0
 
Dar es Salaam. Mbunge wa Lindi Mjini, Salum Barwany amemwomba Rais Jakaya Kikwete kusaini hukumu ya kunyongwa hadi kufa inayowakabili watu wanne waliopatikana na hatia ya kumuua mtu mwenye ulemavu wa ngozi.
Mahakama Kuu, mwishoni mwa wiki iliwahukumu kifo watuhumiwa hao baada ya kupatikana na hatia ya kumuua Zawadi  Magindu (32).
Akizungumza na Mwananchi, Barwany alisema imekuwa ni jambo la kawaida kwa adhabu hizo kutolewa, lakini utekelezaji wake umekuwa mgumu.
“Ningemwomba Rais kabla hajamaliza muda wake, achukue hatua ambayo itamfanya akumbukwe siku zote. Katika jambo kubwa kama hili,  ni vyema akaweka saini ili hukumu hii itekelezwe,” alisema Barwany.
Kwa upande wake Mbunge wa Viti Maalumu anayewawakilisha watu wenye ulemavu wa ngozi bungeni, Al-Shaymaa Kwegir alisema adhabu hiyo ni sahihi kwa kuwa wahusika walionyesha kukusudia kuua.
Alisema amefarijika na adhabu hiyo kali ili iwe fundisho kwa wengine wenye nia ya kufanya uhalifu kama huo.
“Kwa upande wangu, naona adhabu iliyotolewa inastahili kabisa, mtu aliyeua kwanini naye asiuawe,” alihoji Kwegyir.
Alisisitiza kuwa kama adhabu hiyo itaendelea kutolewa, vitendo vya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi vitakwisha nchini.
Naye Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu LHRC Kijo Bisimba alisema licha ya kuwa adhabu hiyo inalenga kukomesha vitendo hivyo, lakini inakiuka haki za binadamu.
Alisema kuna haja ya kuangaliwa upya kifungu cha adhabu ya kifo na kuondolewa kwenye sheria na kitumike kifungo cha maisha.
“Kwa kosa walilofanya wanastahili adhabu kubwa ambayo binafsi naona kifungo cha maisha kingewafaa zaidi siyo kunyongwa,” alisema.
Akitoa maoni yake kuhusu adhabu hiyo, Mwenyekiti wa Chama Albino (Tas), Ernest Kimaya alisema majaji wameonyesha kuzingatia sheria na kusisitiza utekelezaji ufanyike haraka.
Kuhusu kuzichapa Ikulu
Katika hatua nyingine Kimaya amezungumzia vurugu zilizoibuka juzi kwenye Viwanja vya Ikulu baada ya watu wenye ulemavu wa ngozi kumtuhumu kuonana kinyemela na Rais Jakaya Kikwete.
Kimaya alisema vurugu hizo zilisababishwa na baadhi yao ambao hawakuelewa utaratibu. “Ule haukuwa mkutano wa hadhara, Rais alitaka kukutana na viongozi wa chama Taifa, lakini tulishangaa kuibuka kundi kubwa,” alisema.CHANZO:MWANANCHI

Post a Comment

 
Top