0

Tunawaunga mkono wabunge waliojitokeza kupinga kuwasilishwa kwa hati ya dharura muswada wa Sheria ya Kupata Habari wa mwaka 2015.
Wakizungumza bungeni juzi, baadhi ya wabunge waliihoji Serikali sababu ya kuharakisha kuwasilisha muswada huo kwa ajili ya kupitishwa kama sheria.
Si wabunge pekee, wadau wa sekta ya habari wanajiuliza kuhusu uharaka wa muswada huo ambao kimsingi si suala la jana au juzi. Ni suala la muda mrefu ambalo wadau wa habari wamekuwa wakilipigania.
Ikiwa muswada huu utawasilishwa kwa njia ya hati ya dharura, ina maana utasomwa kwa mara ya kwanza na kupitishwa vipengele vyote kwa siku moja. Hii ina maana kuwa si wadau wa habari wala watunga sheria wetu, watakaopata muda wa kutosha wa kuupitia muswada na kujiridhisha kuwa una kila sababu ya kuwa sheria kwa maendeleo ya sekta ya habari na wanahabari.
Aidha, wadau wa habari kama wataalamu wa sekta hiyo, watakosa fursa ya kuwaelewesha wabunge masuala mbalimbali yaliyomo katika muswada, ili hata wanapoupitia wawe na weledi wa kutosha wa kitu wanachotaka kukipitisha kuwa sheria rasmi.
Mchakato mzima wa suala hili umegubikwa na usiri ambao sisi tukiwa wadau wa habari, unatupa wasiwasi na hata kujiuliza una maana gani? Nini kimejificha nyuma ya usiri huu?
Tumesema hapo awali hili si suala la jana wala juzi, tumekuwa tukilipigania kwa muda mrefu. Kwa nini taratibu za kawaida za uwasilishaji wa miswada zisifuatwe ili wadau wote wajiridhishe kuwa sheria itakayotungwa itakuwa na tija na maendeleo kwa sekta yenyewe, wanahabari na Taifa kwa jumla?
Kinachotokea sasa kuhusu haraka na usiri ulioligubika suala hili, wadau wa habari hasa wanahabari wanaweza kusukumwa kuamini kuwa kuna dhamira isiyo njema kwao.
Hofu hii ya wanahabari imeshaanza kujidhihirisha katika mjadala bungeni, baada ya baadhi ya wabunge kufikia hatua ya kuinyooshea kidole Serikali kuwa pengine ina dhamira ya kutaka kuvikandamiza vyombo vya habari kupitia muswada huo.
Hatutaki kuamini kuwa Serikali yetu sikivu na inayoongoza kwa misingi ya kidemokrasia, inaweza kutunga kwa makusudi sheria inayolenga kuvibana vyombo vya habari. Na kama itakuwa hivyo, tunauliza ni kwa masilahi ya nani?
Tunawakumbusha viongozi na watendaji serikalini kuwa Tanzania ni nchi yetu sote, hakuna mtu mwenye haki ya kujiona yeye ni Mtanzania zaidi kuliko wengine au mzalendo kuliko wengine.
Tunatoa tanbihi hii kwa kuwa umejengeka utamaduni wa viongozi serikalini na hata wanasiasa kufikiri kuwa wao ni weledi wa kila kitu kuhusu maendeleo na ustawi wa Taifa hili.
Watu hawa wachache siku zote wanalazimisha maoni, mitazamo na fikra zao vitamalaki hata katika mazingira ambayo umma mpana unaona siyo sahihi tena kwa kuegemea katika hoja zenye mashiko.
Matokeo ya utamaduni huu wa wachache kujiona ndiyo wenye uwezo wa kufikiria kwa niaba ya wengine, tuliyaona wakati wa mchakato wa Bunge Maalumu la Katiba wakati wanasiasa walinyofoa mambo mengi yaliyopendekezwa na wananchi, wakapendekeza wanayoyataka wao. Mwishowe mchakato huo umegawanya nchi.
Na ndio maana tunasema muswada huu hauna udharura wowote, kwanini uwe siri? Urudishwe kwa wadau wauone ili kuzuia mgawanyiko mwingine.

Post a Comment

 
Top