0

Na Ibrahim Yamola, Mwananchi
KWA UFUPI
  • Nukuu: “ Huyu jamaa amekuwa akifanya ziara za mara kwa mara na kujipitisha lango la Ikulu na watu wakimwona wanajua ni mtumishi wa Ikulu na watu amekuwa akiwatapeli”Kamishna Kova

Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, limemtia nguvuni mkazi mmoja wa jijini hapa kwa tuhuma za kutumia wadhifa wa Katibu wa Rais Jakaya Kikwete kujipatia fedha kutoka taasisi na watu binafsi.
Kamishna wa Polisi wa Kanda hiyo, Suleiman Kova akizungumza na waandishi wa habari jana alisema, mtu huyo alikuwa akijiita Prosper Mbena ambaye ndiye Katibu wa Rais Kikwete.
“Mkazi huyo wa Mbagala Rangi Tatu jijini Dar es Salaam tulimkamata jana (juzi) ambaye amekuwa akijiita Prosper Mbena na ameshatapeli Wizara ya Ardhi, Maji, taasisi na watu mbalimbali na mara ya mwisho alikamatwa akichukua Sh300,000,” alisema Kamishna Kova.
Aliongeza: “Tunawaomba wananchi kuwa makini na watu wa aina hii lakini taasisi zihakikishe wanaweka ulinzi katika milango yao ya kuingilia pindi wanapomwona mtu anapita pita mara kwa mara wamchukulie hatua na kujua anachokifanya hapo.”
Kamishana huyo alisema, vitendo vya watu kutumia majina ya watu kujipatia manufaa hususan ya kifedha, yamekuwapo na ili kuyaondosha kabisa ni lazima ushiriki wa wananchi na Jeshi la Polisi uwapo kwa kubadilishana taarifa.
“Tulipata taarifa kutoka kwa mmoja wa waliotaka kutapeliwa na mtego aliowekewa ni kuambiwa kuwa kati ya zile fedha Sh300,000 kuna fedha zilibaki hivyo aje kumalizia na hapo hapo tukamweka chini ya ulinzi,” alisema Kova.
“Vitu vya mwisho au vya kumalizia siyo vizuri, ukichukua umechukua ukirudi matokeo yake ndiyo hayo yaliyomfika huyu bwana ambaye hana kazi wala biashara yeyote.”
 Tukio hilo siyo la kwanza kutokea kwani yamekuwapo matukio kama haya ya watu kutumia majina ya viongozi kujinufaisha.

Post a Comment

 
Top