0

Warren Buffett alizaliwa mwaka 1930 katika mji wa Omaha, Nebraska, Marekani. Baba yake mzazi Howard Buffett, alikuwa akiuza dhamana katika benki ya Union Street, Omaha 1931. Benki hiyo ambayo baba yake alikuwa ameajiriwa ilianguka na kufilisika hivyo kujikuta hana ajira na kupoteza akiba yote. Baba yake aliamua kuanzisha biashara ya udalali wa dhamana, huku akimsihi mwanae kusoma zaidi.

Warren Buffett alipokuwa shule ya sekondari aliwaeleza wanafunzi wenzake kuwa atakuwa milionea kabla ya kufikia umri wa miaka 35. Na alifanikiwa kuwa na dola milioni 6 alipofikia miaka hiyo 35. Warren alisoma shahada ya uzamili ya uchumi katika Chuo kikuu cha kolombia. Alijiunga na chuo hiki kwa kuwa alitaka afundishwe na mwalimu bigwa wa masuala ya uwekezaji, Benjamin Graham. Alipomaliza shahada ya pili, alijiunga katika biashara ya mwalimu wake Benjamin Graham. Akiwa chini ya mwalimu wake huyo aliweza kujifunza zaidi masuala ya uwekezaji.  Watu wengine alioweza kujifunza zaidi kutoka kwao ni Charlie Monger, Philip Fisher, Lawrence N. Boomberg, John B. Williams, Edga Smith, na John M. Keynes. Katika wote hao aliweza kujifunza masuala mbalimbali yanayohusiana na uwekezaji katika soko la fedha na masuala ya hisa.

Akiwa kijana mdogo sana, alipita mitaani kuuza kinywaji cha Coke, akibisha hodi nyumba kwa nyumba na kuweka akiba kwa kila fedha aliyokuwa akipata na hapo akiwa na umri wa miaka 6. Alinunua chupa moja ya Coke kwa senti 25 na kuuza kwa senti 50. Akiwa na umri wa miaka 11, alinunua hisa yake ya kwanza, hisa tatu (3) za kampuni ya Cities Service, kwa dola 38. Hisa zilishuka bei na kufikia dola 25, lakini hakubabaika katika hilo. Aliuza hisa zake baadaye na kupata faida ya dola 5. Lakini baadaye hisa hizi alizouza zilipanda bei na kufikia dola 200.

Alipofikia miaka 19, alianzisha biashara ya kuuza magazeti kwa chini ya saa mbili kwa kupitia mtandao wa kibiashara aliouanzisha na kujipatia dola 175 kwa mwezi, aliuza takribani magazeti 500 kila siku. Pia alijishughulisha na kuuza mipira ya gofu iliyopotea ili kuendelea kuongeza kipato chake. Aliwahi kumiliki gari ya Roll Royce kwa ubia na kujipatia dola 35 kwa siku.

Warren Buffett aliamua kuanzisha kampuni yake ya Berkshire Hathaway baada ya kugundua kuwa haitoshi kujifunza biashara kwa kusoma kitabuni au kuhudhuria kozi tu bali kwa vitendo zaidi. Hadi hapo alikuwa amefanikiwa kusoma kitabu maarufu cha uwekezaji (The Intelligent Investor), kitabu anachokiri hadi kesho kuwa kilimfungua maisha yake kuhusu uwekezaji mwaka 1950, hapo akiwa bado na miaka 19.

“Price is what you pay. Value is what you get.” -Warren Buffett
Alipotoka shuleni, alipenda sana kusoma magazeti yenye habari ya soko la hisa la Marekani (Wall street journals) na taarifa za mwaka za makampuni mbalimbali. Alisoma zaidi ya vitabu 100 vya uwekezaji kwa kipindi kifupi. Hata walimu wake shuleni, walipenda sana kumuuliza na kumwomba ushauri kuhusu uwekezaji. Pamoja na kupenda kusoma taarifa kuhusu masoko ya hisa na dondoo motomoto, majedwali na michoro hayakwenda vizuri sana. Hakuwa na mbinu na mikakati madhubuti ya uwekezaji mpaka alipompata mwalimu wake Benjamin Graham wa Chuo Kikuu cha Kolombia, mwaka 1950. Warren Buffett alikuwa na bidii shuleni na kupata alama za juu A+ wakati akisoma shahada ya pili ya uzamili ya uchumi.

