0

Katibu wa Jumuiya na Taasisi ya Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda.
Shahidi wa kwanza katika kesi inayomkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi ya Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda, (pichani) aliyekuwa Mkuu wa Polisi wilaya ya Morogoro, Sadick Tindwa, amedai kuwa alitoa kibali cha kufanya kongamano kwa sharti la kutokashfu dini nyingine.
 
Akiongozwa na wakili wa Serikali, Benard Kongola Tindwa, alidai kuwa Julai 31, mwaka 2013, akiwa OCD Wilaya ya Morogoro alipokea barua kutoka kwa Umoja wa Wahadhiri wa dini ya Kiislamu, wakiomba kufanya kongamano la siku kuu ya Iddi pili katika uwanja wa Shule ya Msingi Kiwanja cha Ndege, Manispaa ya Morogoro Agosti 9, 2013.
 
Mbele ya Hakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Morogoro, Mery Moyo, Tindwa ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Polisi wa wilaya ya Handeni, alidai siku ya kongamano akiwa na maafisa wengine wa polisi waliimarisha ulinzi na kuangalia kama masharti yaliyoelezwa katika kibali hicho yanafuatwa.
 
Shahidi huyo alitoa ushahidi wake kwa zaidi ya saa mbili na wakati wote huo, Jeshi la Polisi liliimarisha ulinzi katika viwanja vya mahakama hiyo na kuwadhibiti wafuasi wa Sheikh Ponda, ambao walizuiwa nje ya uzio.
 
 Alidai kuwa wahadhiri mbalimbali walitoa mada katika kongamano hilo na msemaji wa mwisho alikuwa ni Ponda, ambaye alitoa maneno yenye mtazamo ya uchochezi, kashfa na kuumiza imani za dini nyingine kinyume cha kibali kilichotolewa. 
 
Tindwa alinukuu maneno aliyozungumza Sheikh Ponda katika kongamano hilo kuwa ni “Waislamu wenzangu tuiangalie Serikali yetu, wananchi wa Mtwara walikuwa wanadai haki yao ya gesi, lakini wameweza kupata matatizo makubwa ya kupelekewa majeshi kwa sababu tu asilimia kubwa ya wananchi wa Mtwara ni Waislamu,”. 
 
Aliendelea kunukuu “Pia angalieni wananchi wa Loliondo walikuwa wanadai haki yao ya ardhi, lakini hawakupelekewa majeshi kwa sababu asilimia kubwa ya wananchi wa Loliondo ni Waskristo, pia Kamati za Ulinzi na Usalama za dini zimeundwa na Bakwata pamoja na Serikali kwa manufaa yao binafsi, hivyo kamati hizo zikija katika misikiti yenu kujitambulisha wafungieni milango na madirisha kisha muwapige sana,” alinukuu.
 
 Alieleza kuwa kwa taratibu za Jeshi, alilazimika kumueleza Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro wakati huo, Faustine Shilogile, juu ya kauli hizo na alipewa maagizo ya kumkamata  Sheikh Ponda na kumfikisha katika kituo kikuu cha Polisi.
 
 Alidai kuwa hakumkamata kutokana na wingi wa watu waliokuwapo kwenye kongamano hilo kutokana na kuzingirwa na wafuasi wake na kuondoka naye kusikojulikana.
 
Kesi hiyo inatarajiwa kuendelea leo kwa mashahidi wengine kutoa ushahidi wao.
 
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment

 
Top