maana nyingine nyingi ya neno hili “ukuta” kutokana na kuwa maarufu zaidi hasa katika kipindi hiki ambacho Chama cha Chadema wamelipa “promo” kubwa neno hilo, na kuenea nchini kote hadi kwa watoto wadogo na wao wakiwa wanajua nchi yetu ya Tanzania kwa sasa habari ya mjini ni neno “ukuta”.
Kuna watu wametoa maana kadhaa ya neno “Ukuta” sitoweza kuzitoa mahali hapa kutokana na sababu maalum na yawezekana nawe umeshakutana nazo huko mtaani kwako au kwenye mitandao ya kijamii. Ila leo hii nataka utumie neno hili na maana yake ya kwanza hasa niliyokupa hapo juu kama sehemu ya kukusaidia wewe binafsi katika kufikia mafanikio makubwa hasa juu ya ndoto na malengo yako. Yapo maeneo unayohitaji kuweka ukuta katika maisha yako binafsi ili uweze kufanikiwa katika viwango vya juu na kufikia katika hatua ya kupata mafanikio makubwa unayoyataka.
Ili ufanikiwe ni lazima ufikie mahali ambapo utaweza kukabilina na mambo yanayokuzia kuendelea mbele wewe mwenyewe binafsi au wakati mwingine kuyakingia “ukuta” ili yaweze kuzuilika na wewe uweze kuendelea mbele zaidi. Kama kujenga ukuta ni sehemu ya kuziba nyufa au matundu au uwazi unaojitokeza kwenye nyumba au jengo lako, basi hata mtu binafsi anaweza kujenga “ukuta” kwa ajili ya maeneo yaliyojitokeza kwenye maisha yake na kuweka uwazi au nyufa au matundu yanayoweza kuwa sababu ya mtu huyo kutokuendelea mbele. Jiulize una ufa au uwazi au tundu gani katika maisha yako lililojitokeza na linaloruhusu kukwama kwako na kukuzuia kuendelea mbele zaidi? Na kumbuka “usipoziba ufa, utajenga ukuta mkubwa zaidi, na wakati mwingine watu watakuchungulia au utawapa nafasi wezi kuingia ndani kwa haraka na kukuibia kila kitu.”
Unahitaji kuziba ufa (nafasi ndogo au kubwa) na kujenga ukuta katika maeneo yafuatayo ndani ya maisha yako ili uweze kusogea mbele na kusababisha mafanikio yatokee katika maisha yako.
1: Ziba ufa au milango ya hofu uliyonayo na jenga ukuta wa kujiamini ili usogee mbele kimaisha.
Hofu ni ufa, hofu ni uwazi, hofu ni tundu linaloweza kusababisha mafanikio yako yasitokea hasa kwa watu wengi walio na ndoto ya kufikia ndoto zao kubwa walizonazo katika maisha. Angalia ni mambo mangapi umeacha kuyafanya kwa sababu ya hofu ya kuogopa kufeli au kushindwa njiani, angali ni mara ngapi umepata mawazo mazuri ya kukusogeza mbele kimaendeleo laini umekuwa na tabia ya kughairisha kuyatekeleza hadi yakapotea nadni ya moyo na akili yako. Tambua hofu ni mlango husio mzuri unaohitaji kuuziba kwa ukuta ili uweze kujenga mlango wa kujiamini na kuweza kuruhusu tabia njema kuingia ndani yako na wewe kusogea mbele.
Unahitaji kujenga ukuta wa kujiamini kwenye maisha yako ili uweze kuona matunda unayotaka kuyaona kwa kipindi kirefu cha maisha yako ulichoishi hapa duniani. usikubali kuishi chini ya kiwango cha maana halisi ambayo Mungu amekupangia uishi bali amua kupigania ndoto yako usiku na mchana hadi uhakikishe unaona matokeo chanya maishani mwako. Soma makala ya Aina 5 za hofu unazotakiwa kuzikabili ili kujiletea ushindi katika ndoto yako.
2: Ziba ufa au mlango wa kujitetea na kuacha kutekeleza wajibu wako na jenga ukuta wa kuchukua hatua kivitendo zaidi ili kufikia ndoto yako.
Wapo watu wengi kiukweli ni wazuri sana katika kuongelea habari nzuri za mafanikio au watu waliofanikiwa na wengine hata kuziandika vizuri kama ninavyoandika mimi mahali hapa kila siku, lakini watu hawa si watu wenye kuchukua hatua kivitendo na kuwa watu wenye kutekeleza wajibu wao walionao kwa ajili ya kufuata ndoto zao za Maisha walizonazo ili kuleta matokeo makubwa katika maisha yao.
Kujitetea ndio jambo kubwa linalojitokeza kwa watu hawa, kwani kila unapojaribu kuwaambia wanaweza kufanya jambo fulani na kufanikiwa watakupa sababu lukuki zinazoweza kutumika kama ufa au mlango au tundu la kuwazuia wao kusogea mbele na kufikia hatua ya juu ya mafanikio yao wanayoyataka. Unakutana na mtu anayehitaji kufanikiwa kiuchumi na kuwa na uhuru wa kifedha lakini unapomshirikisha juu ya habari ya kuweka akiba zaidi ama kuwekeza anakupa sababu ya kutoweza kufanya hivyo kwa kuwa hana kipato cha kutosha; mwingine unapomshirikisha habari ya kuanza biashara hata ndogo ndogo akiwa bado ameajiriwa (part time business) anakuambia siwezi kwa kuwa mambo ya ofisini yamembana lakini mtu huyu anataka kuwa milionea na mtu mwenye mafanikio kifedha. Nakuambia kweli sahau kuhusu mafanikio kama wewe ni mtetezi wa hali mbaya inayokukabili maishani mwako.

