0

Dar es Salaam. Shirikisho la Soka Tanzania (TFF)limesema kuwa litaichukulia hatua za kinidhamu Yanga iwapo itabainika kuwa ilivunja kanuni za Ligi Kuu katika michezo yake miwili iliyopita dhidi ya Simba na Stand United.
TFF imeeleza hayo kutokana na kitendo cha mabingwa hao wa kihistoria wa taji la Ligi Kuu, kutoingia kwenye vyumba vya kubadilishia nguo katika mechi hizo mbili zilizochezwa Dar es Salaam na Shinyanga katika kile kinachohusishwa na imani za kishirikina.
Ofisa wa Bodi ya Ligi wa TFF, Joel Balisidya alisema kuwa kikao cha kamati ya nidhamu cha TFF kitakaa katika tarehe ambayo itatangazwa hapo baadaye ili kupitia ripoti ya mechi hizo mbili, kabla ya kuangalia adhabu gani ambayo Yanga watapewa iwapo walikiuka kanuni zinazoendesha ligi.
“Kanuni za ligi ziko wazi kuwa iwapo timu imegoma bila sababu maalumu kuingia kwenye vyumba vya kubadilishia nguo, adhabu gani inatakiwa itolewe. Hivyo, kama shirikisho tutakutana na kupitia vifungu vinasemaje na tutatoa adhabu kama tukibaini uvunjifu wa kanuni hizo,” alisema ofisa huyo.
Hata hivyo, alipotakiwa ataje tarehe ambayo kikao hicho kitakaa, Balisidya alisema yeye hana mamlaka ya kupanga lini kamati hiyo itakaa hivyo wafuatwe wahusika halisi.
Katika pambano dhidi ya Simba na lile  la Stand United , Yanga iligomea kuingia kwenye vyumba vya kubadilishia nguo.MWANANCHI

Post a Comment

 
Top