0
 
Kwenye toleo letu la jana, ukurasa wa tatu tulikuwa na habari iliyokuwa na kichwa kisemacho “Repoa: Takukuru ilikithiri kwa kupokea rushwa 2014” iliyotokana na matokeo ya utafiti uliofanywa na Taasisi ya Afrobarometr ya Dar es Salaam.
Katika utafiti huo, imeonekana kuwa Takukuru, ambayo inahusika na kuzuia na kupambana na rushwa, ilikuwa moja ya taasisi 10 zilizoongoza kwa vitendo vya rushwa. Baadhi ya taasisi hizo ni Jeshi la Polisi, ambalo lilishika namba moja, Mamlaka ya Mapato nchini (TRA), majaji na mahakimu, maofisa wa serikali za mtaa na kwa kiasi fulani Ikulu.
Kutajwa kwa taasisi hizo kunatia shaka jitihada ambazo Serikali imekuwa ikisema inazifanya kupambana na rushwa kama ni za dhati. Kama rushwa ndani ya Jeshi la Polisi haionekani kupungua kwa kiwango kikubwa, wananchi wategemee nini?
Kama rushwa inazidi kujichimbia kwenye taasisi kama TRA, kuna uwezekano wa wananchi kuwa na maisha bora ambayo yaliahidiwa na Serikali ya Awamu ya Nne? TRA kuhusishwa maana yake ni fedha nyingi ambazo zingeingia serikalini, zinakwenda kwa watumishi hao. Serikali itapata wapi nguvu za kuwapa wananchi wake huduma muhimu kama fedha ambazo zingelipwa kodi, zinaingia mifukoni mwa wafanyakazi wa TRA?
Kama majaji na mahakimu wametajwa, wananchi watapata wapi haki ?
Japokuwa imekuwa ni kawaida polisi kutajwa kwenye tafiti mbalimbali kuwa inaongoza kwa vitendo hivyo vya rushwa, lakini matokeo haya ya Afrobarometer yanastua kwamba rushwa inazidi kutapakaa kwenye sehemu zote muhimu kwenye nchi ambayo raia wake bado wanaishi kwa kipato kilicho chini ya Dola moja (Sh1,830) kwa viwango vya kimataifa.
Kutajwa kwa Takukuru kuwa miongoni mwa taasisi zinazoongoza kwa rushwa, kunakatisha tamaa zaidi kwa kuwa ndiyo inaonyesha ni kwa kiasi gani vita vya kupunguza tatizo hilo, ambalo ni kero kubwa kwa wananchi, haiwezi kufanikiwa.
Kama rushwa imeingia hadi Takukuru, kuna haja gani ya kusikiliza kilio chao kwamba taasisi hiyo ipewe meno ili iweze kushughulikia watu inaowakamata kwa tuhuma za kuhusika na vitendo vya rushwa?
Kwa maana nyingine, kama Takukuru itapewa meno hayo, kuna uwezekano mkubwa kwamba watu wengi wakabambikiziwa kesi za rushwa kwa lengo la kuwatisha watoe fedha ili wasipelekwe mahakamani.
Au kwa maana nyingine, hata wananchi raia wema ambao wangetaka kutoa ushirikiano kwa Takukuru katika kubaini vitendo vya rushwa vinavyohusu watu wenye fedha, maisha yao yatakuwa hatarini kwa kuwa ni vigumu kwa wafanyakazi wa taasisi hiyo kumsikiliza maskini mzalendo anayetoa taarifa za tajiri mtoa rushwa.
Pia, ina maana kwamba kila kitu kinachotakiwa kifanywe kwa kufuata sheria na taratibu, kinaweza kukiukwa kwa sababu tu hakuna chombo madhubuti cha kupambana na rushwa, na matokeo yake ni nchi kuelekea kusikofikirika.
Taasisi kama Takukuru ambayo imepewa jukumu la kuzuia na kupambana na rushwa, haitakiwi iwe na hata chembe ya harufu ya rushwa ili kujenga imani kwa wananchi, ambao wanashindwa kupata huduma bora za hospitali, maji, elimu na nyingine kutokana na kukithiri kwa rushwa.Rai yetu ni kwa wahusika kuisoma ripoti hiyo na kuifanyia kazi kubaini ni wapi hasa taasisi hii imepotea ili pafanyiwe kazi na pili kusaka wote ambao wameifanya taasisi hiyo iingie doa na kuwshughulikia kwa mujibu wa sheria ili iwe onyo kwa wengine wanaojaribu kujiingiza kwenye rushwa.{source:mwananchi}

Post a Comment

 
Top