Dodoma. Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Conchesta Rwamlaza,
amedai kuna minong’ono kuwa askari wa usalama barabarani hupangiwa
kiwango cha kukusanya na kuwakilishwa kwa viongozi wao na hivyo
kuwafanya kujali zaidi fedha kuliko kusimamia sheria za barabarani.
Akiuliza swali bungeni leo, Rwamlaza alihoji serikali inasemaje kuhusiana madai hayo.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Mambo ya
Ndani, Pereira Ame Silima, alisema Sheria za Usalama wa Barabarani namba
67 ya mwaka 1973 inatoa mamlaka kwa askari wa barabarani kutoza faini
za papo kwa papo kwa makosa mbalimbali ya usalama wa barabarani.
“Hili ni moja ya jukumu la msingi la kikosi cha
usalama wa barabarani unaolenga kuimarisha usimamizi wa Sheria za
Usalama wa Barabarani,”alisema.
Alisema ukamataji wa makosa ya barabarani na faini
ya papo kwa papo hulenga katika kuwatia hofu ya adhabu madereva
wakorofi hivyo kuwafanya wafuate sheria na kanuni za usalama barabarani.
“Hakuna kiwango cha pesa ambacho askari wa
usalama wa barabarani amepangiwa kukusanya, askari ameelekezwa kukamata
makosa kwa wingi iwezekanavyo hususani makosa hatarishi kama vile mwendo
wa kasi, ulevi, ujazaji wa abiria na mizigo, uendeshaji wa hatari na
kadhalika,”alisema.
Katika swali la nyongeza, Mbunge wa Viti Maalum ,
(CUF), Mkiwa Kimwaga, alisema askari wa vitochi barabarani wamekuwa ni
kero kubwa kwa madereva.
“Wakati mwingine wanasimamisha magari kama sita na wanakwambia kuwa na wewe umekuwa ukiendesha katika mwendo kasi,”alisema.
Alihoji ni lini serikali itanunua vitochi vya
kisasa ambavyo vitatoa na namba badala ya vya sasa ambavyo vinaonyesha
mwendo tu kama walivyoahidi katika bajeti iliyopita.
Akijibu swali hilo, Silima alisema wananchi hawatakiwi kuona kero kwa vitochi kwa sababu viko pale kwa ajili ya kuepusha ajali.
“Fikra kwamba vitochi ni kero mziondoe kabisa, tunakerwa ili tusife tunataka maisha yenu yaendelee,”alisema.
Alisema ajali nyingi zinazotokea nchini
zinasababishwa na mwendo kasi. Hata hivyo, alisema serikali imeshanunua
baadhi ya kamera za kisasa zinazoonyesha namba za gari.Alisema kuwa kamera hizo zinaweza kurekodi namba na mwendo na kesho yake dereva akaelezwa makosa yake.
CHANZO:MWANANCHI
CHANZO:MWANANCHI
Post a Comment