0

Iran yawaachilia huru wanamaji wa Marekani

  • Dakika 29 zilizopita
Iran 
Boti ya Marekani aina ya Riverline, ambayo ni sawa na mbili zilizokamatwa na Iran
Wanajeshi wa Iran wamewaachilia huru mabaharia 10 wa Marekani waliokuwa wamekamatwa na kuzuiliwa kwa kuingia eneo la bahari la Iran, runinga ya taifa imeripoti.
Walikamatwa Jumanne wakiwa kwenye boti mbili, baada ya boti moja kupata hitilafu za kimitambo wakati wa mazoezi, Marekani imesema.
Taarifa iliyosomwa runingani nchini Iran imesema wanamaji hao wameachiliwa na kuruhusiwa kuingia eneo la bahari la kimataifa baada yao kuomba radhi.
Afisa wa Marekani amethibitishia shirika la habari la Reuters kwamba mabaharia hao wameachiliwa huru.
Waliingia maeneo ya Iran bila kukusudia, taarifa kutoka kwa wanajeshi wa Revolutionary Guards iliyonukuliwa katika runinga ya taifa imesema.
Awali, kamanda wa kikosi cha wanamaji cha Revolutionary Guards, Jenerali Ali Fadavi, alikuwa amesema uchunguzi ulikuwa umeonyesha hitilafu katika mitambo ya kuelekeza boti zilichangia.
"Tumethibitisha kwamba kuingia kwa Wamarekani hao maeneo yetu ya bahari hakukuwa uchokozi au kwa kusudi la kupeleleza au masuala husika,” aliambia runinga ya taifa ya Iran.
  Wanabaharia
Wanabaharia hao walikuwa wamezuiliwa kisiwa cha Farsi
Waziri wa mashauri ya kigeni wa Marekani John Kerry alimpigia simu mwenzake wa Iran Javad Zarif muda mfupi baada ya kisa hicho kutokea.
Wawili hao waliunda urafiki baada ya mazungumzo yaliyofanikiwa kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran.
Waliozuiliwa, wanaume tisa na mwanamke mmoja, walikuwa wamepelekwa kisiwa cha Farsi, katika Ghuba ya Uajemi, ambako Iran ina kambi ya wanajeshi wa majini.
Wanajeshi wa Revolutionary Guards wamekuwa wakitumiwa kulinda serikali ya Kiislamu ya Iran pamoja na kuzuia uingiliaji kutoka kwa mataifa ya kigeni na kuzuia mapinduzi ya kijeshi na maasi tangu mapinduzi ya 1979.
Taifa hilo huwa pia na wanajeshi wa kawaida ambao hulinda mipaka na kudumisha amani na utulivu ndani ya nchi.
 
Wanajeshi hao wa Revolutionary Guards wamekuwa wakilinda wa ukali mipaka ya Iran baharini.
Wanabaharia 15 kutoka Uingereza walizuiliwa kwa siku 13 mwaka 2007 baada ya kukamatwa wakiwa eneo la bahari linalozozaniwa kati ya Iran na Iraq.
Licha ya mafanikio makubwa mwaka jana kuhusu mkataba wa nyuklia, uhasama bado umeendelea baina ya Marekani na Iran.

