0

090201-N-0506A-087
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.
BUNGE limeazimia kuwajibishwa kwa mawaziri Profesa Sospeter Muhongo, Profesa Anna Tibaijuka, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Jaji Frederick Werema, kutokana na sakata la uchotaji wa fedha katika akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu (BoT) kwa kutaka mamlaka ya uteuzi kutengua uteuzi wao.
Mbali na hao, yumo Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi na Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).
Aidha, Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameahidi kuwa Serikali itatekeleza maazimio yote manane yaliyopitishwa jana jioni na Bunge baada ya mjadala mkali wa siku tatu na mvutano wa siku moja juzi katika kupitisha maamuzi hayo ambayo yalifikiwa kwa maridhiano.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe alisoma maazimio hayo manane jana bungeni baada ya kufikiwa kwa maridhiano kati ya Kamati yake, Kambi ya Upinzani, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Serikali.
Maazimio
Katika azimio la pili, Zitto alisema viongozi hao wa umma na maofisa wa ngazi za juu serikali wanapaswa kuwajibika kwa sababu wamehusishwa na vitendo vya kijinai katika sakata hilo, linalohusisha kampuni ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania (IPTL).
“Kwa kuwa vitendo vya kijinai wanavyohusishwa navyo viongozi wa umma na maofisa wa ngazi za juu serikalini, vinakiuka pia maadili ya viongozi wa umma kuwanyima viongozi na maofisa hao uhalali wa kuendelea kushikilia nafasi za mamlaka katika uongozi wa umma;
“Hivyo, basi Bunge linaazimia kwamba Waziri wa Nishati na Madini,  Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini na wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Tanesco wawajibishwe, kwa kuishauri mamlaka ya uteuzi wao kutengua uteuzi wao,” alisema Zitto.
PAC katika mapendekezo yake bungeni, ilitaka Muhongo, Maswi, Jaji Werema, Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Stephen Masele na Waziri Mkuu Pinda wawajibike kutokana na sakata hilo, lakini wabunge wengi walisema Masele na Waziri Mkuu Pinda hawakuhusika katika sakata hilo.
Aidha, kwa mujibu wa Zitto, Bunge limeazimia kuwa Taasisi ya Kupambana  na Kuzuia Rushwa (Takukuru), Jeshi la Polisi na vyombo vingine husika vya ulinzi na usalama, vichukue hatua
stahiki kwa mujibu wa sheria  za nchi kwa watu wote waliotajwa kuhusika na vitendo vyote vya jinai, kuhusu miamala ya akaunti ya Tegeta Escrow, na watu wengine watakaogundulika baada ya uchunguzi mbalimbali unaondelea katika vitendo hivyo vya jinai.
Miongoni mwao ni mmiliki wa kampuni ya PAP, Harbinder Singh Sethi, James Rugemalira wa VIP Engineering Ltd, Jaji Werema, Profesa Muhongo, Maswi, wajumbe wa Bodi ya Tanesco, ambao inasemwa kuwa walihusika kwa namna moja au nyingine kufanikisha kufanyika kwa miamala haramu ya fedha katika akaunti ya Tegeta Escrow kwenda PAP na VIP Engineering and Marketing Ltd.
*Wabunge
Azimio jingine la Bunge ni kuazimia Kamati za Kudumu za Bunge
kuwawajibisha viongozi wake kwa kuwavua nyadhifa zao kutokana na kushiriki kwa namna moja au nyingine katika sakata hilo.
Hao ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bajeti Andrew Chenge, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Katiba, Sheria na Utawala, William Ngeleja na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Victor Mwambalaswa ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Tanesco.
Chenge na Ngeleja wametajwa kunufaika na fedha za mwanahisa Rugemalira kwa Chenge kupewa Sh bilioni 1.6 na Ngeleja Sh milioni 40.2, kwa mujibu wa taarifa ya CAG na PAC.
“Hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba Kamati husika za Kudumu za Bunge zichukue hatua za haraka na kwa vyovyote vile kabla ya Mkutano wa Kumi na Nane wa Bunge, kuwavua nyadhifa zao wenyeviti tajwa wa Kamati husika za Kudumu za Bunge,” alisema  Zitto.
*Majaji
Kuhusu ushiriki wa majaji katika kashfa hiyo, alisema Katiba ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, imeweka utaratibu mahsusi wa kushughulikia nidhamu ya majaji, ambao kwa mujibu wa Katiba hiyo, unamtaka Rais aunde Tume ya Uchunguzi ya Kijaji kuchunguza tuhuma za utovu wa maadili dhidi ya majaji.
Alisema kwa kuwa utaratibu wa kushughulikia nidhamu ya majaji kwa mujibu wa Katiba unamruhusu Rais kumsimamisha kazi Jaji au Majaji husika wakati wa tuhuma dhidi yake unaendelea;
“Hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aunde Tume ya Kijaji  ya Uchunguzi kuchunguza tuhuma za utovu wa nidhamu wa maadili dhidi ya Jaji Aloysius Mujulizi na Jaji Profesa Eudes Ruhangisa wa Mahakama Kuu ya Tanzania,” alisema Zitto.
Aidha, Bunge limeazimia mamlaka husika za kifedha na za kiuchunguzi kuitaja Stanbic Bank Tanzania Ltd na benki nyingine yoyote itakayogundulika baada ya uchunguzi wa mamlaka za kiuchunguzi, kujihusisha na utakatishaji wa fedha zilizotolewa katika akaunti ya Escrow, kuwa ni taasisi zenye shaka ya utakatishaji wa fedha haramu.
*Sheria
Katika azimio jingine, Bunge limeazimia kwamba Serikali iandae na kuwasilisha Muswada wa Marekebisho ya Sheria iliyounda Takukuru kwa lengo la kuanzisha taasisi mahsusi itakayoshughulikia, kupambana na kudhibiti vitendo vya rushwa kubwa, ufisadi, na hujuma za uchumi zinazotishia uhai wa Taifa kiuchumi, kijamii na kisiasa kutokana na kushamiri kwa vitendo hivyo.
Pia Serikali imetakiwa kutekeleza azimio la Bunge kuhusu mikataba mibovu ya kuzalisha umeme kati ya Tanesco na kampuni binafsi ya kufua umeme, hivyo basi Serikali imetakiwa kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mapitio ya mikataba ya umeme kabla ya kumalizika kwa Mkutano wa Bunge la Bajeti.
“Bunge linaazimia kwamba Serikali iangalie uwezekano wa kununua mitambo ya kufua umeme ya IPTL na kuimilikisha kwa Tanesco kwa lengo la kuokoa fedha za shirika hilo,” aliongeza Zitto katika maazimio hayo yaliyoridhiwa na Bunge zima baada ya kuandaliwa na watu 21.
*Pinda
Akiahirisha mkutano huo wa 16 na 17 wa Bunge, Waziri Mkuu Pinda  alisema CAG atapewa kazi mahsusi ya kufanyika kazi kujua kama fedha za Tegeta Escrow zilikuwa za umma, kwa maana alisema sehemu inaweza kuwa za Tanesco, IPTL au Serikali.
Source:Habarileo

Post a Comment

 
Top