0


Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Ernest Mangu

Jeshi la Polisi nchini Tanzania leo limepokea msaada wa kituo cha kisasa cha mawasiliano na mIito ya dharura, kwa ajili ya kukabiliana na matukio ya uhalifu hususani uporaji wa fedha unaotokea kwenye mabenki pamoja na aina nyingine ya uhalifu.

Kituo hicho kimejengwa kwa msaada wa benki ya CRDB na kugharimu fedha za Tanzania shilingi milioni 255 ambapo akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa benki hiyo Dkt Charles Kimei amesema malengo ya wao kufadhili kituo hicho ni kusaidia jitihada za kupunguza vitendo vya uhalifu nchini.

Dkt Kimei amesema biashara nchini haziwezi kufanyika iwapo nchi haina amani na kwamba kupungua kwa vitendo vya uhalifu kunatokana na jitihada za polisi katika kukabiliana na uhalifu.

Dkt. Kimei ameongeza kuwa uhalifu hauwezi kufanyika iwapo kutakuwa na askari wa kutosha tena wenye uwezo wa kufika eneo la tukio kwa haraka na kutolea mfano wa tukio la Mbagala kuwa lisingeweza kutokea iwapo kungekuwa na askari wengi wa doria karibu na eneo la tukio.

Kwa upande wake, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Ernest Mangu amesema kituo hicho kitasaidia kupunguza matukio ya uhalifu kwani ndani yake kimefungwa vifaa vya kisasa vinavyoweza kutambua eneo alipo mtoa taarifa ya uhalifu pamoja na mahali yalipo magari na askari wa doria kwa ajili ya kuwahi kutoa msaada.

Kwa mujibu wa IGP Mangu, kituo hicho ni cha kisasa kwani mbali ya kutambua yalipo magari na askari wa doria, kinaweza pia kuwasiliana moja kwa moja na askari hao na kwamba hiyo ni mwanzo wa hatua za kuboresha ufanisi wa polisi nchini kwa kusogeza zaidi huduma za polisi karibu na wananchi.

IGP Mangu ameongeza kuwa kwa kuanzia, maboresho hayo yatafanyika katika mkoa wa Kipolisi wa Kawe jijini Dar es Salaam ambapo katika kila eneo lisilozidi umbali wa kilomita tatu, kutakuwa na komandi kamili ya polisi wenye magari, silaha na vifaa vyote vya kukabiliana na uhalifu ndani ya eneo hilo la kilomita tatu.

Post a Comment

 
Top