0
           Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta
Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta, ameanza kukumbana na changamoto za wizara hiyo baada ya kukutana na wasafirishaji  wawili wa dawa za kulevya katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) waliokuwa na kete zaidi 154 aina ya Heroine zenye thamani ya mamilioni ya fedha kwenda nje ya nchi.
 
Sitta alikutana na wauza ‘unga’ hao ikiwa ni ziara yake ya kwanza tangu Rais Jakaya Kikwete alipofanya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri na kumteua kuwa Waziri wa Uchukuzi akibadilishana na Dk.Harrison Mwakyembe ambaye amehamishiwa Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
 
Watuhumiwa hao ambao Sitta alikutana nao katika uwanja huo wakiwa chini ya ulinzi wa maofisa wa uwanja huo ambao wote ni raia wa Tanzania ni wanawake (33), mkazi wa Sinza na wa Tabata jijini Dar es Salaam. 
 
Mmoja wa wanawake hao alikuwa na hati ya kusafiria namba AB 651920 wakati mwingine alikuwa na hati ya kusafiria namba AB 636250, walikamatwa Januari 23, mwaka huu saa 5:15 usiku wakitaka kusafiri kwa ndege ya shirika la Emirate.
 
Watuhumiwa hao ambao kila mmoja ilielezwa alikuwa amemeza tumboni kete 77 za dawa hizo.
 
 Waziri Sitta alipowahoji walimweleza kuwa walitumwa na mtu mmoja ambaye hawakumtaja jina ila walikuwa na namba yake ya simu ili wazisafirishe kwenda  Hong Kong kwa malipo ya Dola za Marekani 6,500.
 
Kufuatia hali hiyo,Sitta aliagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuwahoji zaidi watuhumiwa hao ili kuweza kubaini mtandao na kuwachukulia hatua wahusika na kwamba serikali haitaki kuona viwanja vya ndege hapa nchini vinakuwa kichochoro cha kupitishia dawa hizo.
 
Alisema serikali haitamuonea haya mfanyakazi yeyote wa viwanja vya ndege nchini atakayebainika kushiriki kula njama kufanikisha kusafirisha dawa za kulevya na kwamba atakayekamatwa mbali na kusimamishwa kazi pia atawekwa ndani kusubiri uchunguzi ufanyike kabla ya suala lake kupelekwa mahakamani.
 
WALIOFANYA SHEREHE BANDARINI WAONYWA
Katika hatua nyingine, Waziri Sitta, ametuma salamu kwa wafanyakazi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ambao wanadaiwa kufanya sherehe baada ya kuhamishwa Dk. Mwakyembe katika wizara hiyo.
 
Baadhi ya wafanyakazi wa TPA wanadaiwa kufanya sherehe kuhamishwa kwa Dk.Mwakyembe katika wizara ya Uchukuzi na kwamba ujio wa Sitta itakuwa mteremko kwao kuendelea na vitendo vya wizi kama ilivyokuwa awali kwa madai waziri Sitta hataweza kuwathibiti kama ilivyokuwa Mwakyembe.
 
"Nimepata taarifa kwamba baadhi ya wafanyakazi wa Bandari walifanya sherehe baada ya kusikia Dk. Mwakyembe amehamishwa katika wizara hii ya Uchukuzi, kicheko chao kitakuwa kilio chao na kina mwisho, waliodhani maji yamepoa wanajidanganya kwa kuwa maji sasa ndiyo yamechemka" alisema.
 
UCHUMI UPO KICHWA CHINI MIGUU JUU
Waziri Sitta akiwa katika Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara) alisema ni jambo la kushangaza kuona wakati nchi ina mtandao wa barabara zaidi ya kilometa 2000 na mizigo ya kusafirisha ipo lakini kila iku tunatembeza bakuli kuomba China.
 
"Uchumi wetu hivi sasa upo kichwa chini miguu juu,tunasafirisha mizigo kupitia barabara na barabara zinaharibika wakati baadhi ya mizigo tungeweza kusafirisha kwa reli,"alisema.
 
Aliongeza kuwa kila siku Waafrika wanachekwa na kwa bra serikali imejipanga kuhakikisha miundombinu ya reli inaboreshwa na kujenga reli mpya katika maeneo mbali mbali ili usafiri huo uwe wa uhakika.
 
Sitta alisema serikali itatafuta mwekezaji atakayeingia ubia na Tazara ambaye atapewa masharti ya kusafirisha mizigo itakayowezesha kupata fedha za kulipa mishahara wafanyakazi.
 
"Msiendelee na tishio la migomo,dawa ipo jioni,serikali haiwezi kuwatupa,itawalipa Haki zenu zote, jambo la msingi Tazara ifanye Kazi kwa kushirikiana na taasisi nyingine,serikali itahakikisha Kabla ya Oktoba Tazara itakuwa inakimbia na siyo kutembea,"alisema.
 
MABEHEWA MABOVU 
Akiwa Kampuni ya Reli Nchini (TRL), Sitta alisema tume zote za uchunguzi zilizoundwa na DK.Mwakyembe kuchunguza vigogo waliohusika na kununua mabehewa mabovu hatazivunja badala yake zitaendelea na kazi kama kawaida ili wahusika waweze kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa Sheria.
 
Dk.Mwakyembe akiwa katika Wizara ya Uchukuzi alidhibiti wizi mkubwa uliokuwa ukifanywa katika taasisi na idara zilizopo chini ya wizara hiyo hususani TPA ambako ilifikia wakati makontena ya mizigo ya wateja ilikuwa ikiyeyuka katika mazingira yenye utata. 
 
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment

 
Top