0


Watu 10 kati ya 30 wanaodaiwa kuwa wafuasi Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (Cuf), Profesa Ibrahim Lipumba (pichani)  na chama hicho walioachiwa baada ya kufutiwa mashitaka na kukimbia, walijisalimisha mahakamani jana na kusomewa mashitaka yao upya likiwamo la kula njama, kufanya mkusanyiko isivyo halali na kupinga amri halali ya Jeshi la Polisi.
 Washtakiwa hao ni Shaban Ngulangwa, Juma Kombo, Mohamed Kilungi, Mohamed Mbaruku, Issa Wabibi, Kaisi Kaisi, Mohamed Mchuchuma, Saleh Ally, Bakari Maleje na Abdallah Said.
Kesi hiyo ilisomwa mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Hellen Riwa.
Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tumaini Kweka, alidai kuwa kesi hiyo imekuja kwa ajili ya kuwaunganisha washtakiwa kwa sababu hawakuwapo mahakamani Februari 26, mwaka huu amri ilipotolewa ya kuunganishwa na Profesa Lipumba.
Kweka alidai kuwa Januari 27, mwaka jana, Wilaya ya Temeke washtakiwa walikula njama ya kutenda kosa.
 Katika shitaka la pili, ilidaiwa kuwa siku ya tukio la kwanza, katika ofisi za Cuf zilizopo karibu na Hospitali ya Temeke, walikusanyika kwa ajili ya kuandamana kwenda viwanja vya Zakhem Mbagala.
 Katika shitaka la tatu, ilidaiwa kuwa siku ya tukio la kwanza na la pili, washtakiwa baada ya kufanya mkusanyiko usio halali, eneo la mzunguko wa Mtoni kwa Aziz Ally, walifanya fujo walipotawanyishwa na polisi kwa lengo la kuzuia maandamano.  Upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.
Wakili wa utetezi, Peter Kibatala, aliiomba mahakama dhamana za washtakiwa ziendelee kama awali.
 Mahakama iliridhia maombi hayo na washtakiwa wako nje kwa dhamana hadi Machi 23, mwaka huu kesi yao itakapotajwa.NIPASHE

Post a Comment

 
Top