“Huwezi kufanikiwa kwa kujitetea, bali waliofanikiwa waliamua kuondoa hofu wakajiamini na kuchukua hatua kivitendo.” – Wilfred Tarimo (me)

3: Ziba ufa au mlango unaopitisha tabia ya ubinafsi ndani yako na jenga ukuta wa kushirikiana na wenzako katika maendeleo.
Kuna watu wana tabia ambazo zimekuwa ni chachu mbaya kwao ya kuwazuia kusogea mbele katika mafanikio makubwa kimaisha. Tabia kama vile ya kutojitoa kikamilifu katika kitu anachokifanya ili kuleta matokeo makubwa, uvivu na kuendeleza usingizi husio na faida juu yake, chuki na ubinafsi, nakadhalika. Yote hayo na mengine mengi yamefanyika kuwa mlango na ufa mkubwa katika maisha ya watu wengi na kuwazuia kuendelea mbele na kufikia katika hatima njema ya ndoto zao. Usipoziba ufa huu, utajenga ukuta mkubwa zaidi hapo badae.
Tabia ya ubinafsi ndio imekuwa chachu mbaya kwa wengi kutokufanikiwa. Kuna wakati nilipoanza kuwa mwandikaji na mchapaji wa makala mtandaoni kama ninavyoendelea kufanya hivi sasa tangu 2012, watu wengine wenye mitandao kama mimi ya uandishi wa makala wakaibuka na kusema nachukua makala zao na kuandika. Nilishangaa sana huku mimi mwenyewe binafsi ninajua namna ninavyoumiza kichwa usiku na mchana ili kujua ninaandika nini cha kuweza kuwasaidia watu kufikia ndoto zao. Ninajua ninachokiandika kwa kuwa ninayoyandika kuna mengine nimeyapitia na kuyafanya kivitendo hata kuzaa matokeo chanya kwangu kwani siwezi kuandika kitu ambacho mimi binafsi sikitekelezi au sijaona bado matokeo yake, ila mengine ninajifunza kila siku kwa kusoma vitabu mbali mbali vya watu waliofanikiwa.
Jiulize inakuaje mtu anatokea anasema unaandika mambo ninayoandika mimi, kama ni hivyo basi haina haja ya kuwa na waandishi wengi duniani ila ni wewe tu uliye mwandishi au haina haja ya kuwa na waimbaji wengine ila ni wewe tu uliyeitwa kuimba. Si kweli kwamba ni mtu pekee tu mmoja ndiye aliyeitwa kuandika au kuitwa kuimba peke yake, ila ni ubinafsi na hofu ya kupitwa na mwingine anayemwona anampa changamoto juu yake ndio maana anampinga badala ya kujifunza kutoka kwake na kutumia njia hiyo kama changamoto ya kumfanya kuwa bora zaidi. Kama unasoma kitabu kile kile cha Robert Kiyosaki ukaelezea au kuwafunza watu, na akaja mwingine kuandika kwa utaalamu zaidi yako, wewe unaumia nini. Huo ni ubinafsi, na hii ndio sababu ninayokupa kwa nini watu wengi hawatoweza kufikia mafanikio makubwa wanayoyataka au kuyasema ni kwa sababu ya ubinafsi walionao ndani yao. Na kama ndio hivi nchi ya Marekani isingetoa waandishi wengi waliondika vitabu vyao binafsi tunavyovisoma hivi leo.
Ondoa ubinafsi ndani yako na jenga ukuta wa kuuzuia usirudi kwa upya ndani yako ili ufanyike kuwa mfano wa kuigwa na wengi na hatimaye uweze kujiletea mafanikio makubwa katika maisha yako. Nakushauri ungana na watu waliofanikiwa na kuwa miongoni mwa washindi walioamua kujitoa kwa ajili ya kuhakikisha wanageuza maisha yao kuwa katika muonekano mpya zaidi kila siku. Usikubali kwenda peke yako, karibu ujiunge na kundi la whatsapp la “ishi ndoto yako” ili uweze kufikia ndoto yako pamoja na wengine. Tuma jina lako kamili na namba yako kwa kupitia namba ya simu iliyopo hapo chini ili kujiunga na kundi hilo na zaidi utaweza kujifunza mambo mengi zaidi ndani ya kundi hilo yatakayokupa hatua mpya kila siku.
Karibu ujiunge na hawa watu wa “umoja wa kupinga umasikini tanzania (ukuta)” ili uweze kujifunza mambo ya kukupeleka katika hatima njema ya ndoto yako. Kubali kuziba ufa, ili husije kujenga ukuta mkubwa zaidi maishani mwako. Jenga ukuta katika mambo yote yanayokuzia kuendelea mbele katika maisha yako, ili uweze kusogea mbele kimaendeleo wewe mwenyewe binafsi kabla ya kwenda mbele kama nchi au taifa kiujumla, bali anza na wewe kwanza.
JIAMINI NA AMINI UNAWEZA. ISHI NDOTO YAKO.

Post a Comment

 
Top