0
 Bei ya korosho ghafi katika soko la minada chini ya mfumo wa stakabadhi ghalani imeimairika na kufikia Sh1,660 kutoka Sh1,500 kwa kilo katika wiki mbili zilizopita.
Akizungumza jana ofisini kwake, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Korosho nchini (CBT), Mfaume Juma amesema, mwenendo wa bei katika minada ya Novemba 17 hadi 30 umeonyesha kupanda.
“Tofauti na minada ya awali, bei ilionyesha kushuka kwa kufikia Sh1,500 kwa kilo, hizi wiki mbili bei imepanda ” alisema Juma na kuongeza;
“Kuimarika kwa bei kunatokana na wanunuzi kubaini uhakika wa ubora wa korosho zinazopitia mfumo wa stakabadhi ghalani...pia kutekelezwa kwa makubaliano ya matumizi rafiki ya bandari ya Mtwara, meli za kubeba korosho zimeshaanza kuwasili.”
Alisema jumla ya tani 139,123.77 za korosho ghafi zimekusanywa ikiwa ni ongezeko la tani 9,000 la korosho zilizokusanywa katika msimu uliopita hali inayoashiria kuongezeka kwa uzalishaji wa zao hilo.
“Msimu 2013/14 tulikusanya jumla ya tani 130,123.77 kiasi hiki kimeongezeka katika msimu huu na hadi sasa tumekusanya tani 139,123.77...bado wakulima wanazo korosho na ukusanyaji unaendelea hii ni dalili njema kwetu.”
Mkurugenzi huyo alisema pamoja na mafanikio hayo changamoto inayowakabili wakulima ni kulinda ubora wa korosho zao wakati wa kuhifadhi.
“Katika wiki mbili zilizopita tumebaini kupungua kidogo kwa ubora wa korosho kunakosababishwa na baadhi ya wakulima kuweka korosho katika viroba kabla ya kuzipeleka kwenye vyama vya msingi ...viroba vinatunza joto, korosho zinapoteza unyevu ni vyema wakahifadhi kwenye magunia.” ya katani au juti” alisisistiza Juma.MWANANCHI

Post a Comment

 
Top