0

Doha, Qatar. Waziri Mkuu Mizengo Pinda anaendelea na ziara yake ya siku tatu nchini Qatar na kazi kubwa ni kutafuta wawekezaji katika sekta ya mafuta na gesi pamoja na maeneo mengine ya kiuchumi ikiwemo utalii na fursa za biashara.
Awali Waziri Mkuu alikuwa na ziara kama hiyo nchini Dubai kabla ya kukatisha ziara hiyo Alhamisi iliyopita baada ya kuitwa na Rais Jakaya Kikwete kwa shughuli maalumu.
Katika ziara hiyo hapa Qatar, Waziri Mkuu alipokewa kwa gwaride la heshima, atafanya mazungumzo na mawaziri watano; Naibu Waziri wa Nishati na suala kubwa linalotarajiwa kuzungumzwa ni kuhusu uvumbuzi wa mafuta na gesi.
Akiwa Dubai, Waziri Mkuu alikutana na maofisa watendaji wakuu wa Emirates National Oil Company (ENOC), Said Foemy na Fandraj Govindaraj kuzungumzia suala la uwekezaji katika sekta ya mafuta na gesi.
Mawaziri wengine anaotarajia kukutana nao ni; Waziri wa Masuala ya Uchumi, Waziri wa Vitegauchumi, Waziri wa Miundombinu na Usafirishaji na Waziri wa Kazi na Maendeleo ya Jamii.
Ratiba ya ziara hiyo iliyotolewa jana jioni inaonyesha, Waziri Mkuu kabla ya kukutana na mawaziri hao, leo Jumapili atakuwa na mazungumzo na mwenyeji wake, Waziri Mkuu wa Serikali ya Qatar, Sheikh Abdullah Nasser Al Thani.
Baada ya mazungumzo hayo, Waziri Mkuu na ujumbe wake, watapata chakula cha mchana na Waziri Mkuu huyo kabla ya kukutana na Watanzania wanaoishi Qatar baadaye jioni.
Ratiba inaonyesha kuwa kesho Jumatatu, Waziri Mkuu atatembelea Bandari ya Qatar na kufanya mazungumzo na maofisa wa bandari hiyo na baadaye mchana atakuwa na mazungumzo na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara wa Qatar, Jassim Bin Khalifa Bin Ali Thani pamoja na wanachama na wanajumuiya hiyo.
Waziri Mkuu pamoja na ujumbe wake, wanatarajia kurejea nchini Jumanne baada ya ziara hiyo ya siku tatu.MWANANCHI

Post a Comment

 
Top