Huwa nikikaa na kufikiri ni namna gani binadamu aliweza
kubuni ndege, meli kubwa hasa za mizigo, gari na vitu vinginevyo na
badae kuja kuwa msaada mkubwa katika dunia yetu ya siku leo hata
kurahisisha maisha katika eneo fulani lililokuwa na ugumu kwetu, basi
nauona uwezo wa Mungu aliouweka ndani ya binadamu huyu ingawa yeye
binafsi kama binadamu wakati mwingine hatulitambui hilo na kama
tunalitambua basi ni wachache na wakati mwingine hatujakaa vizuri
kuitumia hii fursa ya uwezo huo tuliopewa. Hii inaonyesha ni jinsi gani
binadamu alivyo na uwezo mkubwa wa kufanya ubunifu kwa kupitia akili
aliyonayo na kuleta mageuzi na mshangao mkubwa katika ulimwengu
tunaoishi.
Hebu tazama wengi wa wabunifu waliojitoa kwa kuumiza akili
na kubuni vitu vipya katika ulimwengu huu tunaoishi leo hii, ndio
tunaowaona matajiri katika dunia hii ya leo kuliko watu wengine
waliokataa kutumia uwezo na akili zao walizopewa na Mwenyezi Mungu na
zaidi sana kubakia kulalamikia watu wengine wanaofanikiwa. Nataka
nikuambie unauwezo mkubwa sana ndani yako unaoweza kuutumia ili kubuni
jambo kubwa litakaloleta matokeo chanya na kuwa msaada mkubwa katika
jamii yako unayoishi na kwako pia.
Ndio. Una uwezo mkubwa sana tena sana unaoweza kuleta
matokeo chanya na makubwa katika ulimwengu wako na ukasahau hata habari
ya kuajiriwa na kuanza kujiajiri binafsi kupitia jambo ulilobuni. Tatizo
ni kwamba hupendi kutumia akili yako kufikiri kwa upana na kwa kiwango
cha juu kwa hofu ya kupoteza muda, kuumiza akili, kutokutaka matatizo
(stress), nakadhalika. Kila siku umekuwa ni mtu wa kusema “mimi sitaki kuumiza akili yangu” mara unasema “mimi masuala yanayochosha akili yangu siyataki” unataka kufanya mambo marahisi marahisi ili utoke kimaisha, ni gumu sana kwa namna hiyo rafiki.
“If you do what is easy your life will be hard, but if you do what is hard your life will be easy.” – Les Brown
Nataka nikuambie akili yako inauwezo mkubwa sana, narudia “inauwezo mkubwa sana”
tena sana wa kubuni biashara ya kukutoa kimaisha, kutatua matatizo
yaliyo magumu kwa jamii iliyokuzunguka, kuleta mbinu na mikakati mipya
kwenye kazi au ofisini ili kusaidia kampuni kusimama, nakadhalika.
Tatizo unajitetea na kujenga hofu kubwa ndani yako ya kujitoa na
kufikiri ili kuhakikisha unaleta matokeo mapya na makubwa mahali ulipo
muda huu. Hebu fikiri kama binadamu huyu huyu unayemjua na aliye kama
wewe alibuni balbu za umeme anaitwa Thomas Edison kutoka nchini
Marekani; na zaidi sana binadamu huyu huyu kama wewe aliweza kugeuza
historia ya muonekano wa magari na kuja na kitu kipya zaidi anaitwa
Henry Ford, na binadamu huyu huyu aliweza kubuni biashara ya kuuza kuku
walioandaliwa kama chakula na hatimaye kuwa na mgahawa mkubwa wa KFC
uliosambaa karibu nchi 123 duniani kote anaitwa Harland Sanders. Na
wengine wengi sana ambao sitaweza kuwamaliza kwa kuwataja wote mahali
hapa siku ya leo.
Naamini wapo watu wanaoweza kujitetea na kusema kwa kuwa
hao ni watu weupe yaani wazungu na sijaona mtu mweusi hata mmoja hapo.
