0

 

MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) unakamilisha maandalizi ya kupelekwa madaktari bingwa katika visiwa vya Unguja na Pemba.
Kauli hiyo ilitolewa  na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa mfuko huo, Michael Mhando wakati  akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi katika hafla ya kutoa kadi za kikoa kwa wanachama 260 iliyofanyika Jang'ombe jana.
Hafla hiyo  iliandaliwa na Mbunge wa Jimbo la Jang’ombe Ali Hassan King kuashiria kuanza kwa matibabu ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kwa mpango wa Kikoa ambao ni mpango wa hiari wa huduma za matibabu unaosimamiwa na NHIF.
Alisema madaktari hao watapelekwa katika maeneo ambayo watakubaliana na wenzao wa Zanzibar.
"Tunao mpango wa kutoa huduma za kibingwa kwa kutumia madaktari bingwa ambao tutawapeleka maeneo tutakayokubaliwa ili kutoa huduma hizo kwa wanachama wa mfuko na wananchi wote kwa ujumla. Kazi hii tutaifanya hapa Unguja na tutaifanya vilevile Pemba," alisema.
Alisema hayo yatawezekana baada ya kushauriana na wenzao wa Hospitali ya Mnazi Mmoja na Al-rahma namna bora ya kufanikisha huduma hiyo.
Alisema lengo la kutoa huduma hizo ambazo kwa upande wa Tanzania Bara, wiki ijayo wataifanya mkoani Ruvuma ni kuwahudumia wananchi hata kama ni kwa vipindi vifupi lakini wawezeshwe nao kupata huduma hizo ambao mara nyingi zinapatikana katika hospitali za rufaa.
Aidha katika hotuba yake hiyo alisema kwamba wana mpango wa kuanza kutumia huduma za madaktari bingwa waliostaafu kazi, ili waone namna bora kuweza kuwatumia katika programu za kuhudumia katika maeneo mbalimbali yanayohitaji ujuzi wao.
Akizungumzia huduma za NHIF katika visiwa hivyo Kaimu Mkurugenzi mkuu huyo alisema kwamba wanatoa huduma za matibabu kwa wanufaika zaidi ya 43,056 waliopo Unguja na Pemba wengi wao wakiwa ni watumishi wa Serikali ya Muungano na familia zao.
Naye Naibu Waziri wa Afya, Mahmoud Thabit Kombo, alisema SMZ inaangalia utaratibu wa kuwaingiza watumishi wake kwenye Bima ya Afya. Aidha alimshukuru Mbunge wa Jang'ombe Ali Hassan King kwa kuwajali wazee.

Post a Comment

 
Top