Matukio manane makuu uhusiano kati ya Marekani na Iran

1953 Kupinduliwa kwa Mossadeq
Matatizo yalianza kati ya Iran na Marekani mwaka 1953 wakati waziri mku wa Iran aliyekuwa amechaguliwa kidemokrasia Mohammad Mossadeq alipinduliwa wakati wa mapinduzi yaliyoungwa mkono na mashirika ya ujasusi ya marekani na uingereza. Kiongozi huyo alikuwa na mipango ya kutaifisha sekta ya mafuta ya nchi hiyo.
1979 Mapinduzi ya Iran
Shah aliyekuwa akiungwa mkono na Marekani Mohammed Reza Pahlavi alilazimishwa kuihama nchi hiyo tarehe 16 mwezi Januari mwaka 1979 kufuatia miezi kadha ya maandamano na migomo ya kupinga uongozi wake. Kiongozi wa kiislamu Ayatollah Khomeini alirejea kutoka uhamishoni na kupata ushindi mkubwa katika kura ya maoni. Jamhuri ya kiislamu ya Iran ilitangazwa tarehe mosi mwezi Aprili.
1979 Kuvamiwa kwa ubalozi wa Marekani
Uhusiano ulidhoofika zaidi mwezi Novemba mwaka 1979 wakati wanafunzi wa kiislamu walivamia ubalozi wa Marekania mjini Tehran na kuwashika mateka raia kadha wa Marekani. Wanafuzi hao walikuwa wakita Shah wa Iran afukuzwe kutoka Marekani ambapo alikuwa amepelekwa kupata matibabu ya ugonjwa wa saratani baada ya kupinduliwa. Mateka hao 52 waliachiliwa mwaka 1981 baada ya siku 444 za kushikwa mateka.
  Mateka
Mateka hao wa Marekani walizuiliwa siku 444
1988 Kudunguliwa kwa ndege ya abiria
Tarehe tatu mwezi Julai mwaka 1988 meli ya kivita ya Marekani iliidungua ndege ya abiria ya Iran katika Ghuba. Marekani ikasema kuwa ndege hiyo ilidunguliwa kimakosa ikidhaniwa kuwa ndege ya jeshi la wanahewa. Watu wote 290 waliokuwa ndani ya ndege hiyo waliuawa wenge wakiwa ni raia wa Iran waliokuwa wafarini kwenda kuhiji mjini Mecca.
2002 - Uovu na hofu ya nyuklia
Katika hutuba yake kwa taifa mwaka 2002 rais wa Marekani George Bush alizitangaza Iran , Iraq na Korea kaskazini kama nchi zinazotenda maovu. Hotuba hiyo ilizua ghadhabu nchini Iran. Marekani pia iliilaumu Iran kwa mpango wake wa nyuklia mpango ambao Iran iliukana. Hata hivyo kundi moja la upinzani nchini Iran lilifichua kuwa nchi hio ilikua ikijenga vituo vya kinyuklia katika eneo la Natanz.
2010 Kuipinga hotuba ya Ahmadinejad katika UN
Akihutubia baraza la usalama la umoja wa mataifa mjini New York rais wa Iran Mahmoud Ahmadinejad alidai kuwa watu walikuwa wanaamini kuwa Marekani ilihusika kwenye mashambulizi ya Septemba 11. Marekani na waakilishi wa nchi za muungano wa Ulaya ,Canada, Australia, New Zealand na Costa Rica waliondoka wakati Ahmadinejad alikuwa akitoa hotuba na Marekani ikapinga vikali matamshi yake.
2013 Simu kati ya Obama na Rouhani
  Obama
Obama alizungumza na Rouhani kwa simu
Wiki chache baada ya kushinda urais nchini Iran mwaka 2013, Hassan Rouhani alizungumza na rais wa Marekani Brack Obama kwa njia ya simu. Hayo ndiyo mawasiliano ya kwanza kati ya rais wa Iran na Marekani tangu miaka 30 iliyopita. Wawili hao walizungumzia njia za kutatua tofauti za muda mrefu kuhusu mpango wa nyuklia nchini Iran.
2015 Iran yaafikia makubaliano ya nyuklia
Baada ya miaka kadha ya mazungumzo Iran iliafikia makubaliano na mataifa makubwa duniani kupunguza shughuli zake za nyuklia ili iweze kuondowewa vikwazo. Marekani, Uingereza, Ufaransa, China, Urusi na Ujerumani waliiitaka Iran isitishe shughuli zake za nyuklia ili isiweze kuunda bomu la nyuklia.
Iran imesema kuwa mipango yake ya nyuklia ni ya amani

Post a Comment

 
Top