Hebu fikiri ni watu wangapi wanabiashara ambayo leo hii inawaingizia
mabilioni ya pesa na wakati mwingine biashara wanazozifanya ni za
kawaida na zilizokuwa zikidharaulika na watu kwenye jamii zao na wapo
hapa afrika. Angalia mtu kama Aliko Dangote kwa sasa zaidi ya
kujishughulisha na uzalishaji wa cement na bidhaa nyingine za ujenzi na
hata biashara zake kubwa nyingine kwa sasa ameenza kuzalisha nyanya na
kuuza kwenye nchi yake huko nchini Nigeria. Ulitegemea mtu kama huyu
ambaye ni tajiri wa kwanza afrika kuwaza kufanya biashara kama hiyo ya
nyaya kwa sasa? Yawezekana wewe ulipoambiwa kuuza nyanya uliona ni
biashara kichaa na haina maana ya kuifanya. Ukweli ni kuwa usipende
kuanzia pakubwa bali anza na madogo ili kukupeleka kwenye kilele chako
cha mafanikio na kutimiliza ndoto yako uliyonayo.
Hivyo hivyo kwa Bakhresa, Mengi, Dewji, Sheria Ngowi na
wengine wengi tunaowaona nchini mwetu Tanzania wamefanikiwa kiuchumi,
hii yote ni kutokana na kuamua kubuni kitu kipya kilichoweza kuwa msaada
mkubwa kwenye jamii yao na kuweza kuwaletea wao mafanikio makubwa
katika maisha yao. Sheria Ngowi pamoja na kusomea masuala ya Sheria
nchini India lakini alijua bado ana kitu cha ziada ndani yake
kinachoweza kumlipa na kumfanya awe na uhuru wa kifedha na maisha mazuri
sawa na anavyotaka. Leo hii ni mbunifu wa mavazi Africa nzima inamjua
na kumtazama. Jiulize kama asingetumia akili yake kwa kufikiri zaidi na
kufuata ndoto yake aliyokuwanayo leo hii ingekuwaje kwake na kwenye
jamii yake iliyohitaji mchango wake?
Nataka nikuambie huwezi kutoka kwa siku moja ni lazima
uumize kichwa na akili yako leo hii na kujua ni nini cha kufanya
kinachoweza kukupa uhuru unaoutaka kesho. Na suala la kuumiza kichwa
chako na akili ni sasa na si kesho, narudia tena suala la kuumiza akili
yako kwa ajili ya kubuni wazo la kukutoa kimaisha “ni sasa na si kesho”
kama unavyofikiri. Usiridhike na maisha yako unayoishi leo, usiridhike
na kipato unachokipata huku sema ukweli ndani ya moyo wako na kwa
uhalisia hakikutoshelezi kabisa kufikia kwenye kilele cha mafanikio
makubwa unayoyataka. Usikubali kuwa mvivu wa kuumiza kichwa na kutumia
akili yako kwa ajili ya kuja na kitu kipya kinachoweza kuleta manufaa
kwako na kwa jamii yako iliyokuzunguka, anza kuwa mbunifu ili uweze
kufikia ndoto yako ya maisha.
Umiza kichwa kuanzia sasa na amini katika wazo (idea)
utakayoipata ndani ya moyo na akili yako ili kukusaidia na wewe kuwa
miongoni mwa watatuzi wa matatizo katika ulimwengu huu. Unaweza kutumia
matatizo yaliyopo kwenye jamii yako kama sehemu ya kukupatia wazo jipya
na baada ya hapo kubuni njia na mkakati wa kulitatua tatizo ili kuleta
matokeo chanya katikati ya watu waliokuzunguka na kwako pia. Mwombe
Mungu akupe mwongozo wa kukusaidia kulitimiza na kulifanya hilo wazo
(idea) kuwa wazi katika ulimwengu wa nje ili usibaki na wazo lililo
kwenye akili na kichwa tu pasipo kuleta matokeo na mchango wowote
makubwa kwa watu wako.