Mwaka 1958 alinunua nyumba yake ya kwanza kwa dola 31,500 na bado anaishi katika nyumba hiyo hadi hivi leo. Ni mmiliki wa kampuni ya Berkshire Hathaway. Ni kati ya wakurugenzi watendaji wanaolipwa mshahara mdogo kwa mwaka dola 100,000 ukilinganisha na wakurugenzi wengine katika makampuni mengine makubwa duniani. Hupenda kula katika hoteli za kawaida kuliko kwenda hoteli za kifahari, na kinywaji chake akipendacho cha Coke. Warren siyo mfuja fedha na hana matumizi mabaya ya fedha na mojawapo ya tabia yake ni kuwa “fedha ni lazima ihifadhiwe na kutunzwa  vizuri (preservation of capital).’ Aliwahi kutoa takribani dola bilioni 30 kwa Bill na Melinda Gates Foundation kusaidia miradi ya maendeleo.

Hadi hivi sasa Warren Buffett ni tajiri wa tatu duniani akiwa ana utajiri unaofikia $60.8 Bilioni kwa mujibu wa jarida la Forbes la nchini Marekani. Nakumbuka siku moja nilisoma kijana mmoja aliwahi kumuomba ushauri afanye kitu gani ili aweze kufanikiwa, Warren Buffett alimwambia asome kurasa (pages 500) kwa siku. Hii ni wazi kuwa Warren anatuonesha umuhimu wa kusoma vitabu kama sehemu mojawapo ya kupata ufahamu na taarifa nyingi za kuweza kukusaidia kufanikiwa. Kama Warren anasoma kurasa 500 kwa siku pamoja ana kazi kubwa ya kuendesha kampuni aliyonayo, Jiulize mimi na wewe tunasoma kurasa ngapi kwa siku?

Mambo 5 Ya Kujifunza Kutoka Kwa Warren Buffett:
1: Umri wako mdogo si kigezo cha kuacha kuifata ndoto yako na kuitimiza.
Wapo watu wengi huwa wanaona kama kuna muda fulani maalum kwa ajili ya kutimiza ndoto zao walizonazo, wengine wanaamini umri wa kufanikiwa ni kuanzia miaka 45 au 50 nakuendelea. Wapo wanaoamini kuwa milionea au bilionea kwenye umri mdogo ni kitu kigumu sana, hapana. Warren Buffett akiwa na miaka 35 alikuwa tayari amefanikiwa kutimiza ndoto yake aliyokuwa nayo ya kuwa milionea. Unachopaswa kuelewa ni kufahamu unataka nini kwenye maisha yako, simamia kitu unachokipenda na shikilia ulichonacho hadi uone matokeo yakitokea juu yake. Usikubali umri uwe kikwazo cha kutimiza maono na ndoto yako kubwa uliyonayo katika maisha yako.

Kijana wa kimarekani Evan Spiegel ambaye ni mwanzilishi na mmiliki wa Snapchat ni miongoni mwa vijana wadogo duniani akiwa na umri wa miaka 25 hadi sasa, lakini ni miongoni mwa mabilionea duniani, mwenye utajiri unaofikia dola 2.1 bilioni (zaidi ya trilioni 5.2) na kumfanya kuwa kijana mdogo mwenye pesa nyingi zaidi. Mara baada ya kusoma katika shule ya crossroads, akamalizia elimu yake katika Chuo cha Stanford kilicho nchini Marekani. Baada ya kuona mitandao ya kijamii ikishika kasi, akamua kuungana na mwenzake Bobby Murphy kwa ajili ya kutengeneza mtandao wao wa kijamii wa Snapchat ambao umekuwa maarufu duniani kwa sasa. Umri wako si kigezo cha kushindwa kufuata na kutimiza ndoto zako, amini unaweza na amka leo kuifata ndoto yako pasipo kusubiri kesho.

