0

Raia wawili wa Marekani wanakabiliwa na mashtaka kwa kuhusika kwao katika jaribio la wiki jana la kupindua  serikali ya Gambia.

Wizara ya sheria ya Marekani inasema Cherno Njie  mwenye umri wa miaka 57 ma Papa Faal mwenye umri wa miaka 46  wamewekwa kizuizini na watafika mbele ya mahakama baadaye leo Jumatatu. Njie atapelekwa katika mahakama moja ya  mji wa Baltimore ulioko jimbo la Maryland  wakati Faal atafikishwa mbele ya mahakama moja ya Minneapolis jimbo la Minnesota.

Kwa mujibu wa wizara ya sheria ya  Marekani, wanaume hao wawili walipanga njama za kuvunja sheria za Marekani za kutoingilia kati wala kuhusika katika mapinduzi au majaribio ya mapinduzi ya serikali yoiyote ile.

Wizara hiyo inasema Njie na Faal walisafiri hadi Gambia mwezi Desemba wakiwa na nia ya  kupindua serikali ya Gambia. Kabla ya ziara yao walinunua silaha  na kuzipeleka Gambia kwa njia ya meli ili kutumika katika mapinduzi ya serikali ya nchi hiyo.   

 Ripoti zinasema waliopanga njama hizo walitegemea kwamba Njie atakuwa kaimu kiongozi wa Gambia baada ya kumtimua madarakani rais Yahya Jammeh.

Wizara ya sheria  ya Marekani inasema baada ya jaribio hilo kushindikana, wote Njie na Faal ambao wana uraia pacha  wa Gambia na Marekani walirejea Marekani.

Post a Comment

 
Top