Nakusihi usisubiri kesho. Usione una siku nyingi za kuwaza
au kuleta matokeo (ku_implement) ya hilo wazo lako (idea) uliyonayo au
ndoto ya siku nyingi unayotembea nayo kila kukicha pasipo kuweka vitendo
vya kuifanya izae faida na matunda kwako. Anza leo kuhidhilishia dunia
kuwa nawe unauwezo mkubwa aliouweka Mungu ndani yako. Usijikatae wala
usiogope kukataliwa na wengine pale utakapofanya uamuzi wa kuja na kitu
chako kipya kwenye jamii yako, kumbuka kukataliwa ni sehemu ya
kukupeleka katika mafanikio. Kadri unavyoongeza kukataliwa ndio
unavyoongeza kufanikiwa.
Kama unahitaji kuwa mbunifu wa mavazi kama sheria ngowi
anza kubuni leo hii au ikibidi mtafute na uwe chini yake na afanyike
kuwa msaada na mshauri wako (mentor) wa hicho kitu unachotaka kukifanya.
Amini inawezekana kwani watu waliofanikiwa si wachoyo unapojishusha na
kuonesha uhitaji wa kujifunza kutoka kwao. Kama unataka kuwa
mfanyabiashara mkubwa kama Dangote lakini bado huna wazo la biashara.
Basi elewa una uwezo mkubwa wa kuumiza kichwa na akili kuanzia sasa na
ukapata wazo linaloweza kuishangaza dunia yote hapo badae.
Lakini kumbuka si lazima ukaja na kitu kipya kabisa kwani tambua unauwezo pia wa “kuboresha wazo”
au kitu fulani kinachofanyika na watu wengine ila wewe ukaleta ubunifu
mpya kwenye hicho kitu na kuleta utofauti mkubwa kwenye eneo
(industries) hiyo. Na hii ndio njia inayofanyika kwenye makampuni ya
simu, magari, televisheni, nakadhalika. Leo hii samsung akileta simu
yenye kamera yenye uwezo wa mega pixel 16 kesho yake utasikia Iphone
ametoa simu yake mpya yenye kamera yenye uwezo wa mega pixel 20. Huu ni
ubunifu tu ili kuzidi kutawala soko na kuteka wateja wa soko la simu
ulimwenguni kote. Nataka nikuambie nawe unauwezo wa kufanya ubunifu
mkubwa kwenye jambo lolote lile ili kukuletea mafanikio makubwa na
hatimaye ukafanikiwa kufikia katika ndoto yako.
Nataka nikuambie una mawazo milioni na zaidi ndani yako
ambayo hadi sasa dunia inayasubiri ili yaweze kuwa msaada kwa watu wengi
na kufanyika kuwa faraja kubwa hata kwa watu waliokata tamaa. Ndio.
usishangae wala sijakosea kusema ni “mawazo milioni na zaidi”
uliyonayo ndani yako. Ni wewe tu umejidharau, ni wewe unajiona huwezi
kuwaza na kutoka na kitu kipya au kilichojaa ubunifu, ni wewe tu unajaa
hofu ya kukataliwa kisa unaona utaonekana unaiga, huigi kwani hata
waandishi wanaoandika kama mimi wanaandika kutokana na walichokipitia
kwenye maisha na kujifunza kwa wengine, ni wewe tu unajiona huna lolote
na si chochote katika ulimwengu huu hivyo huwezi kufanya mambo makubwa.
Unajikosea heshima kwa kujiwiza mawazo hayo ya chini na kumkosea
Mwenyezi Mungu yeye aliyekuumba na kukupa akili zote timamu ili uzitumie
kwa ajili ya kuwaza na kubuni mambo mapya yanayoweza kuwa msaada mkubwa
kwako na kwa jamii yako iliyokuzunguka. Anza kuwaza na kuumiza akili na
kichwa chako leo hii, na amini kesho utafanikiwa.
JIAMINI NA AMINI UNAWEZA. ISHI NDOTO YAKO.
Post a Comment