2: Tafuta maarifa na taarifa sahihi juu ya eneo unalotaka kufanikiwa.
Mara nyingi watu wengi wamejaribu kuingia kufanya biashara au uwekezaji fulani pasipo kupata taarifa sahihi zenye kuweza kuwasaidia katika kufanikiwa vyema katika maeneo hayo. Hii ndio sababu ya watu wengi kuishia njiani na kushindwa kufanikiwa katika vitu vingi wanavyoanzisha na kuanza kufanya. Warren Buffett alijifunza uwekezaji wa Hisa baada ya kujenga tabia ya kusoma vitabu zaidi na mojawapo ya vitabu alivyovisoma na kumpa maarifa aliyokuwa akitaka, The Intelligent Investor, Security Analysis, na Common Stock and Uncommon profits. Jiulize ni mara ngapi umetoa muda wa kujifunza au kutafuta ujuzi fulani kwa ajili ya kufanikisha malengo na ndoto yako kubwa uliyonayo?
Kwa mara ya kwanza nilishangaa sana kusikia Warren Buffett anasoma kurasa 500 kwa siku. Hii ni wazi tajiri huyu anafahamu umuhimu wa maarifa katika kumsaidia kufanikisha malengo yake aliyonayo. Watu wengi wanaotaka kufanikiwa leo hii si wepesi wa kujitoa katika kutafuta maarifa na taarifa sahihi kwa gharama yoyote ili kujijenga kiufahamu katika vitu wanavyotaka kuvifanya. Jiulize mara ya mwisho kusoma kitabu ilikuwa ni lini? Huwezi kuvuka eneo moja kwenda eneo jingine kwa kupitia ufahamu au maarifa yale yale uliyokuwa nayo tangu mwaka jana.

“Some people dream of success, while others wake up and work hard at it.” -Mark Zuckerberg
3: Kuwa karibu na watu wenye uwezo kwa ajili ya kukuongoza na kukushauri.
Kuwa karibu na watu wenye uwezo na uzoefu kuliko wewe kunaweza kukusaidia katika kukupa mbinu nyingi zaidi za kukuwezesha kuvuka vikwazo na changamoto kwa wepesi ili kufanikisha ndoto yako. Usijaribu kutafuta mchawi wa mafanikio yako kwa kujaribu kufanya kila kitu peke yako, ili uvuke changamoto zinazoonekana ni ngumu kwako ni vizuri zaidi utafute watu walio na uwezo na uzoefu kuliko wewe ili wakushauri mara kwa mara katika kitu unachotaka kukifanya. Jifunze kuwa na mshauri (mentor) kwenye kila eneo unalotaka kufanikiwa katika maisha yako.

4: Ili ufanikiwe kifedha unahitaji kuwa mwangalifu katika matumizi yako ya fedha ya kila siku.
Warren Buffett hakutokea familia yenye uwezo sana ila baba yake alikuwa mfanyakazi wa benki kabla benki hiyo haijafilisika na kutafuta kazi nyingine ya kufanya ili kujipatia kipato. Akiwa na miaka 6 Warren ndio alipoanza kuzunguka mitaani na kuuza kinywaji cha Coke, na kila fedha aliyoipata alijifunza kuihifadhi kwa kuweka akiba hadi pale alipotimiza miaka 11 akaanza kununua hisa. Hii inatuonesha wazi kuwa Warren Buffett alikuwa ni kijana smart na mwangalifu sana katika matumizi yake ya fedha na hiki ndio kitu kilichomsaidia kufikia kuwa milionea akiwa na miaka 35 kama alivyowatamkia wenzake akiwa shuleni.

Leo hii jiulize ni mara ngapi unapopata fedha baada ya kujishughulisha na kitu fulani unachofanya huwa unaheshimu na kutumia fedha zako kwa matumizi muhimu ili kutoa nafasi ya kuweka akiba na kuongeza thamani ya fedha yako kuongezeka. Usipojifunza namna nzuri ya matumizi ya fedha zako utabaki kuota ndoto za utajiri pasipo kuona uhalisi wowote katika maisha yako. Hakuna utajiri anaoweza kuupata mtu nje ya nidhamu anayoweza kuijenga katika matumizi yake ya fedha. Jifunze kuweka akiba na kujua njia nzuri za kuwekeza fedha zako mahali sahihi palipo na faida ili kukutengenezea utajiri mkubwa.

5: Jifunze kutoa kuliko kupokea.
Warren Buffett inakadiriwa ndio tajiri aliyewahi kuweka historia ya kurudisha fedha nyingi zaidi kwa jamii baada ya kutoa takribani dola bilioni 30 kwa Bill na Melinda Gates Foundation kusaidia miradi ya maendeleo. Hii ni wazi kuwa tajiri huyu anafahamu siri kubwa ya kufanikiwa zaidi ni kurudisha kwa jamii kile alichonacho. Kumbuka ili ufanikiwe zaidi unahitaji kujifunza namna ya kutoa kuliko kupokea tu. Kutoa ni pamoja na kidogo ulichonacho sasa, usisubiri ufanikiwe kama Warrren Buffett ndio uanze kujifunza kutoa. Anza kujenga tabia ya kutoa kuanzia sasa ili utakapofanikiwa kesho watu wengi wazidi kufaidi matunda ya kufanikiwa kwako.

Post a Comment

 
Top