0

Declutter-Your-Mind-Minimalism-Tips-For-The-Bold
Tunapoongelea suala hili au neno mafanikio, kila mtu huwa ana maana yake kulingana na maana yake anayokuwa nayo kwa wakati wake na kwa eneo lake husika analohitaji mafanikio hayo yatokee katika maisha pia kulingana na ndoto yake aliyonayo. Nikiwa na maana kuwa kila mtu ana tafsiri yake kuhusu mafanikio kutokana na muda na wakati alionao na anaoendelea kuuishi hapa duniani. Kwani kuna Mafanikio mengi kutokana na mtu mwenyewe binafsi kwa muda wake husika anaohitaji mafanikio hayo na kwa njia hiyo ndio maana huleta tafsiri halisi ya yeye kuelewa kile anachotaka kufanikiwa kwa wakati huo aliokuwa nao.
Kuna mafanikio ya kiafya, kuna mafanikio ya kiuchumi na kifedha na kuna mafanikio ya uhusiano mzuri nakadhalika Yote hayo na mengine mengi ni sehemu mojawapo ya maeneo ambayo kila mtu anahitaji kufanikiwa kutokana na kipindi na muda husika alionao duniani.
Katika makala yetu hii nitazungumzia zaidi juu ya mafanikio ya kiuchumi na kifedha, hasa kwa mtu binafsi anayehitaji kuishi akiwa na uhuru wa kifedha na uchumi katika maisha yake hapa duniani.
Zipo siri nyingi ninazoweza kukupa na zikakusaidia kufanikiwa katika eneo hili la uchumi na fedha, lakini ndani ya makala yetu nitazungumzia juu ya siri saba muhimu ambazo ndio ngunzo kuu ya kukusaidia kufikia mafanikio makubwa ya kiuchumi na kifedha, na hata katika maeneo mengine ya maisha yako kama vile afya, mahusiano nakadhalika hutumika.
Hivyo ni muhimu kuishi maisha ya mafanikio iwe katika suala la uchumi na fedha, uhusiano, imani na afya. Kwa kuzingatia jambo hilo ni muhimu uzingatie kanuni na siri zifuatazo:
Siri ya Kwanza:
Tembea katika Imani sahihi na Ibada.
Katika jambo lililo la muhimu na kipekee ambalo mtu yoyote anayehitaji kufanikiwa katika maisha yake anapaswa kulifanya ni kuishi maisha ya imani na kuwa mtumwa wa ibada iliyo sahihi. Fahamu katika mambo yote saba nitakayozungumzia hapa suala la imani na ibada ni la muhimu sana na ni vyema niseme linafaa kuwa la lazima kufanywa kila mara na mtu anayehitaji mafanikio makubwa maishani mwake.
Hakuna njia ya kufanikiwa na yenye mafanikio ya kudumu katika maisha haya pasipo kuwa na uhusiano wa imani uliyonayo. Ndio maana wapo watu wanaoenda kwa waganga wa kienyeji kwa ajili ya kupata mali na utajiri wanaohitaji, na wapo wanaomwamini Mwenyezi Mungu kama ndiye msaada wao katika maisha ya kufanikiwa kwao. Ninakataa nji ya kwenda kwa waganga wa kienyeji kwani sio njia nzuri unayotakiwa kuifuata bali kubali kumwamini Mwenyezi Mungu pekee kama chanzo cha kufanikiwa kwako.
Narudia tena ya kwamba; yote kwa yote katika hayo sawa na unavyoamini wewe binafsi la muhimu kwangu kukufahamisha katika hili ni kwamba; ni vyema uwe na imani na ibada katika kile unachokiamini ili uweze kupata baraka na mafanikio ya kweli maishani mwako. Lakini nakupa ushauri ni vizuri hasa Umwamini Mwenyezi Mungu zaidi ya vitu vingine vya kupita.
Jifunze kuwa na ibada kila mara na tambua binadamu si kazi ya mikono yetu binafsi, bali ni kazi iliyotokana na Mungu mwenyezi mwenyewe na kila mwanadamu ana fungu lake jema mbele ya Mwenyezi Mungu aliyemuumba. Usimkimbie Mungu ukatafuta mambo mengine yasiyofaa huku yeye ndie chanzo cha wewe kuwepo hapa duniani na anafahamu njia zako zote za kupata mafanikio.
Siri ya Pili:
Kufanya Kazi kwa bidii na ufanisi.
