0

Walemavu hao wa ngozi wakilia mbele ya kaburi la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.
WATU wenye ulemavu wa ngozi, ambao ni wanachama wa Chama cha Maalbino Mkoa wa Mwanza, wakiwa na wanaharakati wengine, mwishoni mwa wiki iliyopita walitembea kwa miguu kutoka jijini humo hadi Butiama, liliko kaburi la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na kuangua kilio cha nguvu, wakilalamika kutotendewa haki ndani ya nchi aliyoiacha salama.Akizungumza na gazeti hili kiongozi wa wanaharakati hao, Nkwenge Mutash alisema safari yao ilianza Machi 13- 18, 2015 na walitumia siku tano ili kufikisha ujumbe wao wa kupinga mauaji ya Albino na alitoa shukrani kwa wanavijiji waliowaunga mkono wakiwa njiani kwa kuwapa maji, chakula na mahitaji mengine muhimu.
Wakiwa njiani, wanaharakati ambao wengine walikuwa ni pamoja na Khalid Seremani, Michael Athanas na Erick Mutta, walitembelea kituo cha kulelea watoto wenye ulemavu wa ngozi kinachomlea Zakaria Mayala ambaye aliondolewa nyumbani kwao Simiyu ili kumuepusha na hatari ya kuuawa.
Mwenyekiti wa chama hicho, Afred Kapole alisema waliamua kwenda Butiama kwa hayati Baba wa Taifa ili kufikisha kilio chao kwa kulia kaburini mwa muasisi wa taifa ili awasaidie kwani enzi za uhai wake alipenda haki, usawa, upendo na amani, kwa vile hivi sasa wanaona hawatendewi haki katika nchi iliyoachwa ikiwa na misingi ya upendo na amani,” alisema Kapole.
...Wakiwa kwenye picha ya pamoja.
Chifu wa kabila la Wazanaki, Japhet Wanzagi Nyerere aliyewapokea huko Butiama, alisema wageni hao walikuja na kwenda kulia kaburini kwa Nyerere, kiasi kwamba yeye kama binadamu amepata simanzi kubwa hasa walipolalamikia kuhusu kunyanyaswa katika nchi yao na hivyo akatoa wito kwa serikali kufanya kitu ili kurudisha imani ya watu hao mioyoni mwao.
Aidha chama hicho kimeomba kama amani kwao imeshindikana nchini Tanzania, basi wanaomba wahamishiwe katika nchi nyingine.

Post a Comment

 
Top