0


Dar es Salaam. Wanachama wa Chama cha Msalaba Mwekundu Tanzania (TRCS) wamepanga kuishtaki bodi ya chama hicho kwa Rais John Magufuli, kwa madai ya kuuza sehemu ya jengo la Viva Tower na fedha za mauzo hayo kutumiwa kwa ubadhirifu.

Habari kutoka ndani ya shirika hilo zinasema nyumba nane katika jengo hilo la ghorofa 24 lililopo Mtaa wa Ali Hassan Mwinyi, Dar es Salaam zimeuzwa bila makubaliano ya wanachama na fedha zimetumika kulipa mafao ya wafanyakazi wastaafu kinyume cha makubaliano.

“Kuna uchafu mwingi ambao umekuwa ukiendelea ndani ya chama hiki. Rais ndiye mlezi wa chama hicho, hivyo tunaamini atasaidia kukomesha vitendo hivi visijitokeze tena,” alisema Mwenyekiti wa TRCS Mkoa wa Arusha, Dk Christopher Nzella.

Mbali ya kuuzwa nyumba za jengo hilo, malalamiko mengine ni kwamba kuna baadhi ya viongozi wamekuwa wakijinufaisha kwa misaada inayotolewa na wafadhili na hesabu za chama hicho hazijafanyiwa ukaguzi kwa miaka 10.

Post a Comment

 
Top