Katibu Mkuu wa CUF ambaye ni Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim
Seif Sharif Hamad akionyesha fomu za kuwania nafasi ya urais wa kisiwa
hicho kupitia chama hicho baada ya kukabidhiwa na Katibu wa chama hicho
wa Wilaya ya Magharibi, Saleh Muhammed Saleh. Kulia ni Makamu
Mwenyekiti wa chama hicho, Duni Haji. Picha na CUF
Zanzibar. Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi
(CUF), Maalim Seif Sharif Hamad jana alichukua fomu ya kuomba kuteuliwa
na chama hicho kugombea urais wa Zanzibar kwa mara ya tano huku akisema
ushindi wake hautachezewa na mtu.
Mara ya kwanza Maalim Seif aliwania urais wa
Zanzibar mwaka 1995 na amekuwa akifanya hivyo katika chaguzi
zilizofuatia na sasa anawania tena kuingia Ikulu Oktoba.
Baada ya kuchukua fomu katika ofisi za chama hicho
zilizopo Bububu jana, Maalim Seif alisema ataheshimu matokeo ya urais
endapo uchaguzi utakuwa huru na wa haki.
Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais
wa Zanzibar, alisema matarajio yake makubwa katika uchaguzi ujao ni
kwamba utafanyika katika mazingira ya amani na utulivu.
Alisema ni matumaini yake kwamba mara hii ataongoza na kuibuka kuwa rais endapo uchaguzi utakuwa huru na haki.
“Kama wananchi wa Zanzibar watanipigia kura kwa
wingi nawahakikishia hakuna mtu yeyote atakayechezea ushindi wangu,”
alisema Maalim Seif.
Akizungumzia afya yake kuelekea Uchaguzi Mkuu,
Maalim Seif alisema anagombea nafasi hiyo akiwa mzima wa afya na hana
shaka, hivyo wananchi waondoe hofu katika hilo.
“Nachukua fomu ya urais na matarajio yangu makubwa
ni kushinda katika uchaguzi mkuu ambao utafanyika katika mazingira ya
amani,” alisema.
Kuhusu masuala ya uchumi, alisema atahakikisha ajira zaidi kwa vijana zinaimarishwa na kuongeza maeneo huru ya uchumi.
“Hivyo ndivyo vipaumbele vyangu nikichaguliwa na wananchi wa Zanzibar kuwa Rais katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa,” alisema.
Hafla ya Maalim Seif kuchukua fomu ilihudhuriwa na
viongozi mbalimbali wakiwamo mawaziri katika Serikali ya Umoja wa
Kitaifa kutoka CUF. Maalim Seif aliwataka wanachama wengine kujitokeza
kugombea nafasi hiyo kwa kuwa ni haki yao kikatiba.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
Post a Comment