KATIBU
Mkuu wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE), Dk Prime Nkwela na
watendaji wa baraza hilo, wamepewa siku 30 kukagua vyuo vyote nchini,
kujiridhisha na usajili na utoaji wa elimu katika vyuo hivyo.
Agizo
hilo limetolewa na Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi,
Profesa Joyce Ndalichako. Alilitaka baraza hilo kuhakikisha linapata
mwongozo bora katika kuvipandisha vyuo hadhi, kwani sio kila chuo
kinaweza kuwa chuo kikuu.
Profesa
Ndalichako alisema hayo jana wakati akizungumza na watendaji wa Baraza
hilo baada ya kuzungumza na watendaji wa Taasisi ya Elimu Tanzania
(TET). Alisema kuwa wizara itakaa kuangalia mahitaji ya Taifa, kwani
bado linahitaji wasomi kutoka ngazi mbalimbali, ikiwemo astashahada na
stashahada kwa ajili ya kufanya shughuli mbalimbali.
Alisema
suala la utoaji wa elimu bora, linatakiwa kuangaliwa kwa upana zaidi,
kwa kuwa elimu iliyopo ipo katika makaratasi na sio katika vichwa vya
wanafunzi waliohitimu.
Alisema
wapo baadhi ya wahitimu wa elimu ya juu, ambao hawajulikani wanafanya
nini, hivyo inapaswa kutoa elimu inayolingana na mahitaji kwa wanafunzi
kuweza kufanya kitu chochote.
‘’Unapozungumzia
udhibiti wa elimu unapaswa kuangalia kama elimu inayotolewa ina manufaa
kwa wanafunzi au inaishia katika makaratasi. Mwanafunzi anaweza akajaza
kitu katika makaratasi ya mitihani na kufaulu vizuri, lakini hana kitu
alichoingiza katika kichwa chake,’’ alisema Profesa Ndalichako.
Alieleza
kuwa baraza linatakiwa kutoa mwelekeo kwa Watanzania kwamba wanahitaji
vyuo vya ufundi na vigezo vyake ni vipi ili watanzania wenye sifa waweze
kujiunga.
Alifafanua
kuwa watendaji wa NACTE, wanatakiwa wanaposajili vyuo vya elimu na vya
ufundi, wawe tayari kupeleka watoto wao kujifunza katika vyuo hivyo.
Alisema maofisa wasio wazalendo, wanasajili vyuo kwa kuona kuwa ni
biashara, ambapo hata mtoto wake anamshauri akasome katika vyuo vizuri
tofauti na alichokisajili.
‘’Sekta
ya elimu imewekwa kwa ajili ya kuongeza uzalishaji mali, utoaji wa elimu
bora na sio soko. Nawaomba mkague vyuo vyote vilivyopo na mhakikishe
kuwa hakuna chuo ambacho kina shaka yoyote ili tuweze kufikia malengo ya
kuwa na elimu bora,’’ alisema.
Akizungumzia
udahili wa wanafunzi, Profesa Ndalichako alisema kuwa vyuo ambavyo vipo
nje ya mfumo wa NACTE katika kuhakiki taarifa zao, ndio chanzo cha kuwa
na mianya ya udanganyifu. Alisema vyuo vyote vinatakiwa kuingizwa
katika mfumo huo ili kupunguza udanganyifu wa vyeti vya kujiunga na
vyuo.
Post a Comment