KAMUSI YA KISWAHILI SANIFU
MAENEO YENYE WASEMAJI WA LUGHA YA KISWAHILI
Baada ya kutafakari juu ya matumizi yasiyo sahihi ya lugha yetu ya Kiswahili, hivi karibuni nilishawishika kuandika ili kutoa mchango wangu kuhimiza matumizi ya lugha yetu kila mahali.
MAENEO YENYE WASEMAJI WA LUGHA YA KISWAHILI
Baada ya kutafakari juu ya matumizi yasiyo sahihi ya lugha yetu ya Kiswahili, hivi karibuni nilishawishika kuandika ili kutoa mchango wangu kuhimiza matumizi ya lugha yetu kila mahali.
Bado kila ninapopata nafasi nafuatilia kwa karibu
kuona namna ambavyo wasomi na viongozi wetu na waigizaji wa michezo ya
filamu wasivyoienzi lugha yetu.
Katika kituo kimoja cha televisheni hivi karibuni,
Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), walikuwa wakitoa maelezo
ya namna wanavyofanya shughuli zao.
Kilichonivutia ni kwamba miongoni mwa watumishi wa
taasisi hiyo ya umma wamo wageni kutoka nchi zilizoendelea. Mmoja kati
yao ni Fritz Raifmakers.
Raifmakers alinikosha kwa namna alivyozungumza kwa
kutumia lugha yetu kwa ufasaha, ukweli alinifurahisha. Bila kuchanganya
na Kiingereza pamoja na yeye binafsi kutoka moja ya nchi za Ulaya.
Ukweli si yeye tu, nafahamu wapo wazungu wengine wengi ambao kwa kweli
hukizungumza Kiswahili sanifu na kwa ufasaha mkubwa.
Baadaye, ofisa mwingine wa PPRA ambaye ni mswahili
mwenzetu, kama kawaida ya wasomi wetu, ilipofika zamu yake hali
ilibadilika ghafla, alikipa kisogo Kiswahili.
Tuangalie mfano mwingine. Bila shaka wengi
tunafuatilia mfululizo wa tamthilia ya Kichina inayoendelea katika Kituo
cha Televisheni ya Taifa (TBC1) inayoitwa Maudodo na wakwe zake.
Ukiifuatilia tamthilia hii inafurahisha.
Kwa nini? kwanza hadithi yenyewe, lakini la pili
ambalo ndilo ningependa mlizingatie zaidi ni namna lugha yetu
inavyotumika vizuri.
Tamthilia ile inakitangaza Kiswahili sanifu vizuri
na kwa ufasaha. Ikumbukwe Wachina ni zaidi ya robo ya idadi ya watu
wote duniani. Hii ni idadi kubwa mno ikilinganishwa na ya watu wote
wanaozungumza lugha ya Kiswahili duniani kote ambayo inakadiriwa kufikia
zaidi ya 150 milioni. Wachina wakiwamo.
Hii maana yake nini? Tutafakari kidogo. Tuna
uhusiano mzuri na wa karibu na China. Na wao wana mikakati mikubwa na
mingi ya kuwekeza nchini kwetu. Hivi tunavyoongea idadi ya Wachina
nchini kwa tathimini ya haraka inaweza kuwazidi wageni wengine wote kwa
pamoja. Acha wale wazungu wanaokuja nchini kama watalii.
Fikiria zaidi, itakuwaje miaka 20 ijayo kwa
Wachina hawa wanaojifunza lugha yetu kwa bidii? Watanzania kwa takwimu
ya idadi yetu ya hivi karibuni tunakadiriwa kufikia milioni 45. Idadi ya
watu duniani kwa sasa inakadiriwa ni zaidi ya 6 bilioni ambayo, kama
nilivyosema hapo awali, zaidi ya robo ni Wachina.
Kwa hesabu za haraka, wanakaribia bilioni 2.
Linganisha na idadi yetu! Hii ina maana kwamba si muda mrefu Wachina
wanaozungumza lugha yetu kwa ufasaha watakuwa wengi. Sisi tunaendelea
kudandia lugha za wenzetu tena bila ya ufasaha wowote.
Faida kwa nchi yetu hapo ni kwamba lugha yetu itakuwa imepata na
kuongeza idadi ya wazungumzaji wake. Hiyo ni neema maana itatusaidia
kujenga hoja kwenye vyombo vya uamuzi duniani kuifanya lugha ya
Kiswahili kuwa moja ya lugha ya mawasiliano kwenye mikutano yake.
Wasanii ovyo
Wasanii nchini ni moja ya makundi makubwa katika
jamii yetu. Ni kundi linalokua kwa kasi, hivyo linahitaji kuelimishwa
kuwa lina wajibu mkubwa wa kuzingatia matumizi sahihi na sanifu ya lugha
yetu ya Kiswahili.
Waigizaji wengi wetu hawakufanya vizuri shuleni,
walishindwa. Ukifuatilia wengi walifanya vibaya kama sio kufeli somo la
Kiswahili.
Vijana wetu leo hawajui Kiswahili wala Kiingereza.
Matokeo yake, wanaishia kama wasomi wetu wengi hapa nchini,
kuchomekachomeka maneno ya Kiingereza ambayo nayo wakati mwingine wala
sio mahali pake, achilia mbali neno hilo kuwa sahihi au kukosewa
kisarufi.
Hata hivyo, bado yapo matumaini mahali fulani.
Nikirejea tena TBC1, kuna mfululizo wa tamthilia inayorushwa na kituo
hicho cha Taifa, inaitwa ‘Siri ya mtungi’. Yenyewe bahati nzuri
imeigizwa na wasanii wetu hapa nyumbani. Igizo lile limeigiziwa mjini
Bagamoyo. Si nia yangu hapa kuilezea tamthilia hiyo, ila lugha
iliyotumika ni fasaha, wengine waige.
Kukua kwa Kiswahili
Nafahamu na kukubali kuwa Kiswahili kinakua. Swali
la kujiuliza kinakuaje? Kwa mfano, mimi siwezi kukubaliana na wale
wanaodai kuwa kutohoa maneno ya Kiswahili kutoka lugha za wenzetu nako
ni kukua kwa lugha yetu, si sahihi. Kwa nini tutohoe na maneno mengi
tunayo?
Tujadiliane, kukuza lugha ni kufanya nini hasa?
Kukua kwa lugha yetu kwa tafsiri sahihi, maana yake ni kupata neno jipya
lenye asili ya moja na jamii zetu za Kitanzania na kuliingiza kwenye
matumizi ya lugha yetu moja kwa moja. Mifano iko mingi, neno ‘kyenda’
lenye asili ya Uchaga, lina maana ya namba tisa. Ni miongoni mwa maneno
yanayoongeza idadi ya maneno tuliyonayo ya Kiswahili. Huku ndio kukuza
lugha yetu. Yapo mengi. Lakini kuna yale ya Kiswahili chenyewe ambayo
hatuna utamaduni wa kuyatumia kabisa ambayo mara yanapotumika uonekana
kama maneno mageni sana, kumbe sivyo.
Wakati Mwalimu Nyerere alipoamua kupumzika,
aliwaambia Watanzania ‘nang’atuka’. Wengi wetu tulilisikia kama neno
jipya kabisa. La hasha, ni kwamba halikuwa likitumika tu mara nyingi.
Nihitimishe kwa kuwaomba Watanzania wenzangu kukitumia Kiswahili vizuri
mahali popote wanapozungumza na hadhira yoyote ile ili wale
wasiokifahamu sawasawa wapate jukumu la kukitafuta na kujifunza kwa
bidii zaidi.
Post a Comment