Dar es Salaam. Tanzania inaadhimisha miaka 53 ya Uhuru leo huku wananchi wa kada mbalimbali wakiielezea siku hii kuwa haina uhalisia wa maisha ya Watanzania.
Rais Jakaya Kikwete atakuwa mgeni rasmi katika
hafla hiyo itakayofanyika katika Uwanja wa Taifa, ambako atakagua
gwaride la vikosi vya majeshi ya ulinzi na usalama na baadaye kuwatunuku
nishani za heshima kwa watu mbalimbali waliotumikia Taifa.
Katika maadhimisho hayo, pia kutakuwa na michezo
ya halaiki, sarakasi, ngoma za asili kutoka katika baadhi ya mikoa ya
Tanzania Bara na Zanzibar. Kaulimbiu ya mwaka huu ni; “Miaka 53 ya
uhuru; ingia katika historia ya nchi yetu; jitokeze kuipigia kura Katiba
Inayopendekezwa.”
Wakati hayo yakifanyika, wadau mbalimbali wameielezea miaka 53 ya Uhuru kwa mtazamo tofauti.
Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere
ambacho pia kinatimiza miaka 53 leo, Profesa Shadrack Mwakalila alisema
sherehe hizo zinafanyika wakati nchi inatajwa kukithiri kwa vitendo vya
ukosefu wa maadili kwa viongozi.
Alisema hali hiyo imechangiwa kwa kiasi kikubwa na
ukosefu wa mafunzo na elimu ya maadili kwa viongozi kama ilivyokuwa
siku zilizopita, hivyo kuna haja ya mafunzo hayo kurudishwa.
Alisema miaka ya 1971 hadi 1991 wakati chuo hicho
kikiitwa Chuo cha Chama Kivukoni, kilikuwa kinatoa mafunzo ya maadili na
uongozi kwa watendaji wote wa Serikali kabla hawajaenda kulitumikia
Taifa, hali ambayo sasa haipo na ndiyo inayochangia kinachotokea sasa.
Profesa Gaudence Mpangala wa Chuo Kikuu cha Ruaha,
alisema tofauti na mwaka 1972 hadi 1980 wakati elimu iliyokuwa
inatolewa ilikuwa na mwelekeo, kwa sasa kiwango kimeshuka kwa kiasi
kikubwa.
Alisema kuna sababu mbalimbali za kushuka, ikiwamo ukosefu wa walimu, motisha kwa walimu na zana za kufundishia.
Profesa Mpangala alisema pamoja na sasa kuwapo
vyuo vingi, tatizo kubwa ni ukosefu wa ajira... “Kila mwaka vyuo
vinamwaga wahitimu, lakini hawana kazi. Uchumi wa Tanzania hauwezi
kuwaandaa wasomi kuingia kwenye soko la ushindani… tatizo siasa
zinaingizwa kwenye elimu,” alisema.
Mtaalamu wa maendeleo na siasa Chuo Kikuu cha
Mzumbe, Dk Idd Makombe alisema miaka 53 ni mingi na kama nchi ilitakiwa
kuwa imepiga hatua zaidi kimaendeleo badala ya kuendelea kuwa maskini
duniani.
Alisema kuna nchi ambazo kipindi Tanzania inapata uhuru zilikuwa sawa nayo lakini leo zimepiga hatua.
“Ili kufikia malengo yanayoendana na miaka 53, tunahitaji kuwa
na viongozi wazalendo... tufanye kitu cha watu wote kiwe cha watu wote,
kwa sasa hili halipo.”
Mkurugenzi wa Sera wa Shirikisho la Wenye Viwanda
Tanzania (CTI), Hussein Kamote alisema sekta ya viwanda bado ina safari
ndefu ya kufikia Malengo ya Milenia 2025 ya kuwa na Pato la Taifa (GDP)
linalotokana na viwanda kuwa asilimia 15.
Alisema miaka 53 iliyopita, mchango wa sekta hiyo
katika GDP ulikuwa asilimia mbili, kwa sasa umefikia asilimia tisa
lakini bado kuna changamoto ambazo zinatakiwa kufanyiwa kazi.
Alisema Taifa likihakikisha umeme unapatikana wa
kutosha na wa bei nafuu, reli na bandari zikaimarishwa, tunaweza kupiga
hatua zaidi... “Lakini vyuo vitoe wanafunzi watakaokwenda kushindana
katika soko la ajira kwenye viwanda, ili miaka 10 au 15 ijayo tuweze
kuona matokeo chanya ya sekta ya viwanda.”
Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti ya Repoa,
Profesa Samuel Wangwe alisema kwa kipindi chote matatizo kama umaskini,
ujinga na maradhi ambayo yalitajwa kama maadui wa Taifa, hayajaisha na
kubakia kama changamoto zinazotakiwa kutatuliwa.
“Umaskini bado ni changamoto kubwa inayohitaji
kufanyiwa mageuzi, kilimo kiwezeshwe ili kiwasaidie Watanzania kuepukana
na maskini... maradhi na ujinga kwa kiasi fulani vimepiga hatua kwa
kipindi hiki cha miaka 53,” alisema Profesa Wangwe.
Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania
(MCT), Kajubi Mukajanga alisema sherehe za miaka 53 ya Uhuru
zingependeza kama kungekuwa na sheria ya kupata habari.
“Ingependeza kama tungekuwa na sheria ya habari,
lakini leo tunahuzunika kwa kukosa sheria hiyo ambayo ilikuwa ifikishwe
bungeni Aprili, mwaka huu lakini sasa itapelekwa Februari mwakani,”
alisema Mukajanga na kuongeza:
“Tuna masikitiko, tunaposherehekea miaka 53 bado
tuna sheria mbovu za kukandamiza uhuru wa habari ambazo hazijaondolewa,
ingawa, jambo pekee la kujivunia ni Katiba Inayopendekezwa imetaja uhuru
wa vyombo vya habari tofauti na Katiba ya sasa kubainisha haki ya
kupata habari kwa ujumla jumla... hatujui kama itapita au la, lakini
imependekeza hilo.”MWANANCHI
Post a Comment