0


Karibu tena ndugu na rafiki yangu katika wakati mwingine wa Kuelimishana katika eneo maalumu la ujasiriamali na biashara. Leo nataka tuangazie mambo sita muhimu yanayoweza kukusaidia kama mfanyabiashara katika kuifanya biashara yako kuendelea kuishi. Ninaposema biashara kuendelea kuishi, nina maana ya kuendelea kuishi kweli kweli na si nje ya hapo; kwani kila biashara uzaliwa, ukua na wakati mwingine inaweza kufa pale ambapo tu mwenye nayo hatokuwa mwangalifu katika kuilea na kuzingatia kanuni za kuikuza na kuindeleza kwa ufanisi.
Zipo biashara nyingi zilizoazishwa na badae kufa kwa muda mfupi baada ya kuanzishwa na badae kutokana na kukosa usimamizi mzuri na wakutosha zikasababisha kuanguka na kufa moja kwa moja. Wewe mwenyewe ni shahidi yawezekana unafahamu baadhi ya biashara zilizokumbwa na tatizo hili, na kushindwa kufikia hatua ya juu ya mafanikio na malengo yake. Yapo makampuni binafsi na hata ya kiserikali yalipokosa usimamizi mzuri na wakutosha yalikufa na hadi leo yamepotea na kubaki kuwa historia tu.
Je, unazani ni nini kinachosababisha kampuni na biashara nyingi kuanguka na kufa kwa muda mfupi? Hili ndio swali linaloleta majibu sita ambayo yanazaa makala hii na mafundisho haya ya wazi kwa njia ya mtandao siku ya leo. Nimekuandalia kwa ufupi mambo sita ambayo yanaweza kuisadia kampuni yako kuishi, na kuzuia kuanguka; lakini katika mambo haya sita tambua usipoyafanya na kuyazingatia yanaweza kusababisha biashara au kampuni yako kufa na kutokufikia katika mafanikio makubwa unayoyahitaji katika biashara yako.
Jambo la Kwanza:
Kuwa na Maono halisi ya Unachokitaka.
Biashara yoyote ile inahitaji kuwa na maono na picha halisi ya kile inachokifanya katika soko lake, iwe ni katika soko la bidhaa au huduma. Ni vyema kila mtu asimamie maono na melengo makuu ya kuanzisha biashara yake aliyonayo. Yawezekana una biashara au hauna biashara lakini nataka uzingatie kanuni kuu ya kutazamia unachokifanya au ulicholenga kukifanya dhidi ya wateja wako sokoni.
Maono ni muhimu sana katika kuiongoza biashara yoyote ile katika kufikia mafanikio na malengo yake makubwa iliyojiwekea. Kama unahitaji biashara yako iwe sehemu ya kuendelea kuishi na kubaki sokoni ni vizuri uzingatie maono halisi yaliyokufanya uanzishe biashara yako uliyonayo sasa.
Jambo la Pili:
Jitoe Kikamilifu katika Biashara yako.
Nataka nikuongezee jambo hili; kumbuka kwamba kujitoa kunaenda na kupenda. Hivyo kama unataka kuendelea kubaki sokoni na kuwa kinara katika kulitawala soko ni vizuri ujitoe kikamilifu katika kuijali na kuipenda biashara yako unayoifanya siku zote. Huwezi kufanikiwa katika biashara yako kama wewe binafsi hutaki kutoa nafasi ya kupenda kile unachokifanya.
Jifunze kujitoa na kupenda kile kitu unachokifanya. Kwa kufanya hivyo utajisaidia binafsi kuwa na nidhamu ya kufanya biashara yako au kitu hicho pasipo kukata tamaa hata pale inapofikia kutokwenda vizuri kimauzo na masoko. Biashara ni kama mtoto anayehitaji malezi mema ili akue vizuri na kufikia hatua njema ya kujitegemea.
Jambo la Tatu:
Tambua Hasara (Risk) ni sehemu ya biashara.
Unashangaa kusikia jambo la namna hiyo. Nataka nikuambie kuwa; mfanyabishara makini huwa hakimbii wala haogopi hasara zinazotokea katika biashara yake, bali anatafuta namna ya kukabiliana na hasara hizo pale zinapojitokeza. Kikubwa ni kuangalia ukubwa na kiwango cha hasara inayotokea isizidi uwezo wote wa biashara. Kuna hasara (Risk) ambazo kila biashara kwa sehemu yake inaweza kuziendesha na kuziepuka (Manage and Control Risk).
