0

Waziri wa Ujenzi Dk. John Pombe Magufuli akikagua ujenzi wa kituo cha Mradi wa Mabasi yaendayo haraka (BRT) Morocco jijini Dar es Salaam siku za hivi karibuni. Picha na Maktaba  
Dar es Salaam. Machungu ya Watanzania yakiwa hayajapoa kutokana na kashfa ya Sh306 bilioni kutoka katika Akaunti ya Tegeta Escrow, ufisadi mwingine wa zaidi ya Sh252 bilioni umeibuliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad ndani ya wizara ya ujenzi.
Ukaguzi maalumu uliofanywa na ofisi ya CAG katika kipindi cha mwaka wa fedha 2010/11 na 2011/12 umebaini kuwa taarifa iliyotolewa na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli, bungeni Novemba 2013 kuwa fedha hizo zilitumika kwa miradi ya ujenzi wa barabara, haikuwa sahihi.
Kutokana na ufisadi huo, habari zilizolifikia Mwananchi zinasema CAG amependekeza hatua stahiki zichukuliwe kwa wahusika wa wizara ya ujenzi na wakala wa barabara ili kuleta imani na uwazi katika bajeti kwa jamii na wahisani.
“Wizara (ya ujenzi) ililidanganya Bunge kuwa kuna ujenzi wa barabara hizo wakati wakijua kwamba walikusudia kulipa madeni ya wakandarasi na washauri wa ujenzi wa barabara...mpango mkakati wa wakala wa barabara wa mwaka wa fedha 2011/12 pamoja na manunuzi ulioidhinishwa havikuonyesha utekelezaji wa mradi huo,” chanzo cha habari kilikariri ripoti ya CAG.
Matumizi hayo yasiyo sahihi yaliibuliwa na Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) Novemba 22, 2013 baada ya kutilia shaka kiasi hicho cha fedha na ofisi ya CAG kuagizwa kufanya ukaguzi.
Katika kikao hicho ambacho wizara ya ujenzi iliwakilishwa na Katibu Mkuu wake wa wakati huo, Balozi Herbert Mrango alihojiwa na Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe kuhusu hati ya mashaka waliyoipata kutoka kwa CAG mwaka 2011/12.
Kamati hiyo ilieleza kuwa kwenye Bajeti ya mwaka huo Sh348.1 bilioni zilizokuwa zimetengwa chini ya fungu lililokuwa limetajwa kuwa ni la mradi maalumu hazikutumiwa kwa malengo yaliyoelezwa bungeni.
“Ni vizuri leo (ilikuwa Novemba 22 mwaka 2013) uiambie kamati fedha hizi ziliombwa kwa kitu gani na zilitumika kwa jambo gani. Tunajua kwamba fedha hizi zilipunguzwa Sh95 bilioni na kupelekwa Wizara ya Uchukuzi, zilibakia Sh252.975 bilioni katika kifungu hicho lakini kuna bilioni 100 zimetumika visivyo,” alisema Zitto.
Alisema katika majumuisho ya bajeti wizara hiyo, Dk Magufuli na Dk Harrison Makyembe aliyekuwa Naibu waziri wa wakati huo aliyekuwa Waziri wa Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi walitoa maelezo yasiyo ya kweli bungeni kuhusu fedha hizo.
Zitto alikariri maneno yaliyorekodiwa kwenye Hansard ya Bunge yaliyosemwa na viongozi hao watatu.
“Tunaomba fedha Sh252 bilioni kwa ajili ya kuanzia kazi za ujenzi wa barabara.”
“Fedha hizi zitachangia miradi ya wafadhili,” haya yalikuwa maneno ya Dk Makyembe ambaye sasa ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakati akifafanua majumuisho.
“Hizi ni fedha kwa ajili ya Counterpart fund,” alimkariri Lukuvi ambaye sasa ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakati akichangia hotuba ya wizara hiyo.
Chanzo cha habari kimeeleza kuwa ripoti ya CAG imeeleza kuwa, “Katika kikao cha kuanza ukaguzi huo Aprili 3, mwaka jana uongozi wa wizara ulithibitisha kwamba hakukuwa na barabara mpya bali walifanya hivyo baada ya kuona madeni yamekuwa makubwa kiasi cha Sh420 bilioni kama yalivyokuwa kwenye hesabu za wakala wa barabara za mwaka wa fedha 2010/11.”
Katika ukaguzi huo imebainishwa kuwa Sh3 bilioni hazikujulikana matumizi yake.
Taarifa zaidi zinasema baada ya wizara kupeleka fedha kwa wakala wa barabara, fedha hizo zilifanyiwa mchakato wa kuzigawa upya lakini nyaraka halisi zilizotumika kugawa fedha hizo hazikuwasilishwa kwa ukaguzi.
“Hata hivyo, kati ya Sh175.3 bilioni zilizopitia kwenye akaunti ya maendeleo ya wakala wa barabara, kiasi cha Sh3,048,365,229 hakikuweza kupatiwa maelezo jinsi kilivyotumika.
