Raia wawili wa Marekani wanakabiliwa na mashtaka kwa kuhusika kwao katika jaribio la wiki jana la kupindua serikali ya Gambia.
Wizara ya
sheria ya Marekani inasema Cherno Njie mwenye umri wa miaka 57 ma Papa
Faal mwenye umri wa miaka 46 wamewekwa kizuizini na watafika mbele ya
mahakama baadaye leo Jumatatu. Njie atapelekwa katika mahakama moja ya
mji wa Baltimore ulioko jimbo la Maryland wakati Faal atafikishwa
mbele ya mahakama moja ya Minneapolis jimbo la Minnesota.
Kwa mujibu
wa wizara ya sheria ya Marekani, wanaume hao wawili walipanga njama za
kuvunja sheria za Marekani za kutoingilia kati wala kuhusika katika
mapinduzi au majaribio ya mapinduzi ya serikali yoiyote ile.
Wizara hiyo
inasema Njie na Faal walisafiri hadi Gambia mwezi Desemba wakiwa na nia
ya kupindua serikali ya Gambia. Kabla ya ziara yao walinunua silaha na
kuzipeleka Gambia kwa njia ya meli ili kutumika katika mapinduzi ya
serikali ya nchi hiyo.
Ripoti
zinasema waliopanga njama hizo walitegemea kwamba Njie atakuwa kaimu
kiongozi wa Gambia baada ya kumtimua madarakani rais Yahya Jammeh.
Wizara ya
sheria ya Marekani inasema baada ya jaribio hilo kushindikana, wote
Njie na Faal ambao wana uraia pacha wa Gambia na Marekani walirejea
Marekani.
Post a Comment