Angalia husiwe mwoga unapokutana na hasara ndogo kwa kuhofia kuanguka, bali fahamu namna ya kuziendesha na kuziepuka hasara hizo ili uweze kufikia mafanikio makubwa katika biashara yako na kuifanya biashara yako kuendelea kuishi.
Jambo la Nne:
Kuwa Mwenye shauku zaidi.
Kama hauna shauku ya kufanikiwa basi hautoweza kuisaidia biashara yako kukua, bali utakuwa sababu kubwa ya biashara yako kufa. Matamanio ya Mafanikio kwa ajili yako binafsi na biashara yako ni ya muhimu sana katika kukupa msukumo wa ndani wa kujituma na kufanya kazi kwa bidii, ili uweze kufikia mafanikio makubwa kwa ajili yako binafsi na biashara yako.
Jifunze kuwa na shauku kamili ya kutimiza maono na malengo yako uliyonayo katika biashara na kwako binafsi; hii itakujengea kujituma, kutokukata tamaa na kujikubali binafsi katika kile unachokifanya. Kwa kufanya hivyo utakuwa na nguvu ya kuitumikia biashara yako kwa moyo wako wote na kuwa sababu ya kuzuia anguko na kufa kwa biashara yako.
Jambo la Tano:
Fanya Mpango-Biashara (Business Plan) kuwa kiongozi wako.
Hapa ninaongea na wewe unayefanya biashara au kumiliki kampuni iliyo na mipango muhimu na maalum kwa ajili ya miaka mitano, kumi, ishirini hadi maisha. Ni muhimu kutumia mpango biashara wako ulionao kama mwongozo katika kukusaidia kuiendesha na kuiendeleza biashara au kampuni yako hadi kwenye mafanikio makubwa unayoyahitaji wewe binafsi, kama mbeba maono wa biashara au kampuni husika.
Ndio maana kuna umuhimu kila kampuni au mmiliki wa biashara kufahamu umuhimu wa kuwa na mpango biashara wa kampuni au biashara yake, ili kumsaidia na kumwongoza katika mafanikio makubwa ya kutimiza maono na malengo ya kampuni yake husika.
Jambo la Sita:
Kubali mabadiliko yanayojitokeza.
Ninapozungumzia suala la mabadiliko fahamu ninazungumzia suala zima la kukubaliana na ujio wa teknolojia na hali ya mfumo mzima wa kukabiliana na ushindani mkubwa wa kuwepo kwa taarifa nyingi, zinazoongeza watu kufanya kazi usiku na mchana ili kukubiliana na soko la dunia ya leo. Usipokubali kuenenda na mfumo huu, uwe na uhakika utashindwa kufanikiwa katika biashara na utakuwa sababu ya kuiua biashara yako kirahisi.
Usikimbie mabadiliko ya kiteknolojia katika ufanyaji wa kazi katika biashara yako; bali tafuta namna bora ya kuendana nayo ili uweze kushindana katika soko na kuifanya biashara yako iendelee kuishi na kusonga mbele zaidi. Nataka nikuambie kwa dunia ya sasa ushindani wa kibiashara umeongezeka na utaendelea kuongezeka ukichangiwa kwa sehemu kubwa na ongezeko la kuwepo kwa teknolojia na taarifa nyingi duniani. Hivyo hutakiwi kuwa nyuma katika hilo na kusema hutaki kuendana na hali hiyo inayojitokeza; fahamu kwa kufanya hivyo kwa sehemu kubwa utaua biashara au kampuni yako.
Hadi kufikia hapo nakutaka uchukue hatua ya kutekeleza yale yote uliyojifunza katika makala hii, ili uweze kuifanya biashara yako kuendelea kuishi na kuzuia anguko la kufa na kupotea katika soko. Hadi siku nyingine tutakapokutana tena kwa makala nyingine nzuri zaidi za biashara na ujasiriamali; nikutakie siku njema na mafanikio mema katika biashara yako.

Post a Comment

 
Top