Siasa kwa maelezo makini na mafupi ni:
“…Itikadi inayofuatwa na kundi au jamii fulani,
ambao ni msingi wa kuendesha uchumi wake; utamaduni na mwenendo mzima wa
maisha ya jamii hiyo; mfumo wa mawazo yaongozayo utawala wa Serikali ya
nchi. Pia ni utaratibu wa utekelezaji au uendeshaji wa jambo kwa
kutumia busara na hekima ili kufikia lengo tarajiwa sawia.”
Tuliokuwepo enzi hizo, sasa tunayo fursa nzuri ya
kulisemea jambo hilo ‘siasa’, hata kuchanganua tofauti zake kwa nyakati
husika. Siyo lazima uitwe mwanasiasa ili kuweza kuona tofauti ya jambo
lenyewe, bali akili na hekima zako timilifu unayaweza hayo.
Wapo baadhi ya watu katika jamii, wenye kuielezea
siasa kama ifuatavyo. Mtu mmoja alisema hivi; “…Siasa za sasa ni za
kuchumia tumbo, yaani za kuganga njaa.” Mwingine alisema; “…Ukijua
kujikomba au kujipendekeza kwa viongozi wakubwa walioko madarakani, hata
kwa jambo lisilo na mashiko ama la kijinga, basi na wewe utakuwa
mwanasiasa na utafanikiwa kupanda juu, hata ukiwakejeli watu.”
Naye J.J Kizibo wa Mikwamba Muheza (jina siyo
lake) alisema; “siasa za kweli zilikuwepo kabla ya Uhuru wetu na miongo
miwili iliyofuatia, ila hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na
baadhi ya viongozi aliokuwa nao awali wao wameondoka na ‘siasa’ za
kweli”.
Francis Chandima wa Handeni amesema hivi; “...Hapa
hakuna siasa bali ni sarakasi za siasa, hivi tumwombe Mungu kwa kiasi
gani ili atuondolee huu utoto, ujinga na kejeli za siasa kwa taifa na
wananchi wetu kwani matarajio endelevu ya nchi yetu yanatoweka.”
Sarakasi za siasa
Zipo, kwani sarakasi imeelezwa kuwa ni; “…Michezo
ya kistadi ya kuonyesha vitendo visivyo vya kawaida na vya ajabu; kama
vile tembo kupanda baiskeli, nyoka kacheza muziki wa kwaito; au mtu
kawatukana wengine, lakini anaowafurahisha wanasema; “…Kajibu mapigo,
hivyo yuko sawa tu.” Siasa hizi za sarakasi ni upuuzi mtupu na
wanaozishabikia ni wenye mrengo wa kitoto wenye kutia kichefuchefu.
Baadhi ya viongozi wetu wa siasa wanafanya mambo
mengi yaliyo nyeti ‘ndiyo sivyo’ na kutulazimisha ati tuyaone kuwa ni
kwa maendeleo yetu. Siyo kila mtu ni punguwani au hamnazo, jinsi
wanavyotufikiria wao baada ya kuingia madarakani; bali wao ama wengi wao
ndio ‘mwapuza’.
Angalia sarakasi ya ufujaji pesa wa IPTL na Escrow
zinazohusishwa na wahisani kutukatia laini kwenye pesa za kuboresha
bajeti yetu ya 2014-2015. Hivi inaingia akilini kuwa viongozi wetu wakuu
kushindwa kupata hesabu au ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
(CAG) na Takukuru mapema tangu lilipotamkwa ‘zengwe’ hili?
Spika alalama
Tumesoma magazetini kwamba Spika akipiga yowe,
‘Hakuna posho za wabunge’. Mbona hapigi yowe kuwa hakuna pesa kwa
mahitaji ya kukidhi maisha ya wananchi?
Wanajamii tunaambiwa wabunge wanapostaafu wanaishi maisha duni.
Tuwaelewaje wakati nyumba tatu za maspika wawili zinakula mabilioni ya
pesa ile ya Anne Makinda na mbili za Samuel Sitta, nao wabunge wanakaa
kimyaa! Au ni ngoma ya jirani?
Sarakasi ya tatizo la maji haliishi, mara mitambo
mipya inafungwa Ruvu Juu, Ruvu Chini, mara mambomba makubwa yanatandikwa
Boko mara Bunju; na mgawo na ukame wa maji uko palepale. Richmond
kaondoka mdogo wake Dowans kalamba dume Mahakama ya kitaifa, analipwa
mabilioni ya shilingi na ndugu yao Symbion kapata kazi na umeme ni mgawo
vilevile; na kutuunguzia vifaa vyetu majumbani. Sababu za utetezi hata
hazikidhi. Kweli ‘nyoka kacheza muziki wa kwaito’.
Kwa mfano wa wazi tumeambiwa tulikuwa na tembo
142,000 Serikali hii ilipoingia madarakani, lakini sasa tuna tembo
55,000 na papo hapo viongozi wanajitetea hakuna ujangili mambo yako sawa
wameyadhibiti, wanajamii wanajiuliza vipi? Taifa linapata sifa mbaya ya
ujangili na rushwa nje ya nchi imeripotiwa na shirika la kimataifa la
uchunguzi huo. Pia, Waziri Membe kwa majibu mepesi anatuambia hizo ni
taarifa za mpitanjia tu pale Mwenge kwenye mabanda yauzwayo vinyago. Je,
na ile orodha ya majina ya wahusika wakuu na vigogo wa ujangili na bosi
wao wa Arusha imefanywa nini? Mbona kimya?
Miaka ya nyuma tuliambiwa wakazi wa Mwanza
wanakula makapi ya vichwa vya samaki sangara, viongozi walibisha hadi
ilipothibitishwa uuzwaji haramu wa samaki hao nje ya nchi.
Aibu tupu! Ni kweli tuko katika sarakasi za siasa
na viongozi ni wepesi wa kukana kila jambo na kukashifu hao wapinzani
hata kwa matukio ya wazi yaani wanatufanya wanajamii wote vipofu na
viziwi. Rai yangu, tuwalipe Bohari Kuu ya Dawa (MSD), ingawa tumelipana
‘kiinua mgongo’ kwenye Bunge Maalumu la Katiba, ili nao wanajamii
maskini wapate dawa.MWANANCHI
Post a Comment