0


SPIKA wa Bunge, Job Ndugai amewaapisha rasmi wabunge wanne wapya, watatu wakiwa ni wa Kuteuliwa na Rais na mmoja aliyeshinda kwenye Uchaguzi Mdogo wa hivi karibuni jimboni Dimani, visiwani Zanzibar.
Wabunge hao wapya walioapishwa ni Abdallah Bulembo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Profesa Palamagamba Kabudi ambaye ni msomi maarufu nchini na Anne Kilango Malecela aliyekuwa Naibu Waziri na Mbunge hadi kufikia Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Mwingine ni Ali Juma Ali ambaye kwa sasa ni Mbunge wa Dimani aliyechukua nafasi iliyoachwa wazi baada ya kifo cha Hafidh Ally Tahir kilichotokea Novemba mwaka 2016.
Ndugai alianza kwa kumuapisha kwanza Bulembo, akifuatiwa na Kilango, Profesa Kabudi na baadaye Ali ambao wote kwa pamoja baada ya kula kiapo hicho, walisalimiana na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.
Wakati wa uapisho huo, hali ya Bunge hilo ilitawaliwa na shamrashamra na vigelegele kutoka kwa wabunge waliokuwa wanawasindikiza wabunge hao wapya kuingia ukumbini kwa ajili ya kuapishwa.

Post a Comment

 
Top