Suala nzima la kufanikiwa katika maisha linahitaji kujitoa na kujikana kila mara iitwapo leo ili kuhakikisha unafanikiwa na kuwa na mwelekeo mzuri na mwema wa kimaisha. Kufanya kazi kwa bidii huendana na ufanisi na ujuzi wako ulionao ambao katika vyote hivyo kwa pamoja ukizingatia vitaleta matokeo chanya na makubwa katika maisha yako na hatimaye kufanikiwa.
Acha kuwa mtu wa malalamiko na kukata tamaa kwa haraka, bali anza kuanzia sasa kujituma na kufanya kazi kwa bidii ili kuongeza kipato chako cha kila siku unachohitaji kuwa nacho. Utajiri hautokei kwa gahfla tu kama wengi wetu tunavyozani bali kama unahitaji kufanikiwa kifedha na kiuchumi ni muhimu ujitoe kufanya kazi halali na tena kwa kujituma na kwa ufanisi mkubwa.
Siri ya Tatu:
Kutoa nafasi ya Kujifunza zaidi.
Kusoma mambo mbali mbali yahusuyo maisha na yanayohusu kile kitu ulichowekeza maishani mwako kukifanya; hiyo ni sehemu tosha inayoweza kukubadilisha fikra zako na kukufanya kuwa bora, mtaalamu na mfanisi mkubwa katika utafutaji wa mafanikio yako. Hivyo basi unahitaji kuwa msomaji zaidi wa masuala mbali mbali yanayogusa eneo la maisha yako, mafanikio yako na uchumi wako kiujumla; ili kukupa ujuzi na utaalamu mkubwa wa namna ya kufanya.
Tambua ninapozungumzia suala la kusoma sina maana ya kwamba unatakiwa uingie darasani tu, HAPANA. Hapa nina maana kwamba ujifunze kusoma mambo hata yale ya kawaida kabisa yahusuyo maisha ya mafanikio yako binafsi zaidi. Kama vile ulivyotoa muda wako kwa wakati huu kusoma makala hii katika mtandao huu, hakikisha tabia hii uliyoianza isiondoke kwako kabisa bali uiendeleze kwa bidii na juhudi kubwa kila siku maishani mwako.
Nakusihi anzisha tabia ya kusoma vitabu mbali mbali vinavyohusu au kuzungumzia masuala ya maendeleo ya mtu binafsi, utajiri, kuwekeza, afya na usafi, ufanisi wa kazi, masoko, nakadhalika. Vitabu kama vile Self Made Millionare, Rich Dad Poor Dad, Maximum Achievement, The power of positive thinking, Think Big By Donald Trump, Hisa, Akiba na Uwekezaji, nakadhalika.
Tembelea mitandao mbali mbali yenye kutoa elimu na mafunzo mbali mbali ya kibiashara, maendeleo ya mtu binafsi, utajiri na kuwekeza, nakadhalika. Mitandao kama vile huu wa CICBAT na mingine mingi iliyopo kwa sasa utajifunza mambo mengi ya kukusaidia kutimiza ndoto yako.
Siri ya Nne:
Kuwa na Uhusiano Mzuri na watu waliokuzunguka au unaokutana nao kila siku.
Katika dunia ya leo kama unahitaji kufikia mafanikio makubwa zaidi maishani mwako hili ndio jambo au siri na la muhimu zaidi unalopaswa kulitekeleza kwa haraka kwa kuzingatia umakini mkubwa wa kufanya hivyo. Unahitaji watu makini na wenye moyo wa utayari wa kuweza kukusaidia ili uweze kufikia katika hatua ya mafanikio yako makubwa.
Kuwa na uhusiano mzuri na watu wa karibu yako ulionao ni jambo jema linaloweza kukuweka katika mazingira mazuri zaidi ya mafanikio makubwa na ukawa mtu wa tofauti na wengine katika nyanja zote za kimaisha. Kama ukikosa uhusiano mzuri na watu kuna athari kubwa ya kukosa furaha na amani; na kama ukikosa furaha na amani kuna athari kubwa pia ya kukosa uwezo wa kufanya kazi kwa ufanisi na bidii, kwa sababu umekosa furaha inayokufanya uwe mwenye amani wakati wote katika mazingira ya kazi na watu wengine kiujumla.
Siri ya Tano:
Kuwa na Nidhamu ya Kutunza Muda ulionao.
