Anasema hali hiyo si nzuri na inatoa changamoto mpya katika vita
dhidi ya rushwa hasa kutokana na wananchi wengi kupoteza imani katika
vita hiyo, kwa kuwa ndiyo wanaoathirika moja kwa moja na hawaoni hatua
zozote madhubuti kukomesha na kuwashughulikia watuhumiwa wa matukio
hayo.
“Kwa viwango hivyo vya kimataifa, Watanzania
wamekuwa wakitoa mara chache chini ya wastani wa kimataifa katika
masuala yanayohusiana na ardhi kwa asilimia 10 ikilinganishwa na wastani
wa kimataifa wa asilimia 21 na asilimia tano katika elimu ambayo ni
chini ya wastani wa kimataifa wa asilimia 16,” inaeleza ripoti hiyo.
Uthibitisho huo unadhihirisha namna ambavyo
Watanzania wamekuwa wakisumbuliwa na kulazimishwa kutoa rushwa
wanapopata matatizo yanayohitaji huduma ya taasisi hiyo muhimu ya
usalama kwa umma ambayo inaendeshwa na Serikali kwa asilimia 100.
Mushi anasema Watanzania pia wamekuwa wakiingia
katika mtego wa kutoa rushwa baada ya kutembelea ofisi za Serikali au
watoa huduma katika sekta binafsi kama kamati za maji za vijiji,
mashirika yasiyo ya kiserikali, mashirika ya dini au shule zilizo katika
maeneo yao.
Katika mahojiano ya utafiti huo, idadi kubwa ya
wananchi walisema waliwahi kuombwa rushwa na watu watatu kati ya watano,
sawa na asilimia 60 waliombwa rushwa na polisi na mmoja kati ya watatu
(asilimia 34) waliombwa rushwa walipokuwa wakitafuta kazi.
Katika mahojiano zaidi kuhusu mara ngapi waliwahi
kuombwa rushwa, walisema polisi ndio wanaoongoza kwa kuomba rushwa na
asilimia 41 walitoa kwa kuambiwa na asilimia mbili walitoa bila
kuambiwa.
“Tatizo kubwa hapa ni kwamba wananchi wamepoteza
imani kabisa kwa sababu hata zile kesi kubwa za rushwa zinazoibuliwa,
mara nyingi zimekuwa zikipotelea hewani na hakuna anayewajibishwa,”
anasema Mushi na kuongeza:
“Hata Takukuru iliyopewa jukumu la kuchunguza haijapewa meno ya kutosha.
Wananchi walisema wazi kwamba wanapenda kuiona
taasisi hiyo ikiwa na uwezo wa kusimamia uchunguzi na hata kuendesha
kesi hizo yenyewe, yaani iwe na uwezo wa kufuatilia mwanzo hadi kutoa
uamuzi wa mwisho.”
Kwa kutumia utafiti wa kipimo cha rushwa duniani
wa 2013, uliofanywa na shirika la Transparency International, Watanzania
wamekuwa wakilipa hongo mara nyingi zaidi kwa maofisa wa polisi kuliko
wastani wa kimataifa ambao ni asilimia 34.
Uelewa wa wananchi kuhusu rushwa kubwa
Hata hivyo, wakati rushwa ikishtadi nchini,
Watanzania wengi hawana taarifa za kutosha na wengi zaidi hawajui kabisa
kuhusu kashfa kubwa za rushwa zinazoelezwa katika vyombo vya habari.
Hili ni suala gumu lililoguswa katika ripoti ya utafiti huo na
hadi matokeo yanatoka, asilimia zaidi ya 78 haikujua lolote kuhusu
kashfa ya IPTL, asilimia 74 haijui lolote kuhusu kashfa ya aliyekuwa
Katibu Mkuu wa Nishati, David Jairo na asilimia 67 hawajui lolote kuhusu
kashfa ya ununuzi wa rada.
Wengine ni asilimia 52 ambao hawajui lolote kuhusu
kashfa ya EPA na zaidi ya asilimia 44 ambao hawajui lolote kuhusu
kashfa ya Richmond.
Wastani huo unashtua kwa sababu kwa idadi hiyo
kubwa ya Watanzania wasiojua lolote kuhusu kashfa hizo kubwa za rushwa
zinazowagusa moja kwa moja viongozi waandamizi serikalini, zimekuwa
zikiripotiwa katika vyombo vya habari na kujadiliwa kwa kina bungeni na
kisha umma wa Watanzania.
Kwa wastani, matatizo mengi ya nchi yanapata
ukakasi katika kuyatatua hasa kashfa za rushwa kwa kuwa uelewa wa
wananchi uko chini, licha ya kutangazwa na vyombo vya habari na kutawala
mijadala ya kisiasa.
Katika utafiti huo, suala la rushwa katika sekta
za usalama, siasa, kodi, ardhi, afya, elimu, maji, Serikali za Mitaa,
mashirika yasiyo ya kiserikali, mashirika ya dini inawagusa zaidi ya
asilimia 50 ambao wamefikia hatua ya kuiona kama ni kitu cha kawaida.
“Wengi wamekuwa wakitoa rushwa wakiwa kwenye hali
tete, hasa wanapokutana na polisi au wanapohitaji huduma za uhakika za
afya na miongoni mwa wahojiwa watatu kati ya watano waliripoti kwamba
walishinikizwa kutoa rushwa walipokutana na polisi mara ya mwisho,”
inaeleza ripoti.
Uombaji rushwa unaoshika nafasi ya pili ni ule
unaowakabili wananchi wanapoomba ajira na sasa rushwa inatazamwa kama
kitu cha kawaida kabisa au cha kawaida kiasi kwenye huduma zote za
Serikali isipokuwa katika sekta ya maji pekee.
Udhibiti wa rushwa
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, wakati wafadhili,
wanasiasa na mashirika yasiyo ya kiserikali yakijikita kupambana na
kashfa kubwa za rushwa, wananchi wengi wanaangalia zaidi aina ya rushwa
inayowagusa moja kwa moja na kuathiri maisha yao ya kila siku.
Tatizo linaloonekana kuwa na athari ya moja kwa
moja ni namna tabaka la wasomi na wanasiasa wanavyoelekeza nguvu zao
katika rushwa wanazoziita kubwa na kutotilia maanani rushwa wanazoziita
ndogo ambazo ndizo zinazowagusa wananchi moja kwa moja katika maisha yao
ya kila siku katika huduma za polisi, afya, elimu na ardhi.MWANANCHI
Post a Comment