“Pia, kati ya malipo ya Sh77.7 bilioni yaliyofanyika kwa wakandarasi au washauri wa barabara moja kwa moja kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Novemba 30, mwaka 2011 kupitia barua ya kumbukumbu namba GA.65/263/01/VOL.XI Gavana Mkuu wa BoT, alikanusha kulipa asilimia 30 ya fedha hizo Sh30.6 bilioni.
“Gavana wa BoT amekanusha kulipa Sh30.6 bilioni kwa kampuni ya M/S Strabag Internationl Gmbn na M/S China-Engineering Corporation Co, kati ya Sh77.7 ambacho kilipelekwa BoT kwa ajili ya malipo kwa wakandarasi au washauri mbalimbali,” alifafanua zaidi mtoa habari hizi na kuongeza:
“Ukaguzi maalumu umeshindwa kuthibitisha malipo yenye jumla ya Sh47.1 bilioni sawa na asilimia 61 kama yalilipwa kwa walengwa waliokusudiwa kwa sababu Gavana wa BoT amesema kuwa kisheria hatakiwi kutoa taarifa za wateja.”
Pia, habari za ndani kutoka ofisi ya CAG zinadai kuwa, Sh13.4 bilioni za ujenzi wa barabara za mikoa zilitumika kulipia barabara binafsi na za halmashauri za wilaya ambazo hutengewa fedha kupitia mfuko wa barabara kinyume na makusudio yaliyopitishwa na Bunge.
“Pia, nimebaini kwamba baadhi ya miradi haikuwamo kwenye kasma zilizopitishwa na Bunge kwenye makisio ya mwaka wa fedha 2010/11 na miradi mingine ilitengewa fedha kidogo lakini wakala wa barabara alitumia fedha nyingi kulipia miradi hiyo bila kuonyesha jinsi alivyozipata,” chanzo cha habari kimekariri ripoti ya CAG.
Katika ukaguzi huo, ufisadi mwingine wa Sh36.6 bilioni ambazo ni malipo ambayo hayakutolewa taarifa kwenye ripoti za washauri au wakandarasi, jambo linaweza kuwapo kwa uwezekano mkubwa wa wakandarasi kuidai Serikali zaidi ya mara moja na kuitia Serikali hasara.
Mtoa habari wetu alisema kuwa Sh6.2 bilioni zilitumika kuwalipa wakandarasi ambao hawakuonyeshwa katika orodha ya madeni yaliyowasilishwa bungeni pamoja na malipo ya Sh6.6 bilioni yaliyokwishalipwa yaliombewa tena.
“Madeni hayo yalikuwa yamelipwa na wakala wa barabara katika mikoa husika. Hali hii inaashiria kwamba kwa hati ya madai moja kuna uwezekano wa mkandarasi kulipwa mara mbili au zaidi.
Katika mapendekezo ya jumla, chanzo chetu kimesema ofisi ya CAG imeishauri Serikali kusimamisha kuingia mikataba mipya ya ujenzi wa barabara na ilipe madeni ya wakandarasi yaliyopo kwa sasa ili kuepuka ukuaji wa deni hilo kwa siku za baadaye na kuwa mzigo kwa Taifa na wananchi.
“Serikali ihakikishe inaheshimu mikataba iliyowekwa kati yake na wakandarasi ili kuepuka malipo yenye riba na kushtakiwa na wakandarasi kutokana na kuvunja masharti yaliyowekwa kwenye mikataba,” kilifafanua chanzo chetu na kuongeza:
“Zabuni za ujenzi wa barabara mpya ziendane na fedha zilizotengwa katika mwaka wa fedha husika kama itakavyokuwa imeainishwa katika mpango wa manunuzi wa mwaka huo.”
Ukaguzi huo maalumu uliohusisha miradi 46 ya ujenzi wa barabara kuu na barabara za mikoa ambazo wakandarasi na washauri wa ujenzi wa barabara walitoa huduma kwa wakala wa barabara.
“Mbali na miradi hii 46, miradi yote ya wakala wa barabara ilikuwa imezalisha madeni ya jumla ya Sh420 bilioni kama yalivyo kwenye hesabu za wizara kufikia mwaka wa fedha 2010/11,” kilieleza chanzo chetu.
Sakata hili limeibuka wakati lile la uchotwaji wa fedha za Akautni ya Tegeta Escrow halijapoa na hadi sasa limesababisha Rais Jakaya Kikwete kufanya mabadiliko madogo ya baraza lake la mawaziri kufuatia kumfukuza kazi, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka huku Profesa Sospeter Muhongo alitangaza kuachia wadhifa wa Waziri wa Nishati na Madini.
Mbali na hao, pia Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alitangaza kujiuzuru huku Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue akimsimamisha kazi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi kupisha uchunguzi wa sakata hilo.
Katika mlolongo wa hatua za kinidhamu kuchukuliwa, baadhi ya watumishi wa umma wamefikishwa mahakamani na wengine mbele ya Baraza la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma.CHANZO:MWANANCHI

Post a Comment

 
Top