0
 Jeshi La Polisi Tanzania
Ndugu zangu waandishi wa habari,
Kwa ujumla hali ya amani na usalama wa nchi yetu ni shwari. Ingawa yapo matukio machache yametokea katika baadhi ya mikoa kama vile Mwanza, Tanga na Dar es salaam. Matukio hayo tayari yanaendelea kushughulikiwa, baadhi ya watuhumiwa wanaojihusisha na matukio hayo tayari tumekwishawakamata na upelelezi ukikamilika watafikishwa mahakamani ili sheria ichukue mkondo wake.  Aidha, wakati tunaendelea na uchunguzi wa matukio hayo, niwaombe wananchi kuondoa hofu na wasiwasi na badala yake watoe taarifa na ushirikiano kwa vyombo vya dola ili kuhakikisha kwamba wote wanaojihusisha na uhalifu huo wanakamatwa haraka. 


Hata hivyo, ndugu waandishi wa habari, mtakumbuka kuwa zoezi la uhakiki wa silaha lililoanza tarehe 21/03/2016 bado linaendelea nchi nzima ambapo linafanyika kwa kipindi cha miezi mitatu hadi tarehe 30/6/2016.  Zoezi hili la uhakiki wa silaha lipo kwa mujibu ya Sheria ya Usimamizi na Udhibiti wa Silaha na Risasi ya Mwaka 2015, ambapo kifungu cha 66 cha sheria hiyo kinamtaka kila mmiliki kuhakiki kumbukumbu za silaha yake au risasi pale atakapoamriwa na mamlaka husika.

Lengo la kuhakiki kumbukumbu za wamiliki wa silaha ni kupata taarifa sahihi za wamiliki hao lakini pia taarifa zitakazosaidia kubaini wale wote wanaomiliki silaha kinyume cha sheria. Aidha, zipo sababu nyingine kwa mfano, wapo wamiliki ambao walikwishahama kutoka katika makazi yao ya awali na kuhamia katika makazi mapya.

Pia wapo baadhi ya wamiliki ambao walishafariki na silaha zao bado hazijakabidhiwa katika vituo vya polisi, jambo ambalo linaweza kusababisha silaha hizo kutumika katika vitendo vya uhalifu. Zoezi la uhakiki wa silaha linakwenda sambamba na ulipaji wa madeni ya ada za leseni za kumiliki silaha ambayo wamiliki wanadaiwa.

Wito kwa wamiliki wa silaha.
Kufuatia zoezi la uhakiki wa silaha linaloendelea, natoa wito kwa wamiliki wote wa silaha kujitokeza kuhakiki silaha zao haraka katika kipindi hiki kilichobaki katika wilaya wanamoishi, wakiwemo watu binafsi, makampuni binafsi, Taasisi za Kiserikali na zisizo za Kiserikali. Aidha, wananchi ambao ndugu zao walikuwa wanamiliki silaha na kwa sasa wamefariki, au wamepatwa na matatizo ya kiafya wazisalimishe silaha hizo katika vituo vya Polisi ndani ya kipindi hiki cha zoezi la uhakiki wa silaha.
Sambamba na zoezi hili la uhakiki wa silaha zinazomilikiwa kihalali, natoa wito kwa watu wote wanaomiliki silaha kinyume cha sheria kusalimisha silaha hizo katika vituo vya Polisi, ofisi za serikali na kwenye nyumba za ibada na watakaofanya hivyo ndani ya muda uliopangwa hawatachukuliwa hatua zozote za kisheria.

Nitumie fursa hii kusema kwamba baada ya tarehe 30/06/2016 hatutakuwa na msamaha kwa yeyote atakayekuwa amekaidi zoezi hili.

Baada ya muda huo, Jeshi la Polisi nchini litaendesha operesheni kali kwa lengo la kuwasaka na kuwakamata wale ambao watakuwa hawakujitokeza katika zoezi la uhakiki au kusalimisha silaha ili hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi yao ikiwa ni pamoja na kuwafutia leseni zao na silaha zao kutaifishwa na kuwa mali ya serikali.  Aidha, napenda kuwakumbusha wamiliki wa silaha za kiraia wanaozimiliki kihalali kutunza silaha zao ipasavyo ili zisiangukie kwenye mikono ya wahalifu.

Mwisho, Kwa kuwa wahalifu tunaishi nao ndani ya Jamii nawasihi wananchi wafahamu kuwa hawana budi kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuwabaini na kuwafichua wahalifu hao ili usalama na mali zao uendelee kuimarika.

Asanteni kwa kunisikiliza.
Imetolewa na:
Advera J. Bulimba – Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP)
Msemaji wa Jeshi la Polisi,
Makao Makuu ya Polisi.

Post a Comment

Emoticon
:) :)) ;(( :-) =)) ;( ;-( :d :-d @-) :p :o :>) (o) [-( :-? (p) :-s (m) 8-) :-t :-b b-( :-# =p~ $-) (b) (f) x-) (k) (h) (c) cheer
Click to see the code!
To insert emoticon you must added at least one space before the code.

 
Top