Hili ni jambo ambalo watu wengi wa jamii yetu tuliyonayo wameshindwa kulifanikisha kwa asilimia kubwa katika mazingira yao yote ya kimaisha na kazi, hivyo limesababisha watu wengi kushindwa kufikia malengo makubwa na mazuri waliojiwekea maishani mwao. Nataka nikuambie muda ndio msingi mkubwa na wa kipekee wa kukusaidia kufikia katika malengo yako yote uliojiwekea na unayotaka yafanikiwe kwa ajili ya kutimiza ndoto yako na kufikia mafanikio ya kweli unayoyahitaji.
Huwezi kufikia mafanikio makubwa na kufanikisha malengo yako kama bado hauna nidhamu ya kutosha ya kutunza muda ulionao kila siku. Kila mwanadamu anayeishi chini ya jua amepewa masaa 24 ya kufanya kazi na kufanya mambo mengineyo, na kwa kupitia masaa haya 24 ndio utakapoamua unahitaji kufanikiwa au kutokufanikiwa kwa kiwango gani kila siku ili kufikia malengo yako.
Jifunze kwenda na muda ili uongeze ubora wako, heshima yako na nidhamu yako binafsi katika maisha yako na eneo la kazi kiujumla kila siku. Mtu anayetunza muda sifa yake huwa haipotei hata kwa watu wa mbali na yeye.
Siri ya Sita:
Kuwa na Nidhamu ya Kutosha ya Matumizi ya Fedha.
Suala la kuwa na nidhamu ya matumizi ya fedha limenenwa sana na watu wengi katika vitabu mbali mbali vilivyoandikwa. Waandishi wengi wa vitabu vya kibiashara na maendeleo ya mtu binafsi wamejaribu kulisema na kulielezea suala hili kwa ufanisi na ujunzi mkubwa ili kuwasaidia watu kuweza kuwa na mafanikio makubwa katika eneo la uchumi na fedha. Ukisoma vitabu mbali mbali vya fedha kama vile Total Money Makeover, The secret of millionaire mind, Rich Dad Poor Dad, The Richest Man in Babyloan, nakadhalika, Utajifunza mengi zaidi na kuona msisitizo waliojaribu kuuweka juu ya kumsaidia mtu kufanikiwa kifedha.
Nami kwa makala yangu niliyowahi kutoa katika mtandao wetu mahali hapa CICBAT, niliwahi kuzungumzia juu ya suala hili la matumizi ya fedha. Hebu kwa kujifunza zaidi juu ya eneo hili ni vyema usome makala hii; Fanya hivi kama unataka kufanikiwa katika matumizi mazuri ya fedha zako.
Siri ya Saba:
Kujenga tabia ya Kujiamini na Kujikubali binafsi.
Ni moja ya siri kubwa ambayo watu wengi hawaitambui na wengine kuitambua lakini kutoitilia maanani katika utekelezaji wake. Kujiamini ni hali ya kipekee inayokuwa ndani ya mtu kwa kujenga ujasiri pasipo uogo juu ya kufanya au kutekeleza jambo fulani analolikabili mbele yake . Huku pia Kujikubali ni sehemu inayomfanya mtu kujiona wa tofauti au kipekee katika mazingira ya kile anachokifanya au kutaka kukifanya.
Hivyo tambua mambo yote hayo mawili yanaenda pamoja pasipo jambo moja kuacha jingine. Ni vyema kabisa uwe na tabia ya kujifunza kujiamini na kujikubali kama kweli unahitaji kufanikiwa na kufikia ndoto na malengo yako makubwa uliyonayo hapa duniani. Huwezi kufanikiwa kamwe kama hauna tabia ya kujiamini na kujikubali katika jambo lolote unalotaka kulifanya au unalolifanya. Tabia hizi mbili huleta tabia ya UDHUBUTU, yaani tabia ya kujaribu kufanya jambo pasipo uoga wowote ndani yako.
Katika kufahamu jambo hili zaidi hebu soma makala hii; Sababu moja ni hii, kwa nini hadi sasa umeshindwa kuanza biashara.
Hizo ndio siri muhimu za maisha ya mafanikio ya mtu binafsi hasa katika kufikia mafanikio makubwa juu ya ndoto yake ya maisha. Ushauri wangu kwako ni muhimu kila unaposoma makala moja kama hii ujifunze kuweka kwenye matendo haraka (immediately) yale yote uliyoyasoma mahali hapa. Kwa kufanya hivyo itakusaidia zaidi kufanikiwa haraka katika malengo na mipango yako yote uliyojiwekea maishani mwako.
Hadi kufikia hapo sina jambo la ziada; nakutakia siku njema na maisha mema ya mafanikio na baraka kwako, na zaidi sana uweze kuifikia ndoto yako ya maisha uliyonayo.

Post a Comment

 
Top