0


Wafungaji wa mabao ya Yanga SC leo, Amisi Tambwe kulia na Simon Msuva kushoto wakishangilia leo Uwanja wa Taifa 
Na Mahmoud Zubeiry, 
YANGA SC imerejea kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kufuatia ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Kagera Sugar Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jioni ya leo.
Katika mchezo huo, uliochezeshwa na refa Andrew Shamba kutoka Pwani, aliyesaidiwa na Martin Mwaliaje wa Tabora na Hajji Mwalikita wa Tanga, Yanga SC ilikwenda kupumzika ikiwa tayari inaongoza kwa mabao hayo 2-1.
Winga Simon Msuva alianza kufunga bao la kwanza kwa penalti dakika ya nane baada ya yeye mwenyewe kuangushwa na Benjamin Asukile.Mfungaji bora wa Ligi Kuu msimu uliopita, Mrundi Amisi Tambwe aliifungia Yanga SC bao la pili dakika ya 15, akimalizia pasi ya Mrisho Ngassa ambaye naye alipasiwa na Kpah Sherman.Yanga SC walionekana ‘kuridhika’ baada ya kuwa mbele kwa mabao 2-0 na kucheza kwa mbwembwe, hatimaye kuwaruhusu Kagera kupata bao.
Bao hilo lilifungwa na Salum Kanoni kwa penalti, kufuatia Rajab Zahir kumuangusha kwenye eneo la hatari Atupele Green.Kagera waliongeza kasi ya mashambulizi baada ya kupata bao hilo, lakini Yanga SC walisimama imara kuwadhibiti wapinzani wao hadi mapumziko.
Kipindi cha pili, timu zote zilishambuliana kwa zamu na kila upande ulikosa mabao zaidi ya mawili ya wazi.Sherman alipewa pasi nzuri na Ngassa akiwa ndani ya boksi, lakini akazubaa hadi beki wa Kagera, Eric Kyaruzi alipotokea na kuokoa.
Mshambuliaji wa Yanga SC, Mrisho Ngassa kulia akimtoka beki wa Kagera Sugar, Benjamin Asukile 
Kpah Sherman akimtoka beki wa Kagera Sugar Benjamin Asukile 
Rashid Mandawa naye alipiga nje akiwa kwenye nafasi nzuri dakika ya 64. Tegete aliyetokea benchi alipoteza nafasi mbili za wazi dakika za lala salama.
Ushindi huo unaifanya Yanga ifikishe pointi 34, baada ya kucheza mechi 17 na kurudi kileleni mwa Ligi Kuu, ikiwazidi kwa pointi moja mabingwa watetezi, Azam FC.
Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul, Oscar Joshua, Rajab Zahir, Mbuyu Twite, Salum Telela/Nizar Khalfan dk90, Simon Msuva, Hassan Dilunga, Amisi Tambwe/Hussein Javu dk35, Mrisho Ngassa na Kpah Sherman/Jerry Tegete dk74.
Kagera Sugar; Andrew Ntalla, Benjamin Asukile, Salum Kanoni, Ibrahim Job, Eric Kyaruzi, George Kavilla, Daud Jumanne/Juma Mpola dk36, Babu Ali, Rashid Mandawa, Atupele Green/Adam Kindwande dk63 na Paul Ngway.

Post a Comment

 
Top